Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Rwegasira Mukasa Oscar

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Biharamulo Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. OSCAR R. MUKASA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi ya kuchangia na mimi kwenye Wizara hii ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi. Kwanza kabisa namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia uzima, nawashukuru Wabunge wenzangu wote kwa kazi tunayoifanya, nakupongeza Mheshimiwa Waziri kwa kuwasilisha vizuri, ukisikiliza unaona kabisa matumaini kwamba amejipanga kwa maana ya kufikiria na kuweka mkakati, lakini nina haya ya kusema.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sehemu moja ambayo nadhani ni vizuri tuitazame na inaendana kidogo na msemaji aliyetangulia, Mheshimiwa Waziri uangalie pia namna ya kufanya kitu kinaitwa tathmini ya mambo ambayo yanaweza kuwa hatarishi kwenye hii mipango uliyoiweka na mambo ambayo yanawezesha utekelezaji wa mipango uliyoweka, SWOT analysis. Kwa sababu yako mambo ambayo pamoja na mipango mizuri ambayo ukiisikiliza hii hotuba unavutiwa lakini yasipofanyiwa kazi hatufanya lolote kwenye Wizara hii.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi ninavyozungumza wakulima wa Wilaya ya Biharamulo, Ngara na Bukombe na jirani huko kwa sababu wote tunawasiliana wanajiandaa, ni kutengeneza mishale sasa hivi kwa sababu wafugaji tarehe 15/06 wanatoka kwenye hifadhi kurudi huku. Kwa hiyo, haya yote tunayoandaa kama hatukabiliani na mambo haya ambayo ni hatarishi kwa mipango hii ni bora tu tukaongeza bajeti kwenye Wizara ya Mambo ya Ndani ambayo itakwenda kutuliza ghasia kuliko kuweka mbolea na kadhalika. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu limekuwa sasa ni jambo la kawaida, unakumbuka Mheshimiwa Waziri, namuomba anayemsemesha Waziri wa Kilimo atupe nafasi kwa sababu tunaongea mambo makubwa. Mwenyekiti naomba unilinde, naongea na kiti lakini Waziri mhusika asikie.
MHE. OSCAR R. MUKASA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu imekuwa ni kawaida sasa tarehe 27/28 Disemba, sikumbuki exactly tarehe ila wiki ya mwisho ya mwezi wa Disemba, Mheshimiwa Waziri wa Kilimo akiambatana na Naibu Waziri wa Maliasili walikuwa Benako pale mpakani mwa Biharamulo na Ngara kwa sababu tulikuwa tumewaita kwenda kutatua mgogoro kama huo ambao ulikuwa unataka kutokea watu walikuwa wameandaa mishale. Leo pia mimi Mbunge wa Biharamulo badala ya kujadili mkakati sasa najadili namna gani tuzuie mapambano ili baadaye tuje kwenye mkakati, kwa hiyo, hili suala limekuwa la kawaida sasa.
Kwa hiyo, tusipoondokana na hili tunapoteza muda na tunapoteza muda kwa mambo ambayo yako ndani ya uwezo wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nateta na mtu mmoja hapa naambiwa Rwanda ndiyo wanapeleka mzigo mkubwa wa nyama ya ng‟ombe Congo lakini ng‟ombe hao wanatoka Tanzania, Ngara, Biharamulo, Bukombe sasa sisi ni waajabu, wanatushangaa. Kwa hiyo, badala ya kugeuza mifugo hii iwe neema tunaigeuza kwamba ni sehemu ya kuanzisha mapambano kati ya wakulima na wafugaji. Tuondoke hapo ndipo tutaweza kuongea mambo haya kwa maana ya kuweka mikakati na kwenda mbele.
Mheshimiwa Mwenyekiti, leo tunavyozungumza hapa hali huko kwa kweli ni mbaya. Ukizungumza na mfugaji Biharamulo, Ngara, Bukombe sasa hivi hamuwezi hata kuongea lolote ni tarehe 15 imekaribia, tunafanyaje, tuondoke hapo Mheshimiwa Waziri na tunataka tuweke nguvu kubwa kwenye kutatua jambo hili, tumalize tufanye mambo mengine. Wakulima wamechoka, wafugaji wamechoka, Wabunge hatufikirii jambo lingine, unafikiria tu wafugaji na wakulima kila asubuhi, kila jioni. Tunaharibu rasilimali na akili tulizozileta humu Bungeni, tumalize jambo hilo twende kwenye jambo lingine.
