Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Jenista Joackim Mhagama

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Peramiho

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, AJIRA, VIJANA NA WATU WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa
Mwenyekiti, na mimi naomba nimshukuru sana Mheshimiwa Rais wetu Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuniamini mimi pamoja na Naibu wangu, Mheshimiwa Antony Mavunde lakini vilevile kwa kututeulia Mheshimiwa Stella Ikupa, jembe la nguvu kushirikiana na sisi katika kuhakikisha kwamba tunamsaidia Mheshimiwa Rais katika majukumu aliyotupatia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa dhati nimshukuru sana Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania. Mheshimiwa Waziri Mkuu amekuwa ni kielelezo cha utendaji bora wa Serikali ya Awamu ya Tano katika kusimamia majukumu makubwa ambayo hayataki mtu aambiwe aone kazi inayofanywa na Serikali hii. Pia namshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu pia kwa kutulea vizuri sisi Mawaziri ambao tupo katika Ofisi yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri Mkuu nakutakia kila la kheri na hasa pale unaposhughulika na maswali ya Waziri Mkuu hapa Bungeni umeonyesha kabisa kwamba wewe ni kiongozi wetu Mawaziri wote. Nakushukuru na nakupongeza sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuunga mkono hoja ya Mheshimiwa Dkt. Mpango. Dkt. Mpango naomba nikuthibitishie usikate tamaa. Wanaouponda Mpango wako wana ajenda binafsi. Dkt. Mpango chukua mawazo mazuri ya Wabunge waliotushauri sisi kwa pamoja kama Serikali, Mawaziri wote pamoja na wewe lakini yale mawazo ambayo kwa dhahiri unaona yanaponda Mpango wako kwa nia ovu achana nayo. Hasa Wabunge wa CCM wamechangia mawazo mazuri sana kwenye Mpango wa Serikali yao. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wachangiaji hapa wanasema Serikali yetu inakurupuka tu, inakuja hapa haijajipanga, haifanyi utafiti na inapanga mipango tu ambayo haieleweki. Naomba niwaambie hao wanaosema hivyo hawajasoma Mpango wala hawajaangalia mwongozo ulioletwa pamoja Mpango. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, kwenye sekta moja tu ya ajira, hivi unafikiaje mahali pa kujua hitaji la ajira katika nchi yetu ya Tanzania bila kufanya utafiti na kutengeneza mpango. Leo nitawaambia, Serikali yetu inafanya utafiti na ndio inakuja na mwongozo na inakuja mpango. Kwa mfano, sisi tumeshafanya utafiti wa kujua nguvu kazi iliyopo katika nchi yetu ya Tanzania ni idadi gani ya Watanzania na fedha za utafiti zimetolewa na Mheshimiwa Dkt. Mpango ili awe na mpango mzuri wa ajira katika nchi ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika utafiti huo tumegundua Watanzania milioni 25 ndiyo nguvu kazi ya nchi yetu ya Tanzania na tunapozungumzia viwanda hawa milioni 25 ndiyo watakaokwenda kuchukua ajira kwenye viwanda hivyo ambavyo vitajengwa kwenye nchi yetu ya Tanzania. Nani anasema Serikali hii inakuja na mipango bila kufanya utafiti, tunafanya utafiti. Katika hiyo milioni 25 tumegundua asilimia 56 ni vijana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini pia tumefanya utafiti mwingine, sasa kama tunataka kushughulikia tatizo la ajira, hivi ukosefu wa ajira kwa vijana katika nchi yetu ya Tanzania ukoje. Tumegundua kwamba ukosefu wa ajira kwa vijana kwenye nchi yetu ya Tanzania unazidi kupungua, ulikuwa asilimia 11.7 sasa hivi ni asilimia 10.3 na ni kwa sababu ya mipango mizuri ya Serikali na sekta nyingi za uzalishaji zinavyoongezeka na upungufu wa ajira unazidi kupungua. Hiyo ndiyo mipango inayogharamiwa na Waziri wa Fedha na Mipango katika nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumegundua sekta ya kilimo ndiyo inayoongeza