Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Martin Alexander Mtonda Msuha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbinga Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. MARTIN M. MSUHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante. Na mimi niungane na wenzangu kwanza kutoa pongezi kwa Rais wetu Mheshimiwa Dkt. John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri anayoendelea kuifanya. Pia nichukue fursa hii kuwapongeza Mawaziri wote na hususan Waziri wa Kilimo na Naibu wake kwa uwasilishwaji mzuri wa bajeti ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi uliofanyika leo asubuhi. (Makofi)
Mheshimwa Mwenyekiti, lakini pia kwa vile ni mara yangu ya kwanza na mimi kuchangia, nichukue fursa hii kuwashukuru wapiga kura wangu wa Jimbo la Mbinga Vijijini kwa kuniamini na kunituma niwe mwakilishi wao. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakuwa na mchango kwenye eneo moja tu la kilimo kwa sababu tunavyoongelea Jimbo la Mbinga Vijijini asilimia mia moja wote ni wakulima na nitagusa mazao makubwa mawili. Zao la kwanza ni mahindi ambalo upande mmoja wa jimbo langu wanatumia kama zao la biashara, lakini pia zao la chakula. Kwa kiwango kikubwa pia Jimbo la Mbinga Vijijini tunalima kahawa ambayo ina changamoto nyingi ambazo tumeshazisikia siku nyingi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa mahindi, wakulima wa Jimbo la Mbinga Vijijini wana shida upande wa upatikanaji wa pembejeo kwani zinakwenda kwa kuchelewa na zikifika zinakuwa na bei ya juu ukifananisha na pengine na wauzaji wa rejareja. Kwa hiyo, naomba Waziri aangalie namna ya kuboresha upande huu na pengine ule mfumo wa voucher ni wa malalamiko sana, hauwafikii wakulima wote. Kaya nyingi zinakuwa hazipati huduma hiyo ya pembejeo kupitia mfumo wa voucher. Kwa hiyo, nashauri Waziri mhusika aangalie namna ya kuboresha mfumo wa usambazaji mbolea ili wakulima waweze kunufaika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni soko. Soko la mahindi limekuwa halina uhakika, uzalishaji ni mkubwa lakini uwezo wa Serikali kununua mahindi hayo ni mdogo sana. Kwa hiyo, mahindi mengi yanabaki kwa wakulima na wakati mwingine yanaharibika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ile bei elekezi ambayo inatolewa na Serikali, kwa sababu ya mfumo wa ununuzi wa hili zao la mahindi unapitia kwa mawakala unakuta mkulima hafikiwi na ile bei elekezi ya Serikali. Utakuta mkulima pengine ananunuliwa mahindi yake kwa shilingi 380 au chini ya hapo. Kwa hiyo, ile bei elekezi ambayo Serikali inakuwa imetoa inanufaisha watu wa kati. Kwa hiyo, naomba Serikali iangalie ni namna gani zile bei elekezi ziweze kumnufaisha mkulima moja kwa moja.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tuna uhaba wa wataalam wa ugani. Vijiji vyetu vingi, kata zetu nyingi hazina wataalam wa ugani na hao wataalam bahati mbaya sasa hivi wanaunganisha kazi zote mbili, za mifugo pamoja na kilimo. Kwa hiyo, mara nyingi unakuta kazi wanayofanya ni upande wa mifugo kwenye kilimo wamesahau kabisa kusaidia wakulima.
Mheshimwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba Serikali iangalie mambo mawili kuhusiana na eneo hilo. La kwanza, kwenda kuziba hayo mapengo lakini la pili ikiwezekana kutenganisha kazi za hawa maafisa ugani, anaye-deal na kilimo abaki kwenye kilimo na wa mifugo abaki kwenye mifugo ili wakulima hao waweze kupata huduma kwa kiwango ambacho kinastahili.
