Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Zainab Mndolwa Amir

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ZAINABU M. AMIRI: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Waziri wa Fedha na Mipango Mheshimiwa Philip Isdor Mpango (Mbunge) kwa kuwasilisha Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2018/2019 na Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango wa Bajeti kwa mwaka 2018/2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mapendekezo yangu na maoni yangu katika Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2018/2019utakuwa katika sehemu tatu:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali iweke kipaumbele katika viwanda hususani kujenga, kufufua viwanda vyetu mfano, katika Mkoa wa Morogoro kuna viwanda kama vile Canvas, Polyster, Ceramic, Magunia, Tannaries (Kiwanda cha Ngozi), Moro Shoe, Moproco. Vyote hivi vipo katika Manispaa ya Morogoro, viwanda hivi vingine vinafanyakazi na vingine wawekezaji hawaviendelezi. Hivyo Serikali isimamie na kuwapa muda wawekezaji hao kuviendeleza na wakishindwa virudishwe kwa Serikali ili wapewe wawekezaji wengine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, viwanda hivi vikifanyakazi kama miaka ya 1980 na 1990 vitaleta ajira kwa Watanzania pia kuongeza Pato la Taifa la Tanzania, kulipa kodi ya bidhaa zinazozalishwa kutokana na ujenzi wa reli itakayojengwa kutoka Dar es Salaam hadi Morogoro (treni ya mwendokasi itaongeza chachu ya ajira ya wananchi wa Dar es Salaam, Mkoa wa Pwani na Morogoro ambao watapata ajira katika viwanda hivyo vilivyopo Mkoa wa Morogoro).

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu kodi, niipongeze Mamlaka ya Mapato Tanzania (TRA) kwa kukusanya kodi kwa wafanyakazi hususani katika Miji Mikuu mfano Dar es Salaam. Nashauri katika kipaumbele kimojawapo Serikali iandae utaratibu maalum ambao utamwezesha mfanyabiashara alipe kodi kwa wakati na afurahie kuchangia Pato la Taifa na siyo Serikali iwe adui kwa mlipa kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali iboreshe mazingira ya mwananchi wakati wa kuanza biashara. Kuna tatizo katika utaratibu uliopo, nashauri katika Mpango wa Maendeleo 2018/2019 Serikali impe muda angalau miezi mitatu (grace period) mwananchi anayeanzisha biashara na baada ya hapo ifanye makadirio kwa malipo ya mapato.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi sasa mfanyabiashara anakadiriwa malipo ya kulipa kwa mwaka kabla ya kuanza biashara na sehemu kama vile Kariakoo makadiro ni makubwa mno ambayo si chini ya milioni mbili kwa mwaka, na hii hupelekea wafanyabiashara kushindwa kulipa kodi na
hatimaye kufunga biashara. Hivyo maoni yangu Serikali ipitie tena utaratibu huu kupunguza makadirio ili mwananchi aweze kumudu kulipa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia nashauri faini wanazotozwa wafanyabiashara ambao wanakutwa na makosa, mfano ya kutotoa risiti za EFD ni kubwa mno shilingi milioni tatu kulinganisha na bidhaa aliyouza na hii hupelekea mwananchi kushindwa kulipa faini na hatimaye kufunga biashara zao. Pia nashauri wafanyabiashara wadogo wadogo maarufu kama wamachinga hususani waliopo katikati ya Jiji la Dar es Salaam (Kariakoo) Serikali iwasajili ili waweze kuwa na mchango kwa Pato la Taifa kwa kulipa kodi na kwenda sambamba na kauli mbiu ya Rais wetu Mheshimiwa John Pombe Magufuli ya ukiuza toa risiti na ukinunua dai risiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika sekta ya afya Serikali imefanya jitihada kubwa katika kutatua matatizo mbalimbali yakiwemo kutoa madawa, vifaa tiba, ujenzi wa zahanati na vituo vya afya. Maoni yangu Hospitali ya Taifa Muhimbili ni Hospitali ya Rufaa Tanzania, wakati tunaelekea katika Mpango wa Maendeleo wa Bajeti wa mwaka 2018/2019 Serikali ijenge eneo ambalo litasaidia wananchi wanaowasindikiza wagonjwa wao kutoka katika mikoa mbalimbali Tanzania ambao hawana ndugu au jamaa Jijini Dar es Salaam, waweze kupata sehemu za kufikia baada ya kumkabidhi mgojwa wodini. Maana kuna baadhi ya wagonjwa wanahitaji huduma za karibu kutoka kwa ndugu zao ambazo wahudumu wakati mwingine ni vigumu kuzifanya. Wakati mwingine wagonjwa wanaopewa rufaa kuja Muhimbili ni watoto zaidi ya miaka 5 – 15 ambao wanahitaji huduma ya karibu ya mzazi au mlezi wake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho naunga mkono hoja ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa kwa mwaka 2018/ 2019.