Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Prof. Joyce Lazaro Ndalichako

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Kasulu Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

WAZIRI WA ELIMU, SAYANSI NA TEKNOLOJIA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipatia nafasi hii nami nichangie hoja ambayo iko mezani kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuanza kwa kumshukuru kwa dhati Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Dkt. John Pombe Magufuli kwa kuniamini na kuniteua tena niendelee kutumikia katika sekta hii ya elimu. Nimhakikishie Mheshimiwa Rais na Watanzania kwa ujumla kwamba nitafanya kazi yangu kwa uadilifu na kamwe sitawaangusha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kuanza mchango wangu kwa hoja iliyoko mbele yetu ambayo ni Mpango wa Maendeleo ya Taifa wa mwaka 2018/2019 pamoja na Mwongozo wa Bajeti kwa kuanza kusema kwamba ninaunga mkono hoja kwa asilimia mia moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaunga mkono hoja hii kwa sababu imeandaliwa vizuri na imeangalia maeneo ambayo ni muhimu katika kusukuma maendeleo kwa Taifa letu. Napenda kumpongeza kwa dhati Waziri wa Fedha na Mipango Dkt. Philip Mpango na Naibu wake kwa kazi nzuri ambayo wameifanya katika kuandaa hoja hizi pamoja na watendaji wote katika Wizara ya Fedha na Mipango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kutekeleza Mpango huu, Wizara yangu inayo mchango muhimu kwa sababu elimu ndiyo nguzo muhimu katika kuleta maendeleo ya Taifa letu. Kama ambavyo tunafahamu, Mpango wetu wa maendeleo umejikita katika kujenga uchumi wa viwanda na ili tuweze kujenga uchumi wa viwanda ni lazima kuangalia kwa umakini ujuzi wa Watanzania ambao ndiyo nguzo kuu ya maendeleo katika Taifa hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara yangu katika kuhakikisha kwamba tunaweka mchango unaotakiwa katika kukuza ujuzi nchini, tumeweza kufanya mambo mbalimbali, Waheshimiwa Wabunge wamekuwa katika michango yao wanaulizia na kuonesha wasiwasi wao kama kweli hii Serikali imejipanga kuhakikisha kwamba kunakuwa na ujuzi wa kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza niseme katika mpango wetu tumeonyesha kwamba ili tuweze kwenda na kasi inayotakiwa tunatakiwa tuwe na asilimia 55 ya Watanzania wenye ujuzi wa chini, asilimia 33 ya ujuzi wa kati na asilimia 12 ya ujuzi wa juu.

Kwa hiyo, Serikali inao Mpango Mkakati wa Kukuza Ujuzi (National Skills Development Strategy) ambao katika kutekeleza mpango huo, Wizara yangu kwa kushirikiana na Ofisi ya Waziri Mkuu kuna mpango ambao tunazo dola milioni 120 ambazo ni sawa na fedha za Kitanzania bilioni 250 ambazo zinalenga kukuza ujuzi

Mheshimiwa Mwenyekiti, fedha hizi zitawezesha kuimarisha mafunzo ya ufundi stadi kwa kuimarisha miundombinu katika taasisi zetu zinazotoa mafunzo ya ufundi stadi hususan VETA, Arusha Technical, Dar es Salaam Institute of Technology pamoja na taasisi nyingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia huu mpango wa elimu na ujuzi kwa kazi zenye tija (education and skills for productive jobs) umejikita katika kuangalia maeneo ambayo ni ya kipaumbele katika mpango wetu wa maendeleo ambao ni pamoja na sekta ya kilimo, utalii, usafirishaji, ujenzi, nishati pamoja na TEHAMA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namna mojawapo ya kupata fedha hizi ambazo nimezisema bilioni 250 ambazo Serikali tayari inazo kwa ajili ya kutekeleza mradi huu itakuwa ni pamoja na kuandika maandiko ambayo ni shindani. Kwa hiyo, nitumie fursa hii kuwataka Waheshimiwa Wabunge tushirikiane katika kuhakikisha kwamba fedha hizi ambazo tunategemea kutangaza kwa mara ya kwanza maombi kwa ajili ya kupaya ufadhili (skills development fund) mwishoni mwa mwezi huu tushirikiane kuhamasisha taasisi za ufundi zilizoko katika maeneo yetu kwa sababu fedha zitakuwa zinatolewa katika mfumo wa ushindani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo lingine ningependa kuchangia ambalo Waheshimiwa Wabunge wamelizungumza katika michango yao ni suala la utoaji wa elimu bure na suala la changamoto zilizopo katika utoaji elimu.

