Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Dr. Harrison George Mwakyembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyela

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

WAZIRI WA HABARI, UTAMADUNI, SANAA NA MICHEZO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana na naomba nianze kwa kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuendelea kuniamini kumsaidia kuongoza Wizara hii ya Habari, Utamaduni na Michezo na vilevile kwa kumteua Mbunge kijana, mchapakazi na mwanamichezo hodari Mheshimiwa Juliana Daniel Shonza kunisaidia kuongoza hii Wizara.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja hii na ninampongeza sana Waziri wa Fedha na Mipango, Mheshimiwa Dkt. Philip Isdor Mpango na Naibu wake Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kachwamba Kijaji kwa kazi nzuri wanayoifanya ya weledi mkubwa na katika Wizara hii nyeti katika maendeleo ya Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijielekeze kwenye baadhi tu ya michango iliyogusia Wizara yangu ambayo inahitaji ufafanuzi wa kina kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na madai ya Mbunge wa Mbeya Mjini, Mheshimiwa Joseph Mbilinyi, kwamba Mkurugenzi wa Idara ya Habari ambaye vilevile ni Msemaji wa Serikali alitumia kifungu cha 54(1) cha Sheria ya Huduma za Vyombo vya Habari kulifungia Gazeti la Tanzania Daima, kitu ambacho anasema kwamba siyo sahihi, alichotakiwa kufanya si kulifungia gazeti, lakini kuwawajibisha waandishi waliohusika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, madai haya ya Mheshimiwa Mbilinyi yanagusia utekelezaji mzima wa sheria hii mpya, hivyo nafikiri kuna umuhimu sana wa kutoa uchambuzi wa kina kidogo kuhusu sheria hii na hapa tulipofika ili tusiendelee kuwachanganya wanaotusikia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukumbushane kidogo tu kuwa Sheria hii ya Huduma za Vyombo vya Habari tuliipitisha wenyewe hapa Bungeni tarehe 5 Novemba, 2016 na tarehe 16 Novemba, 2016 Mheshimiwa Rais akaridhia hii sheria na tarehe 31 Desemba sheria hii ikaanza kutumika rasmi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kurahisisha na kuwezesha utekelezaji wa sheria hii uende vizuri zaidi ikabidi tutengeneze Kanuni na kanuni zenyewe pia zikawa tayari na tarehe 3 Februari, 2017 zikaanza kutumika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka nielezee hili wanisikilize vizuri hata wadau katika masuala ya habari vizuri kwa makini kwamba chini ya sheria hii na kanuni zake kuna vyombo vikuu vinne vya kusimamia uendeshaji na maendeleo ya vyombo vya habari hapa nchini ambavyo vinatakiwa viundwe. Kwanza ni Independent Media Council of Tanzania ambalo ni Baraza Huru la Habari ambalo linaundwa na wanahabari wenyewe, lakini ni wanahabari ambao ni accredited walishapata ithibati. Chombo cha pili kilichotakiwa kuundwa hapa ni Bodi ya Ithibati yenyewe (Accreditation Board). Kwa sababu tulishakubaliana kwamba Uandishi wa Habari sio kitu cha kubahatisha tena ni taaluma. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama zilivyo taaluma zingine lazima kiwepo chombo kinachofuatilia training ya uandishi, weledi wao na nani atambuliwe kuwa mwandishi wa habari ndiyo maana tuna chombo hicho kinaitwa chombo cha ithibati (Accreditation Board). Tatu ni Kamati ya Kimahakama ya malalamiko ambayo kazi yake kubwa ni kusikiliza malalamiko ya wananchi kama kuna upotofu wa maadili, kama mtu ameonewa na hicho chombo kitakuwa na mamlaka kama ya Mahakama, ndiyo maana ukiona hujaridhika unakwenda Mahakama Kuu kudai kwamba haki yako kwa kweli imefinywa, pengine hukusikilizwa vizuri ama kuna uvunjifu wa hizi kanuni tunaita principles of natural justice. Kwa hiyo, hicho chombo ni Quasi Judicial Board, ni almost kama Mahakama.

