Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali (PAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017 pamoja na Taarifa ya Kamati ya Kudumu ya Bunge ya Hesabu za Serikali za Mitaa (LAAC) kuhusu Shughuli za Kamati kwa mwaka 2017.

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi, nami niungane na wenzangu kuwapongeza Wenyeviti na Wajumbe wa Kamati hizi mbili kwa kazi nzuri walioifanya wale wa PAC na wale wa LAAC. Pia nichukue nafasi hii vilevile nimpongeze CAG kwa kazi nzuri anayoifanya, kwa sababu Kamati hizi mbili zinategemea na taarifa ambazo zinawasilishwa na Mdhibiti na Mkaguzi Mkuu wa Hesabu za Serikali. Kwa kazi nzuri hizi amewezesha Kamati hii kufanya kazi yake kwa umakini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile niipongeze Serikali kwa kuwezesha Ofisi ya CAG kwa sababu kwa mwaka huu wa Fedha CAG ameripoti kwamba amepewa fedha kwa kadiri alivyohitaji na ndiyo maana amewezesha kufanya ukaguzi wake kwa wakati na kaleta taarifa kwa wakati. Kwa hiyo, naipongeza Serikali kwa kusikiliza kilio cha Ofisi ya CAG.

Mheshimiwa Mwenyekiti, michango yangu itajikita sana sana kwenye taarifa ya ya Hesabu za Serikali za Mitaa LAAC. Nianze na lile la ukaimu wa Wakuu wa Idara, nami niungane na Wajumbe waliosema kwamba imefika hatua sasa Serikali ichukue hatua mapema na kama ni sababu ya mchakato mrefu basi irahisishwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati yetu ya LAAC tulipoenda Korogwe, tumekuta kwenye Wakuu wa Idara 16 kuna proper Wakuu wa Idara watano tu; 11 ni Makaimu. Kwa hiyo utaangalia ni jinsi gani Ofisi hii au Halmashauri hii ya Korogwe haitaweza kutekeleza majukumu yake kwa umakini kwa sababu kuna Makaimu wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kaimu anapokaa ofisini kwanza anakosa kujiamini, anakosa ubunifu kwa sababu muda wote anafikiri kwamba Mkuu wa Idara anaingia. Kwa hiyo, naomba Serikali iharakishe na ili kuisaidia Halmashauri ya Wilaya ya Korogwe naomba Ofisi ya Waziri Mkuu, TAMISEMI ichukue hatua za haraka. Kwa sababu kwenye Wakuu wa Idara 16 kuna Proper Head of Departments watano hapo kuna athari kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo ninaomba kuliongelea ni suala la Kitengo cha Wakaguzi wa Ndani. Kitengo hiki ni muhimu sana na Kitengo hiki ni msaada mkubwa sana kwa Maafisa Masuuli. Hata hivyo, kama taarifa yetu inavyoonesha kwamba Kitengo hiki kuna upungufu wa rasilimali watu na upungufu wa rasilimali fedha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, naomba kama tulivyopendekeza kwenye taarifa ya mwaka jana, mwaka huu tumerudia kuwe na mkakati maalum wa kuongeza Watumishi katika Kitengo hiki cha Ukaguzi wa Ndani kwa sababu Halmashauri nyingi ambazo zinakuja mbele ya Kamati kuna Mkaguzi mmoja au wawili na wakati Ikama inatakiwa kila Halmashauri iwe na Wakaguzi wa Ndani watano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba jitihada za makusudi zifanywe ili kuongeza Wakaguzi wa Ndani ili kurahisisha Wakurugenzi kufanya kazi zao kwa umakini. Hili ni jicho la karibu sana kwa Mkurugenzi au Afisa Masuuli kuonesha ni nini kinafanyika katika Taasisi. Kwa hiyo, kuwe na jitihada za makusudi za kuajiri Wakaguzi wa Ndani ili Kitengo hiki kiweze kufanya kazi yake kwa umakini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala la utekelezaji wa miradi ya maendeleo, kwanza niipongeze Serikali kwa kuanzisha miradi mingi ya maendeleo na kama tulivyopitisha kwenye bajeti kwamba fedha nyingi zimeenda kwenye miradi ya maendeleo. Hata hivyo, hapa kuna changamoto mbili; changamoto ya kwanza kama tulivyosema fedha nyingi hazipelekwi kwa wakati, lakini fedha zinazopelekwa kuna maelekezo mengine ambayo yanachelewesha utekelezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa wazo kwamba TBA na na SUMA JKT