Mheshimiwa Mwenyekiti, pembejeo za kilimo. Mwezi Disemba nilikwenda kijiji kimoja kinaitwa Ntumagu kiko Kata ya Nyanza - Biharamulo. Nimefika pale kabla sijaongea ajabu wananchi mara nyingi wanapenda tunazungumza halafu nao wanapata nafasi ya kuzungumza, wakasema leo tunaanza sisi. Wakaniambia wewe bwana tunajua umekwenda shuleni, unasema sijui una digrii ya ngapi, Mkuu wa Wilaya tumesikia ana digrii moja, mbili, Mkurugenzi ana digrii mbili, Bwana Shamba alikuja hapa juzi ametuletea mbegu za kupanda wakati sisi mahindi yameshafika kiunoni naye tunaambiwa ana digrii moja, sasa mna digrii zote hizo lakini hamjui mahindi yanapandwa lini ni nini? Wananchi wanashangaa. Nalo tumelisikia kwenye hotuba lakini limekuwa linasemwa tena na tena hata tukiwa na mipango mikubwa sana huku juu kama yale ambayo ndiyo yanawagusa wananchi hayafanyiki yote haya mengine yanapoteza maana yake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sasa yale mambo yanayogusa wananchi tumetaja la kwanza, vurugu za wakulima na wafugaji zishughulikiwe. Mheshimiwa Maghembe anasema ni tarehe 15 anakwenda kuwatoa wafugaji wote kwenye hifadhi, ni jambo zuri kwa sababu hawapaswi kuwa kwenye hifadhi, lakini si tupange? Mkulima anatekeleza wajibu wake, analima mpunga, mahindi, tunanunua tunakula, mfugaji naye anatekeleza wajibu wake, tukienda butchery pale hatuulizi kwamba naomba kilo tano; mbili za ng‟ombe aliyekula hifadhi halafu tatu za ng‟ombe wa maeneo mengine, hatusemi hivyo. Tunaomba kilo tano tunapewa ametimiza wajibu wake. Serikali yenye wajibu wa kuwapanga ili haya yote yafanyike haitekelezi wajibu wake. Kwa hiyo, tunapoteza muda kufikiria migogoro badala ya kwenda kwenye mambo ya mkakati. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini la pili ni hilo tumesema linagusa wananchi, habari ya pembejeo ambalo tunaomba pamoja na michakato yote zifike kwa wakati. Baada ya kuongea na wale wananchi walioniambia mbolea ya kupandia imefika wakati mahindi yamefika kiunoni nilikwenda kuongea na watu wa Halmashauri, nikakutana na Bwana Kilimo pale. Nilivyomuelezea akanipa story nzuri ambavyo mchakato wa kufikisha hiyo mbolea kwa mwananchi ulivyo, ikitoka hapa inafika pale lakini haya ni maelezo tu, mwananchi hayamsaidii. Kinachomsaidia ni pembejeo kufika kwa wakati ili apande kwa wakati tupate tija.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ukanda wa wafugaji ambao unajumuisha Biharamulo, Ngara na Bukombe na kwingine wana umoja wao. Wakikupa takwimu utashangaa, wanasema kwa wastani kwa mwezi kuna kodi wanailipa kwa njia ya rushwa kwa hao watu wanaowafukuza kwenye hifadhi ya karibu milioni 30 mpaka 50. Kwa hiyo, kodi hiyo hiyo tukitafuta namna ya kuigeuza iwe halali itatusaidia hata kuwapanga hawa, lakini inatoka kwa mwezi na wenyewe wametunza takwimu vizuri kabisa lakini ni kodi ambayo inakwenda kwa njia ya rushwa kwa sababu watu wanatengeneza tu mazingira kwamba leo tukafanye doria, tutaondoka na milioni 30, kesho tukafanye hivi. Kwa hiyo, tutumie rasilimali tuliyonayo kwa njia ambayo inaleta tija ili kodi hiyo hiyo ilipwe kihalali badala ya kulipwa kwa namna ambayo haifaidishi Taifa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, chini ya 30% ya mifugo ya ukanda ule inapata chanjo na hao wafugaji wanasema wao wako tayari hizo huduma zikipatikana wanazilipia tu. Ukiweka mfumo sahihi wa kulipia huduma hizo ina maana una mfumo sahihi wa kuweka takwimu, una mfumo sahihi wa kufuatilia kodi na wao wako tayari kulipa kodi. Hivi tunavyozungumza wafugaji wa ukanda ule wanalipa tu ushuru wa Halmashauri lakini hakuna namna wanalipa kodi ya Serikali Kuu na ukizungumza nao wanasema wako tayari, sasa hiyo potential tunayo mbona hatuitumii? Ukishatatua suala la wafugaji umetatua la wakulima kwa sababu sasa hivi mkulima ambaye angekuwa anafikiria afanyeje kwenye msimu unaokuja anafikiria namna gani atapambana na hawa jamaa watakavyotoka msituni huko kwenye hifadhi tarehe 15/06.
Mheshimiwa Mwenyekiti, hili limekuwa tatizo sugu na sisi wananchi wa ukanda ule tunadhani sasa inatosha. Kwa hiyo, tunamuomba Mheshimiwa Waziri afanye uratibu na Wizara nyingine zinazohusika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, niliwahi kuambiwa siku moja kwamba tunawafukuza hawa wafugaji kwenye hifadhi kwa sababu wako wengine wanatoka Rwanda, sasa hiyo siyo kazi ya mfugaji wa Tanzania kujua kwamba huyu ni wa Rwanda asiwe hapa ni kazi ya Wizara ya Mambo ya Ndani. Kwa hiyo, Waziri wa Kilimo, Waziri wa Mambo ya Ndani na wa Maliasili wakae waseme huyu ni mfugaji wa Tanzania afuge, alipe kodi, awekewe miundombinu lakini unakuta kiongozi anasema kabisa tunawafukuza kwa sababu wako wafugaji wa Rwanda, sasa hii siyo kazi ya mfugaji wa Tanzania.