Mheshimiwa Mwenyekiti, chombo cha nne ni Mfuko wa Habari ambao kazi yake kubwa ni kuandaa waandishi wa habari vizuri zaidi waweze kupata weledi katika kazi na vilevile kufanya utafiti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa nasema hayo yote kwamba dhamira ya sheria hii ilikuwa nzuri sana, kuwa vyombo hivi vinne vikifanya kazi vizuri kwa kushirikiana, sio tu vyenyewe vilevile na Serikali na kwa kuzingatia maadili na sheria za nchi, basi tasnia ya habari ingeweza kujiendesha wenyewe kwa kweli bila mtu yeyote kuvisogelea Vyombo vya Habari, hilo ndilo lilikuwa lengo la sheria.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, najua kuna swali limekuwa linaulizwa mpaka kwenye Kamati kwamba, vyombo hivyo ulivyovitaja mbona havijaanza kufanya kazi mpaka leo? Ndiyo ni kwa sababu kubwa mbili, sababu kwanza tumeanzisha usajili mpya wa majarida na magazeti yote, tatizo moja ni kwamba hatujapata ushirikiano mzuri kutoka kwa wadau wenyewe, tumeahirisha zaidi ya mara tatu deadline ya usajili. Mwisho tumekuja kusajili tarehe 31 Oktoba ambazo ni wiki mbili tulizopita na ni robo tu ya majarida na magazeti yaliyoandikishwa. Tumefungua milango wanaweza kuendelea kujiandikisha. Kwa hiyo, hatuwezi kupata idadi ndogo ya wadau hao tukaanzisha vyombo hivi muhimu kesho utaambiwa Serikali imelazimisha hivyo vitu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili tukumbuke kwamba kuna uwepo wa kipindi cha mpito (transition period) katika hii sheria, yote ilitokana na hoja za Wabunge hapa. Wabunge wanasema hatuwezi kuwawajibisha waandishi wa habari kwa sababu kazi ya uandishi wa habari ni kazi nzito ya kutafsiri mtu amesema nini, anakaa kwenye chumba cha habari, unahitaji elimu at least basic education ambayo tukubaliane hapa. Ndiyo maana wote tukasema tunaiga na nchi zingine kama Uganda ambapo lazima uwe na degree mbili, tukasema lakini hapa angalau uwe na Diploma au Shahada ya Chuo Kikuu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Waheshimiwa Wabunge mkasema tuwape miaka mitano tusiwe unfair kawa hawa watu tukatoa miaka mitano, wenzetu wajipange vizuri waingie ili waweze kuwa accredited kama waandishi wa habari.