wapewe kazi, lakini miradi mingi ambayo imekaguliwa hivi karibuni imeonesha Taasisi hizi mbili zimeshindwa kutekeleza ile miradi ambayo imepewa kwenye halmashauri nyingi. Kwenye Halmashauri mpya TBA na SUMA JKT walipewa kujenga majengo ya Ofisi za Wakurugenzi, lakini ukaguzi ambao unafanywa sasa hivi wa kutembelea miradi hii bado TBA na SUMA JKT wameshindwa kuitekeleza miradi hii kwa wakati, wamepewa fedha lakini inaelekea wameelemewa na miradi mingi. Kwa hiyo, naomba Serikali iangalie upya uamuzi huu ili kuharakisha utekelezaji wa miradi katika mamlaka ya Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawapongeza sana Ofisi ya Rais, TAMISEMI juzi juzi walienda kwa Mkuu wa Mkoa wa Mara wamechukua uamuzi wa haraka wa kuvunja Mkataba na TBA. Kwa hiyo, naiomba Ofisi ya Rais, TAMISEMI itembelee miradi mingine hasa ya ujenzi wa Ofisi za Wakurugenzi katika Halmashauri mpya 17. Ujenzi bado ni wakusuasua na bado hakuna kasi ambayo inaonesha kwamba miradi hii itakamilika kwa wakati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua wakifika kule watajionea wenyewe na inawezekana ikachukuliwa hatua kama ilivyochukuliwa kwa mradi ule wa Musoma, ambao Naibu Waziri Mheshimiwa Kandege aliamua kuvunja Mkataba kwa niaba ya Ofisi ya Rais, TAMISEMI. Kwa hiyo nakupongeza sana Mheshimiwa Naibu Waziri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile, nichangie kuhusu miradi ya maji kama ulivyosema katika taarifa yetu kuna utekelezaji wa kusuasua katika miradi ya maji na hapa kuna changamoto kubwa sana. Changamoto kubwa iliyopo, kuna utofauti sana wa utekelezaji wa miradi kati ya halmashauri na halmashauri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tulienda Mkoa wa Tanga tukakuta Halmashauri ya Korogwe kuna changamoto kubwa sana ya utekelezaji wa miradi ya maji, inaanzia kwenye usanifu. Kuna miradi mingine wananchi wamekataa kutoa maji kwa sababu kwenye chanzo pale cha maji wananchi hawapewi water point. Mradi unatoa maji Kijiji X wananchi wa Kijiji X hawapewi maji wanapeleka Kijiji Y, wanachi wa eneo husika wanasema haiwezekani. Sasa huu ni udhaifu wakati wa usanifu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tumeona miradi inachelewa kutekelezwa, mradi mmoja ulikuwa unatekelezwa kwa milioni 900, lakini kwa sababu ya kuchelewesha sasa hivi gharama yake ni bilioni nne, kwa hiyo, hizo ni hasara kwa Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili hata huo usimamizi wa miradi yenyewe ya maji ni changamoto kubwa. Tulienda kwenye mradi mmoja ambapo limetengenezwa hozi ya kunyweshea mifugo wakifika ng’ombe au mbuzi hawawezi kunywa maji na Mhandisi wa Maji yupo na Mhandisi wa Ujenzi yupo lakini wameshindwa kushirikisha wananchi wakatengeneza hozi ambayo ingetumika katika mazingira yale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo miradi ya maji ina changamoto kubwa sana katika mamlaka ya Serikali za Mitaa na ndiyo maana ndiyo maana Kamati yetu tukaja na wazo basi uundwe Kamati maalum ya kufuatilia miradi hii ili tujue chanzo na sababu yake ni nini. Pengine tutoe mapendekezo ambayo yataisaidia Serikali katika utekelezaji wa miradi ya maji. Kwa hiyo, naomba Wabunge tuungane katika wazo hili ili Mheshimiwa Spika aunde Kamati Teule ifanye shughuli hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa hoja ya ucheleweshaji wa fedha za maendeleo. Kama nilivyosema kuna miradi mingi fedha zinakwenda kwa kusuasua na zinapofika kunakuwa na maelekezo tofauti lakini mbaya zaidi kwamba fedha hizi sasa zingine zinaletwa mwezi Juni, mwezi ambao kwa taratibu za manunuzi huwezi kufanya chochote. Kwa hiyo, naomba Hazina waharakishe utoaji wa fedha hizi ili mamlaka za Serikali za Mitaa zisiwe na bakaa na kusababisha hoja nyingi za ukaguzi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi.