Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

Hon. Vedasto Edgar Ngombale Mwiru

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kilwa Kaskazini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

MHE. VEDASTO E. NGOMBALE – MWENYEKITI WA KAMATI YA KUDUMU YA BUNGE YA HESABU ZA SERIKALI ZA MITAA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kwa kunipa nafasi. Nichukue fursa hii kuwaashukuru wachangiaji wote waliochangia katika taarifa ya Kamati yangu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, taarifa hii ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya usimamizi wa Hesabu za Serikali za Mitaa imechangiwa na jumla ya wachangiaji 22; kati yao saba walichangia kwa maandishi na 15 walichangia kwa maelezo. (Makofi)

Mheshimiwa Bobali alieleza kuhusiana na aina ya Wakurugenzi waliopo na kama wana uwezo wa kusimamia shughuli za maendeleo. Alieleza pia kwamba Wakurugenzi waliopo hawakupatikana katika mfumo wa watumishi wa umma. Pia alieleza kwamba kuna tatizo katika ukusanyaji wa mapato na hili linatokana na kushuka kwa bei ya mazao ya wakulima. Kamati imepokea ushauri huo na Kamati ilitoa mapendekezo katika taarifa ya mwaka jana kwamba Serikali inatakiwa semina kwa Wakurugenzi ili waweze kufanya kazi ipasavyo. Pia Kamati inashauri Serikali kuhakikisha kila Halmashauri inakuwa na mfumo wa kieletroniki ili basi iweze kuongeza mapato ya Halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Bobali pia ameeleza pia kuhusu tatizo la mradi wa maji. Ameeleza kwamba kuna mradi wa vijiji kumi ambao umeonyesha kutofanikiwa kabisa. Kamati imechukua ushauri huo, Kamati imeliona hilo na katika taarifa yake imeeleza na kutoa mapendekezo kwa Bunge kuazimia kuunda kamati teule ya Bunge kuchunguza matatizo ya maji nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Lubeleje ameishauri Kamati kupewa fedha nyingi zaidi ili kuweza kukagua miradi mingi ya maendeleo na hivyo kuona thamani halisi ya fedha zinazotumika. Tunashukuru kwa ushauri huo na katika taarifa yetu tulieleza kwamba tusingeona vizuri kufanya tu kazi ya mezani, ni vizuri tukatembelea miradi ya maendeleo ili kuona thamani halisi ya matumizi ya fedha za Serikali. Pia alieleza suala la watumishi kukaimu kwa muda mrefu bila kuthibitishwa. Kamati nalo katika taarifa yake imeliona hilo na imeitaka Serikali kuhakikisha kwamba watumishi wasikaimu zaidi ya miezi sita, wathibitishwe ili kuleta tija katika utendaji katika Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Chikota ameeleza kuhusu tatizo la kukaimu kwa Wakuu wa Idara na ametolea mfano halmashauri ya Korogwe ambayo kuna wakuu wa idara 11 wanaendelea kukaimu mpaka sasa, lakini pia ameeleza tatizo la miradi ya maji, ameelezea pia kucheleweshwa kupelekwa kwa fedha za miradi ya maendeleo. Taarifa ya Kamati imezingatia hayo yote na tunashukuru Mheshimiwa Chikota kwa ushauri wako.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Selasini ameelezea uwezo wa baadhi ya Wakurugenzi wa Halmashauri zetu, hali ambayo inaleta matatizo na migongano na baadhi ya watumishi.

