Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

Hon. Dr. Mwigulu Lameck Nchemba Madelu

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Iramba Magharibi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

WAZIRI WA MAMBO YA NDANI YA NCHI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kunipa fursa na mimi niweze kusema machache kwenye hoja zilizojitokeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zimejitokeza hoja takribani tatu ambazo zinahitaji kutolewa ufafanuzi, na mimi nitaenda moja baada ya nyingine. Nikianza na hoja iliyojitokeza kuhusu ununuzi wa magari ya polisi.

Kwanza nishukuru Waheshimiwa Wabunge kwa kusema hoja hiyo lakini nitoe majibu ya Serikali kwamba jambo hili Serikali inalijua na limeshafanyiwa kazi kwa kiwango kikubwa sana. Niwakumbushie tu Waheshimiwa Wabunge kwamba kabla jambo hili hata halijatoka kwenye
ripoti hii Mheshimiwa Rais ameshafanya ziara bandarini alishatoa maelekezo na baadhi ya vyombo vinaenedelea kufanyia kazi, kila chombo na nafasi yake ya utaalamu wake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna timu zinazofanyia kazi upande mmoja tu wa ubora wa magari na hilo ni jambo ambalo na Waheshimiwa Wabunge wamelisemea, hakuna gari bovu litakalopokelewa. Kuna timu inayofanyia kazi kuhusu ubora wa magari, lakini kuna timu ambazo zinafanyia kazi kuhusu masuala ya kiujumla ya kimkataba. Nimpongeze pia Mheshimiwa Naibu wangu Engineer Masauni baada ya maelekezo ya Mheshimiwa Rais kwenye Wizara na yeye alishaenda akiwa na Katibu Mkuu pamoja na IGP. Kuna timu ambayo inaundwa na watu wa kutoka ofisi tofauti tofauti ambao nao wanafanyia kazi jambo hili hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kuna vyombo vingine ambavyo vinafanyia kazi upande wa kimaadili kama kuna maeneo kama ambavyo Kamati iliweza kusema yanayohusisha mambo ya kimaadili, kuanzia mchakato wa kwanza mpaka ukamilishwaji wake. Jambo moja tu ambalo Kamati ilisema kwamba magari yamelipiwa cash, si cash. Utaratibu unaotumika wa credit export guarantee ni kwamba nchi na nchi zinaingia mkataba, zikishaingia mkataba malipo yanakuwa yanafanywa na yule aliye guarantee mkopo ule, pale ambapo recipient atakuwa amepokea na kukiri kupokea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo baada ya units za kwanza kuwa zilipokelewa, mnakumbuka yalikuwa magari takribani 77, ndipo malipo yakafanyika kwa zile units ambazo zilikuwa zimepokelewa. Kwa hiyo si kwamba fedha zote zimelipwa kabla ya magari kupokelewa, si hivyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo kwa ujumla wake kwa hoja zilizojitokeza yale yote ambayo yana makandokando yanafanyiwa kazi na Serikali kwa hatua ya mbele kabisa kabisa katika kuhakikisha hatua hizo zinachukuliwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na Waheshimiwa Wabunge mimi niwaombe muendelee kuiamini Serikali, muendelee kumuunga mkono Mheshimiwa Rais na hakuna kitu ambacho kina ukakasi kitakachofanyika, Serikali iko macho na iko mbele ya matukio kuhakikisha kwamba hatua zinachukuliwa haraka iwezekanavyo pale ambapo panatokea kuna jambo lisilo la kimaadili limefanyika. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili limesemwa ni hili la upande wa mkataba wa Vitambulisho vya Taifa, amelisemea babu yangu Mheshimiwa Heche. Niseme tu kwamba taarifa alizozisema si sahihi na kile ambacho kimefanyika. Moja, amesema kwamba mkataba ulibadilishwa na bei ya kitambulisho ikabadilishwa.