Mheshimiwa Mwenyekiti, matokeo yake ni kwamba utekelezaji mzima wa uanzishwaji wa vyombo hivi vinne unachelewa mpaka pale wadau wenyewe haitokuwa Serikali, wadau wenyewe walisema pale to speed up, tuko tayari hata tukaanzisha kesho Media Council na wale waandishi wenye shahada na wenye diploma wanatosha hao waliopo, tukifanya hivyo kama Serikali itakuwa na mgogoro mkubwa. Kwa hiyo, tunasubiri wadau wenyewe watuambie muda umefika tuitekeleze hiyo sheria sasa tuepukane na transitional period, hiyo hatuwezi kuamua kama Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndiyo maana namjibu Mheshimiwa Mbilinyi kwamba Mkurugenzi wa Habari hajawahi hata siku moja kulifungia gazeti lolote kwa chini ya sheria hii mpya na wala hajawahi kutumia hicho kifungu cha 54. Kifungu cha 54 kinatoa ufafanuzi tu wa kosa la kuchapisha habari za uongo na kuitia jamii katika hofu. Madaraka anayoyazungumzia Mheshimiwa Mbilinyi ni madaraka ya Waziri nilitaka nilieleze hili. Pamoja na sheria hii kuunda vyombo vinne ambavyo vitaweza kabisa kuleta pengine nidhamu kama kweli Watanzania tutaamua kutumia vyombo hivi kuheshimu kanuni na maadili ya nchi, kuna kitu kinaitwa residual powers of the government, hizo residual powers hatujanyanganywa na hii sheria ningeshangaa sana tungenyanywa na hii sheria. Duniani kote Serikali lazima iwe na residual powers kuhakikisha kwamba inalinda haki za watu wake na pili inalinda usalama wa nchi hizo lazima tuwe nazo, hata kama kuna vyombo vingine
vinafanya hiyo kazi. Sasa hayo madaraka yamo katika sheria mpya katika kifungu cha 59 ndiyo ambayo Waziri anatumia. Ukiona trend ya gazeti toka siku ya kwanza unaionya, siku ya pili unaionya, siku ya tatu unamwambia bwana eeh, unaleta uchochezi mara ya sita unaonya unasema aah, pengine ukapumzike miezi mitatu utafakari vizuri, ndiyo hicho tunachofanya ili kulinda mstakabali wa nchi yetu hii.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hayo hatuyafanyi Tanzania tu iko dunia nzima na tunafanya kwa kuzingatia matakwa ya Mkataba wa Kimataifa tulioingia Watanzania International Covenant on Civil Political Rights ya mwaka 1966, sisi ni signatories dunia yote ni signatories na kila nchi imechukua hayo maudhui yako kwenye Ibara ya 19 ya huu mkataba na sisi tumechukua tumeingiza kwenye Katiba yetu Ibara ya 18 na Ibara ya 30 kwamba hata kama una haki, hata kama una uhuru, uhuru huo lazima uwe na mipaka kwa ajili ya maslahi ya nchi. Mipaka lazima iwepo na hata hii sheria imeingizwa katika kifungu cha 59 kwamba pamoja na kuwaachia mjiendeshe yanapokuja maslahi ya Taifa, inapokuja kulinda usalama wa nchi, lazima Serikali iwe na sauti hapo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimalizie kitu kimoja Mheshimiwa Saada Mkuya naye aliongelea kuhusu ujenzi wa mazingira wezeshi ya michezo kuitangaza nchi kimataifa. Nampongeza sana Mheshimiwa Saada Mkuya kwa kuja na hilo wazo, ni wazo zuri sana. Sasa hivi tunamalizia utengenezaji wa rasimu ya Sera ya Michezo ya Taifa mpya, imefika mbali sana, nina uhakika ndani ya miezi sita tutakuwa sera mpya ya michezo hapa Tanzania. Hata kabla hiyo sera haijakamilika tumeshaanza kutekeleza, kuhakikisha kwamba tunatumia michezo kuitangaza nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka huu mapema tumeweza kuleta timu ambayo iko kwenye Premier League ya Uingereza iitwayo Everton, kuja kucheza kwenye uwanja wetu wa kisasa hapa kitendo hicho tu peke yake kimeweza kuinyanyua Tanzania katika macho ya ulimwengu na ndiyo maana tukaweza kupata hata ufadhili wa kutengeneza kiwanja chetu upya na nitakabidhiwa nafikiri tarehe 24 na mwenzangu Naibu Waziri kikiwa na nyasi ambazo zitakaa kwa zaidi ya miaka kumi bila kutusumbua tena ama kupata ugojwa wa moyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo asubuhi nimeingia kutoka Arusha baada ya Mheshimiwa Waziri Mkuu kuniruhusu kwenda kufunga michezo ya golf. Naomba nimshukuru tena Mheshimiwa Dkt. Mpango na mwenzake Mheshimiwa Dkt. Ashatu kwa kutoa pesa kuelekeza kwenye mahitaji ya barabara, hii barabara kwenda Arusha imekamilika. Hii shortcut kwenda Arusha nimetoka Arusha saa 11 asubuhi nimewahi kipindi asubuhi, hayo ndiyo maendeleo Mheshimiwa Mpango hongera sana, Mheshimiwa Kijaji hongera sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikwenda Arusha kufunga mashindano ya golf ambayo yamevutia wacheza golf wa kimataifa wa mataifa 250. Nampongeza sana mwekezaji wa Arusha ambaye amejenga kiwanja cha golf ni Mholanzi Mtanzania wamejenga kiwanja cha golf cha kisasa kupita vyote katika Afrika ya Mashariki na Kati. Wamekuja wageni wengi na ndiyo maana tumekubaliana na Mheshimiwa Waziri wa Utalii hapa tufanye kazi kwa karibu sana kwa sababu michezo sasa hivi na utalii vinaenda pamoja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wenzetu wote duniani michezo ya golf inachezwa na matajiri, kwa hiyo, ukivisogeza karibu na mbuga za wanyama unapata watu wazito kweli. Nimepishana tu juzi na mcheza sinema mashughuli wa Marekani Harrison Ford amekaa hapo akicheza golf wiki nzima, siyo yeye tu wengi wanakuja. Ndiyo maana naomba nitoe wito kwa viongozi wenzangu hasa huku kwenye Wilaya kama kulikuwa na kiwanja cha golf zamani naomba msivigeuza kuwa magulio, maana kulikuwa na imani kwamba hii michezo ya golf siyo yetu, hapana!

Mheshimiwa Mwenyekiti, kijana aliyeshinda golf tournament ya kimataifa ya Arusha jana ni kijana wa Kitanzania kwa jina la Victor Joseph na ni mwanafunzi, mtoto wa kawaida tu. Unajua hawa vijana ambao hawajawahi kucheza golf Mungu amewapa kipaji cha ajabu, anapiga tu mara moja anaingia moja kwa moja kwenye shimo utafikiri Tiger Woods! Tiger Woods wapo wengi, naomba ndugu zangu tutenge maeneo kwa ajili ya kujenga viwanja vya kisasa vitatusaidia. Ukinipa tu eneo nitatafuta Wawekezaji kama ambavyo tumefanya upande wa Arusha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kusema naunga mkono hoja hii kwa nguvu kweli. Ahsante sana.