Suala hili limekuwa likijirudia mara kwa mara na ni kweli Wakurugenzi wengi tulionao sasa hawatokani na mfumo wa utumishi wa umma na hii imeleta tatizo kubwa katika utendaji wa kazi na usimamizi wa shughuli za maendeleo katika Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Gekul yeye alielezea kuhusiana na suala la asilimia 10 ya mfuko wa maendeleo ya vijana na akina mama na alishauri pia hii ihusishe pia wazee. Alieleza pia tukajifunze kutoka Halmashauri ya Babati ambayo imefanikiwa kwa kiasi kikubwa katika kuchangia fedha hizi. Nichukue nafasi hii kuitaka Serikali iende ikajifunze katika Halmashauri ya Babati tuone namna gani wameweza kuchangia pesa za mfuko huu kwa asilimia 100.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Edward Mwalongo alieleza kuhusiana na tatizo la maji, ameeleza kuna tatizo la wakandarasi washauri na miradi mingi ya maji inaharibika mara tu baada ya kuanza kutumika. Tatizo hili sisi kama Kamati tumelieleza kwa kina na kama tulivyoelekeza tunalitaka Bunge liunde Kamati Teule ya Bunge ili kuchunguza matatizo yote ya maji kwa maana kuna tatizo la miradi ya maji karibu nchi nzima. Katika kila miradi tuliokuwa tumetembelea miradi mingi bado haijafanya kazi vizuri. Kuna tatizo kubwa la usanifu wa miradi hiyo kwa hiyo tumeelekeza Bunge liunde Kamati Teule ya Kibunge kuchunguza matatizo ya miradi ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Musa Mbarouk naye pia alieleza tatizo la kukaimu kwa Wakuu wa Idara na Vitengo kwa zaidi ya miezi sita na ucheleweshaji wa pesa za miradi ya maendeleo. Hili nalo tumelieleza vizuri kwenye maazimio ya Kamati yetu na tunaitaka Serikali itekeleze hilo haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Leah Komanya alieleza kuhusiana na kutojibu hoja za ukaguzi na matumizi ya mfumo wa kihasibu wa EPICOR. Mfumo huu hauna asset model, wakurugenzi wanaweza wakajifanyia mahesabu kwa kadiri wanavyotaka; mfumo huu una cash basis, lakini hauna a clause basis na hii kuleta tatizo katika suala zima la mahesabu. Lakini upo uwezekano pia wa kufanya mahesabu nje ya mfumo. Kamati imeshauri Serikali ihakikishe mfumo wa EPICOR unafanyiwa marekebisho, bado kuna tatizo kubwa la mfumo wa EPICOR ambao tunautegemea kwa kufanya mahesabu katika halmashauri zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Conchesta Rwamlaza ameeleza kuhusiana na mfuko wa maendeleo ya wanawake na vijana akasema mfuko huu ni muhimu kwa maendeleo ya wananchi lakini utaratibu unaotumika hauko sawa sawa, vikundi vingine vinavyolipwa pesa za mfuko huu ni vikundi hewa. Pia alieleza kwamba mfuko huu unatumika kisiasa; lakini pia alikubaliana na wazo la Mheshimiwa Zitto. Tumepokea ushauri huu na sisi Kamati tumeitaka Serikali ilete muswada wa sheria kwa ajili ya mwongozo wa matumizi ya mfuko huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Kigua ameeleza kuhusiana na miradi ya maji, lakini ameeleza tatizo la makusanyo ya mapato ya Halmashauri. Kamati imeeleza kwa kina matatizo ya miradi na maji na pia Kamati imeitaka Serikali ihakikishe kila halmashauri inatumia mfumo wa kieletroniki ili kuhakikisha kwamba inaongeza mapato ya Halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Zitto Kabwe alileta nyongeza ya kuiomba Serikali iangalie uwezekano wa kuunda Benki ya Maendeleo ya Serikali za Mitaa kwa kutumia asilimia 10 ya mapato ya ndani ambayo itatekeleza wajibu wa kutoa mikopo kwa vikundi vya vijana na wanawake. Vilevile Serikali itafiti uwezekano wa kuanzisha scheme ya hifadhi za jamii kwenye Serikali za Mitaa ili kusimamia mikopo ya vijana na wanawake. Ongezeko hili Kamati tumelikubali lakini pia kamati tulisisitiza kwamba haya yote yataweza tu kufanyika kama Serikali italeta Sheria ya Mwongozo wa Uendeshaji wa Mfuko huu wa Wanawake na Vijana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Isack Kamwelwe yeye alielezea kuhusiana na matatizo ya maji katika Wizara, akaeleza kwamba Wizara inatoa pesa tu pale ambapo