Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Bajeti Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017, Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Uwekezaji na Mitaji ya Umma Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Viwanda, Biashara na Mazingira Kuhusu Shughuli za Kamati kwa Mwaka 2017

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii ya Maftaha nami niweze kuchangia. Naomba nianze mchango wangu kwanza kwa kuzishukuru Kamati zote tatu kwa michango yao mikubwa na kuona haya waliyotuletea sisi yanatufaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nitoe angalizo letu moja tu kwamba sisi kama Watanzania ni watu wazuri sana wa kupanga mipango; na mimi ningependekeza tuunde taasisi ya kupanga mipango pengine tukiuza mipango yetu nchi za nje tukapata pesa za kigeni. Kwa sababu tumekuwa wapangaji wazuri sana lakini kwenye utekelezaji tuko zero.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matatizo haya tuliyaongelea wakati tunapanga bajeti hapa, kwamba hizi bajeti hazitoshi kwa maana kwamba hazitakwenda kukidhi matakwa ya kile tunachokitarajia; na hiki ndicho ambacho Wenyeviti wa Kamati wametuletea. Kwa sababu Mwenyekiti wa Kamati amesema kwamba CAG hana resources za kutosha, kwa maana kwamba hana pesa za kutosha kuyaendea majukumu yake na haya tuliyaongea tangu mwanzo kwamba hizi pesa ambazo CAG tunamtengea hawezi kutekeleza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile hata kwenye Kamati zetu za Bunge nazo tumeshindwa kuyaendea majukumu yetu, kukagua miradi iliyopelekewa pesa na Serikali kwa sababu ya tatizo la pesa. Ukienda kwenye halmashauri zetu nako huko watu wenyewe wanakaimu. Sasa ukiangalia bajeti ya Serikali asilimia 70 zinakwenda kwenye halmashauri. Hivi, Waheshimiwa Wabunge kama hawawezi kwenda kukagua miradi, CAG kama hawezi kwenda kukagua hesabu za Serikali, hivi tunatarajia weledi gani tulionao wa matumzi bora, matumizi sahihi ya hizi pesa tunazozipeleka kwenye halmashauri zetu. Hili ni jambo linaloshangaza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niwaambie wenzetu mliopata uteuzi au madaraka ya kuisimamia nchi mtuone sisi nasi ni wazalendo. Hayo tunayoyasema tunasema kwa uzalendo kama ambavyo ninyi mnajiona; kwamba ninyi ni wazalendo zaidi kuliko sisi na ndiyo maana hata tunaposhauri mnatuona kwamba tunashauri kama vile tunawapuuza, lakini tunawashauri tukiwa na nia ile ile kwamba na sisi ni wazalendo na tunashauri kwa uzalendo mkubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nije kwenye viwanda. Hapa tunapigiwa kelele tu kila siku kwamba viwanda vinafufuliwa, lakini sisi watu wa kusini tunalalamika kwamba kulikuwa na viwanda vya korosho kila wilaya, lakini hakuna kinachofufuliwa hata kimoja na vyote leo hii tunaambiwa vilivyo vingi viko kwenye kesi, kwa hiyo haviwezi kufufuliwa viko kwenye kesi tunabaki kuwa maskini. Kama mama yangu alivyokuwa anasema, kwamba sisi tumebaki kama nchi kama vile haina mwenyewe, hili jambo hata sisi linatuumiza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia kwenye uwekezaji sekta ambayo kama kweli Serikali ya Awamu ya Tano kama imeamua kuwekeza kwa ajili ya kumkomboa Mtanzania basi sekta mojawapo ambayo ilikuwa ni muhimu ni sekta ya kilimo; lakini sekta ya kilimo imebaki kwenye makaratasi. Mheshimiwa Waziri wa kwanza wa Wizara hii alisema awamu ya tano tunaweka jembe la mkono litakuwa makumbusho, lakini mpaka leo hii tunafika huko katikati jembe la mkulima bado halijaenda makumbusho na sidhani kama litakwenda makumbusho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini bado hata wale wachache wanaojitokeza kuwekeza kwenye kilimo bado hatuwatendei haki. Mimi hainiingii akilini mtu umewekeza, umelima, umevuna mahindi, inatoka Serikali inasema hayo mahindi usiuze halafu NFRA hawanunui, huyu mkulima amewekeza, kwamba amechukua mikopo benki, anailipaje? Yaani tunategemea mkulima yeye ndiye awe food security unit ya Taifa, hii haingii akilini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii kama tulivyosema, kwa mfano kama sasa hivi korosho ndizo zinazofanya vizuri kwenye soko la kimataifa; lakini hizi korosho ni Mwenyezi Mungu tu katupendelea, Serikali haijawekeza mkakati wowote wa kuendeleza zao hili zaidi ya kwenda tu kutafutia soko hapa Vietnam basi, lakini, hakuna mkakati wowote ule ambao umesimamiwa kwamba Serikali imefanya mkakati huu, zao hili la korosho limefika hapa lilipofika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia, kuna matamko ya viongozi. Naomba hayo matamko ya viongozi lazima yaendane na uhalisia. Tulipokuja kwenye zao la korosho katikati ya msimu tumekuja kuambiwa sulfur itatolewa bure, magunia yatatolewa bure, lakini ukienda kwenye Bodi ya Korosho wanakwambia wao bajeti yao ilikuwa wamesha- order tayari sulfur ya tani elfu tisa, lakini mahitaji halisi ni tani elfu kumi na nane. Sasa tani hizo zingine elfu tisa zinapatikana wapi? Ndiyo maaana sasa hivi kwenye msimu tukahangaika mpaka sulfur ya 35, 000 tumenunua 75,000 lakini lile tamko lilikuja katikati ya mradi. Tunakwenda wapi?

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii hapa Mwenyekiti amesema Kodi ya Korosho mpaka leo hii ile asilimia 65 hawajapata lakini leo hii hawa hawa Bodi ya Korosho sasa hivi wanatakiwa waagize sulfur. Itakapofika mwezi wa Nne mwaka huu sulfur inatakiwa imfikie mkulima lakini mpaka leo Bodi hawajapata hela. Ndiyo maana nikasema hili zao la korosho nalo Mwenyezi Mungu tu kataka ndiyo hapo lilipofikia lakini mkakati wa Serikali sijauona.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukija kwenye uwekezaji wa viwanda vidogo vidogo, kama ambavyo waliotangulia kuchangia walivyosema mimi mwenyewe na-declare interest kwamba na mimi nina kiwanda kidogo cha usindikaji wa nafaka. Mkitaka kujua shida ya nchi hii wewe anzisha kiwanda chako. Atakuja TFDA, atakuja OSHA, atakuja TBS, atakuja bibi afya wa kata, atakuja NEMC, atakuja sijui wa mazingira gani hawa wote wanakuja wanakutafuna, wanakumaliza moja kwa moja, unatamani kwa nini nimeanzisha hiki kiwanda? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa basi hizi taasisi zote basi ziingie kwenye mfumo mmoja, kwamba mtu unakwenda mahali pamoja unalipia hizo taasisi zote, lakini uzunguke leo niende TFDA, kesho niende TBS, kesho kutwa nakwenda OSHA yaani ni vurugu. Kwa kweli…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)