Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Waziri wa Fedha na Mipango, Mheshimiwa Dkt. Philip Mpango, pamoja na timu nzima ya Wizara ya Fedha na Mipango kwa kuleta mapendekezo mazuri ya Mpango na pia Mwongozo wa Maandalizi ya Mpango na Bajeti kwa mwaka 2018/2019. Naomba nipendekeze kuwa katika kipaumbele cha viwanda vya kukuza uchumi na ujenzi wa msingi wa uchumi na viwanda msukumo wa kuboresha kilimo, hasa katika suala la bei na uhakika wa masoko ya mazao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuboresha kilimo tutaweza kuwa na malighafi ya kutosha kwa viwanda vyetu. Pamoja na msukumo wa kuanzisha kanda maalum za kiuchumi na kuimarisha SIDO, napendekeza katika mpango kuwepo na viwanda vidogo huko vijijini ili kuongeza thamani ya mazao, uwepo msukumo wa viwanda vya kuchakata pareto kutokana na mahitaji makubwa ya duniani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipaumbele cha kufungamanisha uchumi na maendeleo ya watu, kipaumbele hiki ni muhimu sana hasa ukizingatia kuwa kukua kwa uchumi wetu kuendane na hali za wananchi hasa vijijini. Katika mpango wa mwaka 2018/2019 napendekeza Serikali iweke katika bajeti ya maendeleo umaliziaji wa miradi iliyokwama kwa muda mrefu. Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya wananchi wamejitoa sana katika ujenzi wa zahanati na vituo vya afya na pia ujenzi wa madarasa pamoja na ujenzi wa kituo cha polisi cha wilaya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ya upatikanaji wa maji hairidhishi katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya. Kati ya miradi tisa iliyoanzishwa mwaka 2013, ni mradi mmoja tu uliokabidhiwa wakati zaidi ya shilingi bilioni 4.2 kati ya shilingi bilioni 5.5 ambayo ni 84% zimelipwa, lakini wananchi hawapati maji, Serikali ihakikishe miradi hii inakamilika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, wakati huo huo napendekeza mradi wa maji wa chanzo cha Mto Kiwira kwa matumizi ya Wilaya ya Mbeya. Pia kuwepo na kuunganisha Mamlaka ya Maji ya Jiji la Mbeya na Mamlaka ya Maji ya Mji Mdogo wa Mbalizi. Pia kuwepo kwa bajeti ya ujenzi wa mabwawa kwa wafugaji wa Kata ya Mjele.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipaumbele cha ujenzi wa mazingira wezeshi, napendekeza msukumo uwepo wa kuboresha miundombinu ya barabara vijijini. Pamoja na uchumi mzuri wa Wilaya Mbeya, hali ya barabara ni changamoto kubwa. Napendekeza msukumo uelekezwe kuboresha barabara za kuunganisha mikoa, ikiwemo barabara ya Mbalizi – Makongorosi, barabara ya Mbalizi – Shigamba, barabara ya Isyonje – Kikondo – Makete – Njombe, barabara ya Mjele – Mlima Njiwa, barabara ya Kawetere – Ikukwa, barabara ya Mbalizi – Songwe – Jojo, barabara ya Ilembo – Mwala, barabara ya Ilembo Isonso na pia, by pass ya Mlima Nyoka (Uyole) – Songwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napendekeza reli ya TAZARA iboreshwe na iende sambamba na uboreshaji wa Bandari ya Dar es Salaam ikiwa ni pamoja na ujenzi wa Bandari Kavu Inyala, Mbeya. Pamoja na uboreshaji wa reli ya TAZARA, pia iwekwe kwenye bajeti ujenzi wa Reli ya Uyole, Mbeya kwenda Malawi, ili kukabiliana na ushindani wa biashara ya Bandari yetu ya Dar es Salaam na bandari nyingine kama Beira, Msumbiji na zile za Afrika Kusini na hata Angola.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kipaumbele cha kuimarisha usimamizi na utekelezaji wa Mpango, napenda msukumo uwekwe kuboresha ufuatiliaji na utoaji taarifa za utekelezaji, ikiwa ni pamoja na kuwepo kwa mfumo utakaotoa taarifa sahihi. Taarifa nyingi za miradi zimekuwa hazina uhalisia na zinapotosha, taarifa za miradi ya maji katika Halmashauri ya Wilaya ya Mbeya zimekuwa zinapotoshwa. Naunga mkono hoja.