Kwanza niseme kwamba suala la utaoji wa elimu bure katika Nchi hii limekua na mafanikio makubwa sana. Kila mwezi Serikali inatoa kiasi cha shilingi bilioni 20.8 kwa ajili ya elimu bure na mojawapo ya vigezo ambavyo tunaweza tukavitumia kusema kwamba kumekuwa na mafanikio makubwa, ukiangalia takwimu za wanafunzi ambao wanafanya mtihani wa kidato cha pili ambao wameanza leo hii wameongezeka kutoka wanafunzi 435,075 mwaka 2016 hadi kufukia wanafunzi 521,855 ambalo ni ongezeko la wanafunzi 87,730.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia mpango wa elimu bure ulianza kutekelezwa mwaka 2016, hii ina maana kwamba, wale wazazi ambao walikuwa wanashindwa kuwapeleka watoto wao sekondari kwa sababu ya ada, Serikali imefungulia na ndiyo maana leo hii tunaona hata idadi ya watahiniwa wanaofanya mtihani wa kidato cha pili imeongezeka sana. Niwahakikishie Watanzania kwamba, Serikali imejipanga vizuri katika kuimarisha miundombinu katika ngazi zote za elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kukabiliana na changamoto za ongezeko la wanafunzi tumekwishajenga madarasa 1,409 tumeshajenga matundu ya vyoo 3,394 lakini vilevile tumeongeza mabweni kwa ajili ya kuhakikisha kwamba watoto wa kike wanaotoka umbali mrefu wanaweza kusoma katika mazingira ambayo ni tulivu zaidi kwa hiyo, tumejenga mabweni 261.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kwa kutambua kwamba mazingira ni muhimu kwa wananfunzi kujifunza vizuri tunafanya ukarabati wa shule zetu kongwe na mpaka sasa tumekwishaanza ukarabati katika shule 42 kati ya shule kongwe 88 katika nchi hii, niwahakikishie Waheshimiwa Wabunge kwamba shule zote kongwe nchini zitafanyiwa ukarabati.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile tumeboresha miundombinu katika vyuo vyetu vya ualimu na tunaendelea kufanya hivi. Sasa hivi ninavyozungumza Vyuo vya Ualimu vya Kitangali, Mpuguso, Ndala na Shinyanga miundiombinu yake inaimarishwa kwa kiwango kikubwa, majengo ya kisasa yanajengwa, hii yote ni katika kutekeleza mpango wa Serikali ambao unalenga kufungamanisha maendeleo na rasilimali watu, ili kufanya hivyo lazima tuhakikishe kwamba tunayo rasilimali iliyobobea katika ujuzi katika kutekeleza mpango wetu wa maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo Wizara imekuwa ikifanya katika kutekeleza mpango huu ni kuhakikisha kwamba tunakuwa na msingi ulio imara. Kwa sababu tunafahamu kwamba nyumba bora inajengwa katika msingi ulio imara, Serikali imekuwa ikiweka kipaumbele katika elimu ya awali kuhakikisha kwamba vijana wanapata utayari wa kuanza elimu ya msingi, tumeendelea kutekeleza Programu ya Kukuza Stadi za Kusoma, Kuandika na Kuhesabu ili kuwajengea vijana wetu msingi mzuri wa kuweza kupata maarifa wanapokuwa wanaanza darasa la kwaza, la tatu hadi la nne.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kufanya hivyo tumekuwa tukitoa mafunzo kwa walimu wa darasa la kwanza, la pili, walimu wa darasa la tatu na la nne pamoja na walimu ambao wanafundisha wananfunzi wenye mahitaji maalum.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali pia imeendelea kuweka mazingira wezeshi kwa wanafunzi wenye mahitaji maalum ambapo tumewanunulia vifaa vya kujifunzia vyenye thamani ya shilingi bilioni 3.6 lakini pia Serikali inaendelea kuimarisha ufundishaji wa sayansi kwa sababu tukipata Wanasayansi wazuri ndiyo chachu muhimu ya kuweza kupata wataalam ambao wanahitajika katika fani mbalimbali nchini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tumeendelea pia kuhakikisha kwamba tunakwenda sambamba na utoaji wa elimu ya juu kwa kuimarisha miundominu katika elimu ya juu. Ninapende kuliarifu Bunge lako Tukufu kwamba pamoja na taarifa ya Serikali ambayo niliisoma hapa Bungeni tarehe Tisa pia Bodi ya Mikopo imeendelea kutoa mikopo na wananfunzi zaidi ya 1,775 wamepangiwa mikopo na hivyo kufanya sasa jumla ya wananfunzi ambao wameshapangiwa mikopo kufikia 31,353.

