Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niwapongeze Wenyeviti wote wa Kamati kwa kuwasilisha hoja nzuri na zenye tija na Serikali ichukue hoja hizo na izifanyie kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikizungumzia uti wa mgongo wa Taifa hili ina maana umezungumzia kilimo. Naomba niishauri Serikali iwekeze kweli kweli kwenye kilimo kwani ukizingatia zaidi ya asilimia 75 ni wakulima. Kwa hiyo Serikali ipeleke pesa za kutosha katika sekta hii ya kilimo na ukizingatia sekta hii ikikaa vizuri hata vijana wengi hawatakimbilia mijini zaidi ya kubaki vijijini na kuendeleza kilimo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali ihakikishe inaweka miundombinu, hasa kujenga mabwawa ili wakulima walime kilimo cha umwagiliaji. Serikali iongeze Maafisa Ugani katika kila kata na kuwapa vitendea kazi pamoja na kuwashirikisha Maafisa Maendeleo ya Jamii ili waweze kuwapa elimu ya kilimo wananchi waliopo vijijini, ndiyo maana inafikia hatua wanauza ardhi ili wahamie mijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini tukifanya hivyo hawatauza maeneo yao. Pia kuwapatia pembejeo wakulima kwa wakati hata wale wakulima wa mbogamboga na matunda, kwani hii tutakuwa tumeinua kilimo na wakulima hawa watalima kilimo chenye tija na kuongeza mnyororo wa thamani katika mazao yao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Maji; ukizungumzia maji katika nchi hii kila mtu atakuunga mkono kwa asilimia mia moja, lakini yote haya yanafanywa na watendaji wetu ambao si waaminifu katika sekta hii. Kwa hiyo niishauri Serikali kuwe na Mamlaka ya Maji Vijijini kama ilivyokuwa TARURA. Hii itasaidia sana hata wale watendaji wetu wasiokuwa na nia nzuri na nchi yetu hawatapata nafasi tena ya kuchakachua miradi hii ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Lushoto kuna mito mingi sana inayotiririsha maji kutoka milimani na kuelekea baharini, lakini tukitumia kwa kujenga mabwawa hii itasaidia sana kwa wananchi wetu kupata maji safi na salama pamoja na kutunza vyanzo. Hata hivyo unakuta maeneo kama Lushoto kunakuwa na shida kubwa ya upatikanaji wa maji safi na salama na yapo maeneo mengi tu yenye mito na vyanzo vya kutosha lakini mito hii haitumiki ipasavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho, naunga mkono hoja ya Kamati ya Kilimo, Mifugo na Maji.