kazi itakuwa imefanyika na Serikali itahakikisha kwamba huduma za maji zinapatikana. Mheshimiwa Waziri nichukue nafasi hii kukueleza kwamba katika ukaguzi tulioufanya tumegundua miradi mingi ya maji haitekelezwi ipasavyo na tatizo kubwa ni kwamba wakandarasi wanavyo- raise certificate Wizara inachukua muda mrefu kutoa pesa hizo na inasemekana ni lazima ukauze sura Wizarani ndipo certificate hizo ziweze kulipwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Mheshimiwa Waziri inatakiwa hili ulifanyie kazi ili kuhakikisha miradi ya maji inatekelezwa ipasavyo. Kamati pia imeliona hilo na kutaka kuundwa kwa kamati teule ya Bunge ambayo itaangalia nini kiini cha matatizo katika utoaji wa huduma ya utekelezaji wa miradi ya maji nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Mpango ameeleza kwamba Serikali inapeleka pesa za miradi ya maendeleo tofauti na tulivyoeleza Kamati. Mheshimiwa Waziri nieleze tu kwamba unasema kwamba Serikali inapeleka fedha za miradi ya maendeleo ipasavyo, lakini fedha hizo hazifiki katika Halmashauri na ndio maana miradi mingi ya maendeleo inashindwa kutekelezeka. Kama fedha hizo zingekuwa zinafika kwa wakati miradi ingekuwa inatekeleza bila matatizo na kusingekuwa na malalamiko yoyote kutoka kwa Waheshimiwa Wabunge na Halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Ndalichako ameeleza utekelezaji wa elimu bure na ameeleze ufafanuzi uliotolewa na waraka, kwa mfano suala la chakula kwa wanafunzi. Mheshimiwa Waziri nieleze tu kwamba kauli iliyotolewa na Mheshimiwa Rais ikikuagiza wewe pamoja na Waziri wa TAMISEMI kwamba kuanzia sasa ikipiga marufuku michango yoyote kwa ajili ya uchangiaji katika suala zima la elimu imeleta mkanganyiko mkubwa. Ipo haja ya kutoa tafsiri sahihi ya agizo la Rais na wakati mwingine inashindwa kueleweka kama je, tufate Waraka au agizo la Mheshimiwa Rais. Sasa ninavyoongea kuna shule nyingi huko zimefungwa na watendaji wa Serikali, wakuu wa shule wanapata shida kubwa ya nini kifanyike katika agizo hilo la Mheshimiwa Rais. Kwa hiyo, nitoe wito kwa Serikali kutoa ufafanuzi wa agizo hili la Rais ili kuepusha mkanganyiko unaoweza kujitokeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Jafo ameelezea kuhusiana na hatua zilizochukuliwa kwa Wakurugenzi ambao wameeonyesha kutokuwa na utendaji mzuri, lakini ameelezea suala zima la ukusanyaji wa mapato ya Halmashauri na pia ameeleza kuna baadhi ya watendaji wamelazimika kulipia hasara walizosababisha na ameeleza pia wako katika vetting kuangalia utendaji wa baadhi ya Wakurugenzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili la kufanya vetting, la kuangalia utendaji wa baadhi ya Wakurugenzi tunaliomba lifanyike kwa haraka kwa sababu wananchi wetu na Halmashauri zetu zinapata shida. Wapo Wakurugenzi ambao mpaka sasa utendaji wao haueleweki na hivyo kurudisha nyuma maendeleo katika Halmashauri zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kuyasema hayo naomba kuchukua fursa hii sasa kueleza azimio kubwa la Kamati ambalo lingependa lifanyiwe kazi kwa haraka ni kuhusu kuundwa kwa Kamati Maalum ya Kibunge itakayochunguza sababu za chanzo la tatizo la miradi ya maji kutekelezwa chini ya kiwango au kutotekelezwa kabisa.

Pia nichukue fursa hii kumshukuru Mheshimiwa Spika, Job Ndugai kumshukuru Katibu wa Bunge Ndugu Stephen Kagaigai, kwa ushirikiano waliouonyesha pamoja na shukrani za dhati kwa Ndugu Athuman Hussein - Mkurugenzi wa Kamati za Bunge, Waziri wa TAMISEMI - Mheshimiwa Jafo na Manaibu wake, Makatibu wa Kamati, Ndugu Dismas Myanjwa, Ndugu Godfrey Kassanga, Ndugu Victor Mhagama pamoja na watumishi wengine wote wa Bunge.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia kwa namna ya kipekee nichukue nafasi hii kuwashukuru na kuwapongeza kwa namna wanavyotoa ushirikiano Wajumbe wote wa Kamati ya LAAC kwa kufanya kazi bila kuchoka kuhakikisha kwamba taarifa hii inakamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naomba kutoa hoja.