Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

Hon. Mussa Bakari Mbarouk

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Tanga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Ardhi, Maliasili na Utalii kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Kilimo, Mifugo na Maji kuhusu shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

MHE. MUSSA B. MBAROUK: Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Kamati kwa taarifa iliyosheheni maelekezo, mapendekezo na ufuatiliaji katika mambo mbalimbali yanayohusu ardhi, maliasili na utalii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimefarijika kuona Kamati imefanya ziara katika maeneo mbalimbali katika tasnia ya ardhi, maliasili na utalii na kujionea physically badala ya kukaa katika kumbi na kujadiliana bila kutembelea maeneo husika na mara nyingine hata Mahakama huhamia eneo la tukio. Ningeshangaa kama Kamati isingetembelea na kujionea hali halisi ya sekta ya ardhi, maliasili na utalii hali iliyopelekea kuishauri vema Serikali yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu imejaaliwa mapori na mbuga nyingi za wanyama, lakini ni Watanzania wenyewe wanajihusisha na ujangili na uharibifu wa maliasili zetu. Ushauri wangu, ni vema Serikali ikatoa elimu ya ufahamu kwa wananchi. Wananchi wakipata elimu na uelewa kuwa hata nchi zilizoendelea zilikuwa na wanyamapori na maliasili nyingine lakini kutokana na matumizi mabaya (ujangili) leo nchi hizo wananchi wao wanalazimika kuja Afrika na Tanzania kujionea wanyamapori na vivutio vingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo natoa wito kwa Serikali kuwapatia elimu ya ufahamu na waelewe pato linalotokana na utalii linachangia pato la Taifa. Mfano, ni vivutio vilivyopo katika Mkoa na Jiji la Tanga kama Hifadhi ya Amani, Hifadhi ya Taifa ya Saadani, Fukwe (Beaches) zilizopo Pangani, Magofu ya Tongoni na Amboni Sulphur pamoja na Amboni Caves. Niungane na mapendekezo ya Kamati lakini nashauri kwamba Amboni Caves iongezewe uwekezaji mkubwa pamoja na kupatiwa umeme na tochi zenye mwanga mkali na barabara pia iboreshwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iendeleze mpango wa Kata Mti Panda Mti na iandae utaratibu wa kufanya mashindano ya kupanda miti mijini na vijijini kama inavyofanya nchi ya Malaysia. Nashauri maeneo ya mjini kwa kushirikiana na Halmashauri zote nchini zipatiwe miche ya miti ya matunda ambayo itatoa vivuli, itabadilisha mandhari za miji na itatoa matunda na itatoa kipato kitakachopatikana kutokana na zawadi zitakazotolewa kwa watunzaji wa miti hiyo pia itatoa matunda na wananchi watafaidika na matunda hayo kiafya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Hifadhi za Taifa kuvamiwa na wafugaji. Ni vema Serikali ikajipanga vizuri katika jambo hili kwani imekuwa ni tatizo la Kitaifa kwani wafugaji nao ni Watanzania wanafuga na wanauza mifugo hiyo ndani na nje ya nchi na kuingizia kodi Serikali. Wafugaji wanatoa kodi na tozo mbalimbali katika minada kwenye Halmashauri zenye wafugaji. Serikali itoe elimu kwa wakulima na wafugaji na kuwapangia maeneo ya kulishia mifugo na maeneo kwa ajili ya kilimo. Pia maeneo yenye Hifadhi na Mapori Tengefu, yawekewe alama maalum na zitambulishwe kwa wananchi wetu (wakulima na wafugaji). Tukumbuke ardhi haikui na watu wanaongezeka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, migogoro ya ardhi mijini/ vijijini. If you fail to plan, you plan to fail. Katika Halmashauri zetu nchini 98% kuna migogoro ya ardhi, mingine ni kwa wananchi kutokufahamu lakini mingine inasababishwa na wataalam wa ardhi katika Halmashauri kwa interest zao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya Serikali kutoa shinikizo la kila Halmashauri kuwa na ukanda wa EPZ (Exporting Processing Zone), ardhi za wananchi zimetwaliwa na ama kulipwa fidia ndogo ama kucheleweshwa hadi leo fidia zao hawajalipwa. Mfano, ni katika Halmashauri ya Jiji la Tanga kuna Kata za Donge, Mabawa na Tangasisi na Masiwani Shamba, wananchi bado wanasumbuliwa katika fidia zao. Nashauri Serikali iwalipe wananchi fidia zao kwa mujibu wa Sheria ya Ardhi Na.5 ya mwaka 1999.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mgogoro wa ujenzi wa uwanja ndege. Katika mradi wa upanuzi wa Uwanja wa Ndege Tanga kuna mgogoro wa nyumba kuvunjwa. Zipo nyumba 208 zilizofanyiwa evaluation mwaka 2008 hadi leo fidia haijalipwa. Pia zipo nyumba 802, nazo hazijalipwa fidia lakini zinatakiwa zivunjwe. Hivi ni kwa nini katika miradi lazima tuwatie wananchi hasara. Nashauri Serikali iwe na vision na mission na tulipe fidia.