Waheshimiwa Wabunge, jambo lilofanyika liko namna hii; ni kweli Serikali ilikuwa na mkataba na kampuni ile ya kutengeneza vitambulisho vya uraia na kulikuwepo na makubaliano ya kimkataba ya malipo pamoja na urefu wa mkataba. Hata hivyo kwa kuwa kuna baadhi ya vitu vilikuwa bado havijakamilika havikukamilika vyote kwa mfano mambo kama ya connectivity mambo ya server, mambo ya integration mmeona mengine yamekuja kuanza kukamilika wakati printing zikiwa zimeshaanza kufanyika, yakiwemo na mambo ya malipo pia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kilichofanyika muda wa utekelezaji wa mkataba ulikuwa unafika, mwisho muda wa utekelezaji ulikuwa unafika mwisho. Mathalani tukienda kwa uhalisia wenyewe ulikuwa unatakiwa uishie Septemba 2016. Sasa mwaka 2016 imefika server hazijakamilika zile ID zenyewe raw card hazijakamilika, malipo hayajakamilika. Kilichotakiwa na ambacho kimefanyika ilikuwa ni kuwapa ruhusa ya kuendelea kufanya kazi lakini kwa fedha ile ile kwa makubaliano yale yale kwa gharama zilezile hakukwepo na makubaliano mapya ya bei za vitambulisho wala fedha zingine zaidi ya zile ambazo zilitakiwa zifanyike katika mkataba huo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa maana hiyo, kama ambavyo nimesema tangu mwanzo na namjua babu yangu Mheshimiwa Heche, tangu akiwa kwenye BAVICHA kule haka kawimbo ka ufisadi kalikuwa kananoga sana majukwaani. Hata hivyo nikuhakikishie tu si kwa awamu hii, Serikali iko macho na inachukua hatua mara panapokuwepo na jambo lenye harufu za aina hiyo na kama kuna mtu anadhani haya ninayosema siyo atasubiri sana. Mimi niwahakikishie Serikali iko macho na wala hairuhusu harufu za aina hiyo ziweze kujitokeza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la mwisho lililoongelewa lilikuwa la passport. Hili na lenyewe taarifa alizozisema sio hizo na mimi niwaaambie kwamba mwanzo upembuzi uliokuwa unafanyika na hatua ambazo zinachukuliwa kabla ya Serikali haijaingilia kati, ukubwa wa mradi ni ule ule na fedha zilizokuwa zinatarajiwa kutumika ilikuwa dola takribani milioni 192; ukiweka na VAT zilikuwa zinaenda kwenye mia mbili plus. Component zile kama ulizosema zilikuwa zile nne.

Sasa hivi tunachotofautisha sasa babu yangu anasema imekuja kufanyika component moja kwa dola milioni 50 si hivyo component ni zilezile nne na kinachofanyika na kilichofanyika jana ni kwamba tunaanza na component ya kwanza, lakini mkataba ambao umesainiwa una component zote nne na ni sharti uanze na kimojawapo ambacho kina uharaka ni dola milioni 57.8.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inatumika kwa component zote. Tunaanza na e-passport tutaenda e-gates, tutaenda e-permit na tutaenda la mwisho ambalo kwa mfululizo ambao sio huu nilioutaja tunatoka e-passport, tunaenda e-visa, tunaenda e-gates, tunaenda e-permit ni dola milioni 57.8. Hii ndiyo tumeshaanza na hicho ndicho kitakachofanyika. Sasa mimi ninayesema ndio Waziri wa Wizara ninyi kama mna retire imprest hapa rudisheni hizo taarifa hizo mnazozitoa si sahihi, hizi ninazosema ndio taarifa sahihi za jambo linaloenda kufanyika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Waheshimiwa Wabunge wengine ambao mnajua kazi inayofanyika nitoe wito kwamba sasa mnaweza mkafanya application online mkapata e-passport mtakapoenda Dar es Salaam mtaenda kupiga picha. Hapo hapo unapomaliza kupiga picha ukimaliza kupanda juu unaenda kuchuka passport yako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sababu tuko online hapa ulipo unaweza ukaingia kwenye mtandao ukafanya application, ukatuma picha halafu utakapozungukia Dar es Salaam ukapate passport.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa Wabunge na kwa Mtanzania yeyote ambaye anataka apate passport ya kisasa ambayo inatumika duniani si lazima kusubiri kwanza kile kitabu kingine kiishe hata sasa unaweza ukapata hiyo nyingine na ukaendelea kuitumia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo hili limefanyika kwa uangalifu mkubwa. Mimi nimpongeze na nimshukuru sana Mheshimiwa Rais kwa kutoa fedha pia kwa kutoa dira nzuri sana ambayo imetuweka kwenye historia nzuri, na jambo hili limezingatia matumizi bora ya fedha za walipa kodi watanzania na si vinginevyo kama ambavyo ndugu yangu alitaka kusema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo Waheshimiwa Wabunge kwenye hizi hoja zilizojitokeza niwahakikishie kwamba hatua thabiti zitachukuliwa pale ambapo Serikali imeshaona kuna jambo la kuchukua hatua, lakini kwa hizi zingine Serikali imezingatia matumizi bora ya fedha za walipa kodi na miradi ambayo imetekelezwa inatekelezwa kwa umakini mkubwa tena kwa ubora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, passport yetu hii ambayo imeshatoka mtachukua hata nninyi na mtakayechukua Yule atakayesafiri aende aifananishe na ya Marekani, aende aifananishe na ya Uingereza, yetu itakuwa ya kisasa kuliko ya Uingereza naitakuwa ya kisasa kuliko ya Marekani ya sasa.

Ninaamini na wao watataka kufanya za kisasa baada ya kuwa tumeshaenda kwenye teknolojia ya kisasa zaidi na kampuni iliyofanya kazi hii ilishashinda kwenye European union ilikuwa na passport za kisasa kuliko zote kule. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ni kitu ambacho nakisema na ni kitu ambacho ni cha uhakika nakushukuru sana na naunga mkono maelezo yaliyotolewa na Waheshimiwa Mawaziri katika hoja zingine zote, Serikali iko macho, iko macho, iko macho kupindukia na imebeba dhamana ya kuhakikisha kwamba inawafikisha Watanzania kwenye matarajio yao nakushukuru sana asante sana kwa kunipa fursa hii.