katika kutoa ajira nyingi kwenye nchi yetu ya Tanzania na tumegundua asilimia 60.7 kilimo kinaongoza katika kutoa ajira. Sasa tunapofanya hivi ndipo tunapowaambia Watanzania baada ya utafiti huo tumemwagiza Mheshimiwa Mwijage aanzishe viwanda lakini viwanda vitakavyotumia malighafi ya kilimo inayolimwa ndani ya nchi ya Tanzania ili tutatue tatizo la ajira kwa vijana wa Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumesema Mheshimiwa Mwijage kwa kushirikiana na sekta hizo nyingine zote za umeme, maji na kadhalika atusaidie kutengeneza sera za viwanda unazozizungumza wewe Mheshimiwa Mwenyekiti iwe ni hospitali, gereji au kitu chochote, hivyo vyote ni viwanda vinatofautiana ukubwa na mazingira. Akifanya hivyo viwanda hivi vitazalisha bidhaa ambazo ndizo zinazohitajika zaidi katika soko la Watanzania hapa nchini na hivyo mwisho wa siku tutakuwa tumeweza kutatua tatizo la ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mpaka sasa tumeshafanya nini? Ili kuhakikisha vijana wa Tanzania wanaajiriwa, tumetengeneza programu maalum ya kukuza ujuzi katika nchi yetu ya Tanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitasema mafanikio yaliyopatikana, kwa kutumia Mpango huu wanaouponda wa Mheshimiwa Mpango tumefanya yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, la kwanza, tumetambua na kurasimisha ujuzi wa vijana wa Tanzania mpaka sasa 3,900 wameshamaliza mafunzo ya ujuzi katika nchi yetu, 3,440 wanaendelea na mafunzo na vijana 13,432 tumeshawatambua wanasubiri tuwafundishe. Sasa nani anayesimama hapa na anasema eti huu mpango fake wakati unajibu mahitaji ya Watanzania. Hawa vijana ambao tumewapa ujuzi wengine wanatoka mpaka kwenye Majimbo ya wapinzani, watawashangaa Wabunge wao kama hawaungi mkono Mpango huu ambao umewapa ujuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunao graduates wengi katika nchi yetu ya Tanzania lakini wamekosa mafunzo ya vitendo ya kukuza ujuzi wao. Tumeshatengeneza programu ya internship ya kuwasaidia vijana wa Kitanzania wakapate uzoefu na inalipiwa na Serikali kwa fedha za Mheshimiwa Mpango Waziri wa Fedha. Vijana 2,122 wameshaomba na Serikali inawapangia utaratibu wa kwenda kwenye mafunzo ya vitendo, hela yote inatolewa na Mpango na iko kwenye Mpango wetu. Nataka kuwaambia Watanzania kwamba tunafanya kazi na Serikali yetu inafanya kazi sana tena kwa kupitia Mpango ambao unaletwa na Mheshimiwa Mpango ndani ya Bunge la Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hayo ni machache tu ningeweza kusema mengi, lakini muda tu hauniruhusu. Napenda sana nizungumze jambo lingine hapa kuhusu mwenendo wa shughuli za Bunge. Wabunge hapa na hasa Wabunge wa Upinzani wamelidhalilisha sana Bunge lako eti Bunge hili halifanyi kazi yake sawa sawa, linaingiliwa na Serikali na halina tija yoyote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme, Ibara ya 62 na nakupongeza sana wewe, Naibu Spika na Wenyeviti wote wa Bunge, ndiyo iliyokuweka wewe na Bunge lako hili Tukufu na sio mtu. Hata hivyo, unapimaje tija ya Bunge, hupimi tija ya Bunge kwa kelele nyingi ndani ya Bunge, hupimi tija ya Bunge kwa kuleta fujo na kupambana na askari ndani ya Bunge, hapana. Hupimi tija ya Bunge eti kwa kufunga midomo ndani ya Bunge kwa plasta na kuvaa nguo nyeusi, hapana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti,…

MWENYEKITI: Mheshimiwa Waziri nakuongezea muda, kwa hiyo, endelea vizuri, endelea Mheshimiwa Waziri. (Makofi/ Kicheko)

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA WAZIRI MKUU, SERA, BUNGE, KAZI, VIJANA, AJIRA NA WATU WENYE ULEMAVU: Mheshimiwa