Mheshsimiwa Mwenyekiti, nitumie fursa hii kwa Wanafunzi ambao hawajapata mikopo lakini wanaona bado wana uhitaji, dirisha la kukata rufaa limefunguliwa leo na litafungwa tarehe 19 Novemba, 2017. Niwaombe na niwaelekeze wanafunzi wote ambao hawajapata mikopo lakini wanaona wana uhitaji mkubwa, watumie fursa hiyo kukata rufaa na Serikali inaendelea kujiridhisha kama Je, kweli wanafunzi wale waliopangiwa mikopo ndiyo wale ambao wana uhitaji ukilinganisha na wale ambao hawajapata ili kuhakikisha kwamba dhamira ya Serikali kuhakikisha kwamba mikopo ya elimu ya juu inatolewa kwa wanafunzi tu wenye uhitaji kwa mujibu wa vigezo vilivyowekwa inazingatiwa, kwa sababu hiyo tayari nimeagiza Bodi ya Wakurugenzi ya Bodi ya mikopo kupitia jina moja baada ya lingine ili kujiridhisha kwamba je, wale waliopangiwa mikopo ndiyo wenye uhitaji kuliko wale ambao hawajapangiwa, lakini pia kupitia majina yote ya wanafunzi ambao hawajapata mikopo ili kujiridhisha kama kweli hawana vigezo kwa mujibu wa vigezo mbavyo vimewekwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niwahakikishie kama nilivyosema, wanafunzi wa elimu ya juu kwamba Serikali inatekeleza sera ya kutoa mikopo kwa wanafunzi wenye uhitaji tu na hapo Waheshimiwa Wabunge tuelewane kwamba sera yetu ya elimu ya juu ni sera ya uchangiaji. Hatujafikia mahali ambapo Serikali inatoa mikopo kwa wanafunzi wote na ndiyo maana hata Sheria ya Bodi ya Mikopo imeainisha wazi kwamba mikopo itatolewa kwa wanafunzi wenye uhitaji, kazi ya Wizara yangu ni kusimamia na kuhakikisha kwamba wale ambao wanapangiwa mikopo ni wale tu wenye uhitaji na siyo vinginevyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kushukuru kwa nafasi na kama nilivyosema tangu mwanzo wakati naanza ninaunga mkono hoja hii na ningeomba Wabunge wote tuiunge mkono kwa sababu ni Mpango ambao ni mzuri sana. Ahsante sana.