Mheshimwa Mwenyekiti, nirudi upande wa kahawa. Uchumi wa wananchi wa Jimbo la Mbinga Vijijini unategemea zao la kahawa. Wakulima wa jimbo hili wamekuwa wakilima zao hili kwa mazoea kwamba tangu enzi za mababu wamekuwa wakilima kahawa lakini kwa kukosekana pia huduma za ugani, uzalishaji unashuka. Wakulima hawapati huduma za kuelekezwa ni namna gani wanaweza kuzalisha kwa tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ni mzigo sana kwa wakulima hawa wa kahawa wa Jimbo la Mbinga Vijijini ni utitiri wa tozo, kuna tozo zipatazo 36 kwenye zao la kahawa. Mwisho wa siku unakuta mkulima bei anayopata inakuwa haimpi motisha kwa sababu ya hizi tozo. Nimuombe Mheshimwa Waziri anayehusika aangalie tozo hizi. Kuna tozo moja ya ugonjwa wa vidung‟ata. Ugonjwa huu ulikuwa ni wa mlipuko, lakini baadaye ulikuja kudhibitiwa. Hata baada ya ugonjwa huu kudhibitiwa wakulima wale wameendelea kukatwa tozo hii mpaka leo. Kwa kweli tozo hii ni kero sana kwa wakulima wa kahawa Wilayani Mbinga. Naomba Waziri mhusika atakapokuwa anapitia tozo mbalimbali kwenye zao la kahawa Mbinga, hii naomba iwe tozo la kwanza kuliangalia namna ya kuliondoa kwa sababu ni kero ya kwanza kwa wakulima wa Mbinga. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna tatizo la ushirika. Vyama vingi vya ushirika vya msingi Wilayani Mbinga havikopesheki kwa sababu ya mzigo wa madeni. Kwa vile vyama vya ushirika haviwezi tena kuhudumia hao wakulima, wanunuzi wa soko huria wanachukua nafasi hii kuwanyonya wakulima. Wananunua kama mawakala wakati mwingine wanauza wenyewe nje wakati fulani wanakiuzia chama kikuu cha ushirika. Hawa wanunuzi inafika mahali wanatengeneza umoja, wanafanya cartel kwa hiyo, wanavyokwenda wanakwenda na bei zao elekezi, mwaka huu tuanzie hapa na kwa sababu wakulima wanakuwa na shida unakuta wanalazimika kuuza kahawa yao kwa hasara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, pia mfumo wa soko wa uuzaji kahawa kule Mbinga hauko rafiki kwa sababu utakuta kipindi hiki ambacho sio cha msimu hawa wafanyabiashara wa kati wanakwenda kufanya mikataba ya kununua kahawa ikiwa shambani. Inapokuja kipindi cha mavuno, mkulima anavuna, anatoa kahawa kama vile anatoa bure lakini kama haifikii deni wanunuzi hawa wanafika mahali pa kunyang‟anya mashamba ya wakulima. Wakati mwingine wakulima hawa wanabaki kuwa wakimbizi kwenye Wilaya yao. Nashauri Waziri mwenye dhamana na Wizara hii aangalie namna ya kurekebisha hali hii na pengine sasa ule ununuzi wa kwenda kununua zao la kahawa likiwa shambani upigwe marufuku. (Makofi)
Mheshimiwa Mweyekiti, jambo lingine ni kwamba Chama Kikuu cha Ushirika cha Mbinga kilipata matatizo ya kiuchumi miaka ya 1994 mpaka kikaja kikafa baadaye kikaanzishwa chama kingine kikuu cha Ushirika MBIFACU. Hicho chama ambacho kilikufa mwaka 94 kiliacha madeni makubwa kwa wakulima kiasi cha shilingi milioni 424. Wakulima hao walikuwa wanakidai hicho chama cha Ushirika ambacho kilikufa, Serikali iliagiza ukafanyike uhakiki wa madeni haya. Bahati nzuri Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali alitoa taarifa yake mwaka 2013 baada ya kufanya uhakiki wa madeni ya wakulima waliokuwa wanakidai chama hicho madeni yapatayo shilingi milioni 424. Taarifa hiyo imebainisha ni vyama gani vinahusika, lakini pia imebainisha ni wakulima gani mmoja mmoja anahusika kukidai chama hicho. Sasa niiombe Serikali, iangalie namna ya kuwalipa hawa wakulima deni lao.
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini katika kuanzisha Chama Kikuu cha Ushirika cha MBIFACU kuna mali nyingi sana ya Chama Kikuu cha Ushirika kilichokufa ambazo zinashikiliwa na mrajisi. Mali hizo ni majengo lakini yalikuweko magari…
MHE. MARTIN M. MSUHA: Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.