Mwenyekiti, naomba niseme unapima tija ya Bunge kwa namna Bunge linavyoongoza shughuli za Bunge na shughuli zinazojadiliwa ndani ya Bunge zina manufaa kwa kiasi gani kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni nani Mbunge hapa atakayesimama ambaye hatashukuru na kupongeza kazi kubwa iliyofanywa na Wabunge wa Bunge la Kumi na Moja? Niwaombe Wabunge wenzangu na hasa Wabunge wa Chama cha Mapinduzi, bebeni ajenda ya mafanikio makubwa ya Bunge letu ndiyo itakayotuvusha mwaka 2020. (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitatoa mifano, wewe mwenyewe umedhihirisha kwa mifano dhahiri kabisa kwamba Bunge hili limefanya kazi itakayokumbukwa na vizazi vyote katika nchi ya Tanzania. Umeunda Kamati hapa kwenye Bunge hilihili la Kumi na Moja ambayo imeweza kuisaidia Serikali kuweka mfumo wa kupata faida ya nchi kwenye madini ya vito katika nchi yetu ya Tanzania. Leo hii Mbunge anapata wapi courage na kusema Bunge hili halifai, halijawa na mvuto, halifanyi kazi zake linavyotakiwa! Mbunge gani huyo? Leo nitawaeleza Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge lako hili limeweka historia ya kutunga sheria ya kuhifadhi maliasili za nchi yetu ya Tanzania, ni Bunge hili la Kumi na Moja chini ya uongozi wako Mheshimiwa Job Ndugai na siyo mtu mwingine yeyote. Leo hii Wabunge wanapata wapi courage ya kulibeza Bunge hili badala ya kujisifia na kwamba ni kazi nzuri tuliyoifanya ambayo pia inaendana mipango mizuri ya Serikali yetu ya Awamu ya Tano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Bunge hili limetunga sheria ya Msaada wa Sheria kwa Watanzania watakaohitaji kusaidiwa kwenye masuala ya sheria hata wanyonge kwenye maeneo ya vijijini, ni Bunge hili la Kumi na Moja. Nimesema Waheshimiwa Wabunge wenzangu tabia ya kulibeza Bunge letu na mwenendo mzima wa Bunge siyo tabia njema. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitamalizia la mwisho kwa ufupi sana, wakati tunachangia humu ndani na hasa Kiongozi wa Upinzani alipokuwa anachangia humu ndani alitaka kupotosha umma na kutaka kuyajadili madaraka ya Mheshimiwa Rais ya uteuzi wa viongozi eti kwamba anafanya uteuzi huo kwa upendeleo, hapana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara ya 36(1), (2), (3) na (4) inatoa mamlaka kwa Rais kuanzisha na kufuta nafasi za madaraka ya namna mbalimbali katika utumishi ndani ya nchi yetu ya Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Ibara hiyo haisemi Rais atakapokuwa anafanya uteuzi eti aangalie ukanda, haisemi hivyo Ibara yetu kwenye Katiba. Ibara hiyo haisemi Rais anavyoandaa na kufanya uteuzi aangalie makabila mbalimbali kwenye nchi ya Tanzania, haisemi hivyo hiyo Ibara. Ibara hii haisemi Rais atakapokuwa anafanya uteuzi eti aangalie rangi ya Mtanzania, haisemi hivyo. Unasimamaje ndani ya Bunge kuhoji uteuzi wa Mheshimiwa Rais wa nafasi ambazo amepewa Kikatiba, ni upotoshaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini niseme unaona wateule wa Mheshimiwa Rais wanafanya kazi vizuri. Ameteuliwa hapa Mheshimiwa Mwanri kutoka Siha na ni Mkuu wa Mkoa wa Tabora, anafanya kazi nzuri sana. Ameteuliwa Mheshimiwa Mnyeti kuwa Mkuu wa Mkoa wa Manyara, anafanya kazi vizuri sana. Ameteuliwa hapa Mama yetu, Mama Anne Kilango jembe la nguvu kutoka Same anafanya kazi nzuri sana. Nina orodha ndefu nikiisema hapa ni ndefu kweli, lakini uteuzi huo unafuata madaraka ya kikatiba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, niwaombe sana Wabunge wenzangu tusiingilie madaraka ya Rais aliyopewa kwa mujibu wa katiba. Anayafanya kwa utashi wa hali ya juu na ukiangalia Ibara ya 34 inamtaka ateue watu watakaowajibika kumsaidia kubeba dhamana kwa niaba yake yeye mwenyewe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kwa kuniongezea muda na baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja iliyopo mbele yetu asilimia mia moja, nakushukuru sana.