Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

Hon. Prosper Joseph Mbena

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kwa mwaka wa fedha 2016/2017.

MHE. PROSPER J. MBENA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kutoa maoni na mchango wangu wa mawazo kwenye hotuba ya bajeti hii ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kama ilivyowasilishwa kwetu na Mheshimiwa Mwigulu Nchemba Madelu, Waziri wa Wizara hiyo.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze sana Mheshimiwa Waziri kwa uwasilishaji wake mzuri na hotuba nzuri ambayo imesheheni maeneo yote muhimu ya sekta hii. Pia nimpongeze kwa jinsi ambavyo anajituma katika kufanya kazi zake. Yeye na Mawaziri wengine wamekuwa mstari wa mbele katika kutatua matatizo ya wananchi wetu, nakushukuru na nakupongeza sana Mheshimiwa Waziri. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, naiunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. Ninachokifanya hapa ni ushauri tu katika nia ya kuboresha lakini pia ni mawazo, Mheshimiwa Waziri anaweza kuyachukua na anaweza kuyachuja. Katika bajeti hii ya Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi kama nilivyosema maeneo mengi yameguswa lakini mimi ningependa nione linajitokeza zaidi ufumbuzi wa tatizo kubwa la migogoro kati ya wakulima na wafugaji. Nasema ningetamani nilione hilo limejitokeza kwa sababu kwa kweli kwa sehemu kubwa katika baadhi ya Majimbo langu likiwa mojawapo Morogoro Kusini, migogoro hii inatishia usalama wa wananchi wetu. Wapo walioumizwa, wapo ambao wametengeneza uhasama mkubwa sana na chanzo ni migogoro hiyo. Nafahamu Wizara zaidi ya moja inahusika katika kutafuta ufumbuzi wa jambo hili mojawapo ikiwa ni Wizara hii ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi nyingine zikiwa ni Ardhi na TAMISEMI. Napenda Wizara hizi zote zinazohusika zituonyeshe na kutueleza waziwazi jinsi watakavyoweza kutatua migogoro hii iwe historia, tumechoka nayo. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, ufumbuzi wake uko kwa namna nyingi, moja kiutawala ambayo naamini kabisa Mheshimiwa Waziri anafanya hivyo kwenda kuzungumza na makundi haya lakini lingine kusema ukweli ni la kiuchumi na hapa ndipo napenda Mheshimiwa Waziri ajielekeze zaidi. Mifugo hii imeshaingia hata kwenye maeneo ambayo siyo ya ufugaji. Wakati mwingine kutoa mifugo ile yote ni nadharia, kiutekelezaji ni ngumu. Ufumbuzi wake upo katika kuanzisha viwanda vitakavyoweza kutumia malighafi za mifugo ile kutengeneza bidhaa ambazo zinaweza kuwa nyama za kusindika, ngozi na mifano mingi. Tunaposema uchumi wa viwanda katika eneo hili vielekezwe kwenye maeneo hayo ambayo kwa kweli mifugo tayari imeshakuwa mingi na sasa tunahitaji hata wale wafugaji wanufaike zaidi na mifugo yao. Hii itatupunguzia uhasama kwa sababu sasa wakulima mashamba yao yatakuwa salama na wafugaji watakuwa na mahali pa kupeleka ng‟ombe zao, soko la karibu litakuwa viwanda vitakavyojengwa, hivyo Mheshimiwa Waziri ningependa sana hili lijitokeze. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ni ushauri tu kama nilivyosema na kwenye eneo hili naomba nitumie fursa hii kuwapa pole sana wananchi wangu wa Jimbo la Morogoro Kusini hususani kata zile ambazo zimepata mafuriko makubwa sana, Kata ya Serembala, Mvuha pamoja na Konde. Wananchi wameathirika sana, wamepoteza nyumba zao, mashamba yao, mazao yao yaliyokuwa shambani na mengine nyumbani na kwa kweli mazingira yale ni magumu kwa mtu yeyote. Nawapa pole lakini Serikali inajua, mimi mwenyewe nimelifikisha kwa Waziri anayehusika na naamini ufumbuzi wa kudumu utapatikana. Ikiwezekana na hapa ndipo ninapotaka kuchangia Wizara ione inaweza ikafanya nini kwenye maeneo haya.
Mheshimiwa Mwenyekiti, yapo maeneo Mheshimiwa Waziri ametueleza ambayo yamebainishwa katika mradi ule wa BRN, ni maeneo ambayo yametengwa kwa ajili ya kilimo cha miwa pamoja na mpunga. Katika Jimbo langu yapo maeneo mawili, Kisaki na Mvuha, ni maeneo mazuri kwa ajili ya kilimo cha miwa. Mimi napendekeza liongezwe eneo lingine la tatu lile la Serembala ambalo ni hatarishi kwa wananchi na ni eneo kubwa sana. Wananchi wale wangeweza kutolewa wakapelekwa sehemu iliyo salama kwao ili sasa eneo lile lilimwe miwa, ni eneo zuri sana kwa ukulima wa miwa. Tuondoe tatizo hili kwa wananchi wetu.
Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ambalo nitapenda nilichangie ni lile ambalo wenzangu wamelisema, lakini labda mimi niliseme kwa maana ya kuongezea tu uzito. Miundombinu yetu si rafiki sana kwa wakulima na kwa ajili ya kuongeza kilimo. Yapo maeneo katika jimbo langu yana historia ya kutoa mazao mengi sana lakini hayapitiki kwa barabara kipindi kama hiki na mazao yanaharibika bure. Ni vizuri Serikali ikawa na strategic, yale maeneo ambayo wanajua kabisa kwamba ni potential kwa ajili ya kilimo, mazao yanapatikana mengi watengeneze pia na miundombinu bora na ile ambayo mwaka mzima inapitika ili wakulima kweli waweze kulima. (Makofi)
Mheshimiwa mwenyekiti, pia tupatiwe zana, Mheshimiwa Waziri amesema hapa kuna mpango wa Serikali wa kupata matrekta, nadhani kutoka Poland au kwa kutumia msaada wa Poland, matrekta zaidi ya 2,000, ni jambo zuri. Jimbo langu la Morogoro Kusini linajulikana kwa ukulima hebu tupatiwe hata matrekta 20, tunahakikisha tutalisha sehemu kubwa ambayo wenzetu wanakuwa na upungufu wa chakula mara kwa mara. (Makofi)
Mheshimiwa Mwenyekiti, niunge mkono hoja kama nilivyosema na nakushukuru kwa kunipa nafasi hii, ahsante sana.