Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Edward Franz Mwalongo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Njombe Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. EDWARD F. MWALONGO: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi. Awali ya yote, nimpongeze Mheshimiwa Waziri kwa kutuletea Mpango huu wa maandalizi ya maendeleo wa mwaka 2018/2019.

Pia nitakuwa ni mchache wa fadhila kama sitampongeza Mheshimiwa Rais John Pombe Magufuli kwa kazi nzuri ya kuiendesha na kuisimamia nchi yetu. Sisi Wana- Njombe kwa maana ya Jimbo la Njombe tunamshukuru sana Mheshimiwa Rais kwamba tumepata mafanikio makubwa katika kipindi chake, tunajengewa kituo cha kisasa kabisa cha afya katika Kijiji cha Ihalula chenye thamani ya shilingi milioni 500, tunajengewa soko la kisasa katika Mji wa Njombe lenye zaidi ya shilingi bilioni nne lakini pia tunajengewa stendi ya kisasa kabisa katika Mji wetu wa Njombe. (Makofi)

Kwa hiyo, hayo ni mafanikio mazuri na nampongeza sana Mheshimiwa Rais na tunamshukuru sana kwa kutupatia hizo fedha za maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikianza na kuchangia Mpango wa Maendeleo ambao upo mbele yetu, sisi Njombe tunaitwa Njombe Mjini, lakini ni wakulima, kwanza kabisa nianze na suala la wakulima. Watu wengi wameongelea suala la mahindi, ni kweli kabisa suala la mahindi kiuchumi, mfumuko wa bei katika nchi yetu unashikiliwa na mahindi. Kama Serikali inaliona hilo na inataka kweli wananchi hawa wanaolima mahindi waweze kunufaika na kilimo, lakini vilevile waisaidie Serikali kuweza kushikilia mfumuko wa bei basi ihakikishe kwamba Serikali inawekeza vizuri kwa wakulima kwa maana ya kuwapa pembejeo, wataalam wa ugani na mbegu zilizo bora.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pale Njombe kuna Kituo cha Usimamizi wa Mbegu Bora, kituo kile kina wataalam wachache, kina gari moja linatumika Kanda nzima kwa ajili ya udhibiti wa mbegu. Sasa hawa wakulima wanaolima mahindi na kile kituo ndio kinadhibiti mbegu za aina zote za mpunga, mahindi na kahawa, kwa kweli inaonekana kwamba tunafanya tu kwa sababu sheria imesema, lakini nia ya dhati ya kusaidia wakulima inaonekana haipo, wakulima wanauziwa mbegu fake, wanaletewa mbolea zisizofaa na kadhalika. Niombe sana tuimarishe huduma kwa wakulima wakati tunatambua kabisa kwamba mahindi ndiyo yanayoshikilia shilingi ya Tanzania iweze kuwa imara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikiendelea kwa suala la wakulima, lipo zao la viazi Njombe ambapo vinadhurika sana. Viazi tunalima Mkoa wa Njombe lakini vilevile Mkoa wa Mbeya, Tanga na Kilimanjaro. Viazi vya Tanzania vinaathiriwa sana na viazi kutoka nje hasa katika ujazo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hebu niombe sasa Serikali kupitia Idara ya Vipimo tutengeneze mifuko maalum kwa ajili ya zao la viazi. Mazao mengine kama kahawa na korosho yana magunia na viazi tuwekwe mifuko maalum ya viazi ambapo unajua kabisa piga ua mfuko huu hauzidi kilo 90 na huo ndio mfuko wa viazi, yeyote atayekutwa sokoni na mfuko tofauti na ile maana yake huyo awe ni mhalifu, itakuwa imeasaidia sana wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lipo zao la parachichi katika Jimbo langu la Njombe Mjini, parachichi za Njombe ni za export. Mwaka huu tume-export tani 700 lakini kwa bahati mbaya sana tuna-export kwenda nchi jirani na wale wa nchi jirani ndio wanapeleka Ulaya. Niiombe sasa Serikali itusaidie, wakulima hawa wa parachichi kwanza kabisa wapatiwe mbegu bora, lakini pia tupate wataalam kutoka Serikalini kwa sababu parachichi hizi ni za export maana yake tayari zitatusaidia kupata fedha za kigeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kwamba tatizo kubwa la parachichi ni kwamba hatuna pack house. Katika Halmashauri yetu tuna pack house moja tu na hawa wanaokuja kutoka nchi za nje kuchukua parachichi wanakuja na magari yao maalum yenye ubaridi. Kwa hiyo, Serikali ione kwamba kuna nafasi ya kuwekeza kwenye miundombinu ya ubaridi ili kusudi wananchi wanaolima parachichi waweze kupata mahali maalum pa kutunzia hizi parachichi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi kutokana na mfumuko wa kilimo hiki, wananchi wengi wameitikia sana na parachichi zinaendelea kuongezeka. Itusaidie kwamba sasa parachichi ziwe exported kutoka Njombe kwenda masoko ya nje Ulaya na kadhalika lakini tukipeleka Kenya maana yake wanatulipa Tanzanian shillings halafu wao ndiyo wanapata dola na sisi hapa tuna shida kubwa sana ya dola.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambao napenda kuliongelea ni umeme. Upo umeme wa REA Awamu ya Tatu lakini vilevile lipo suala la TANESCO. TANESCO ndiyo wanaweka umeme katika maeneo ya mijini pale Njombe tuna vijiji vilivyo karibu na mji kilometa tano kama Itulike havina umeme na havina umeme kwa sababu havimo kwenye REA, lakini vilevile vinatakiwa viwe TANESCO na uwezo wa TANESCO wa kupeleka umeme uko chini sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe kwenye bajeti itakayoandaliwa tuone TANESCO wanavyopewa miradi ya mjini angalau wapewe miradi unayokwenda mpaka kilometa tano, wanapewa mita 700, 600 au 300. Sasa utaona vijiji vilivyo karibu na mji havipati umeme, kwa hiyo, niombe sana hilo liangaliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili tuweze kufanikiwa kiuchumi tunahitaji barabara nzuri. Katika Jimbo langu la Njombe Mjini iko barabara inayoenda Ludewa inaitwa barabara ya Itoni – Manda. Awamu zote za uongozi zimekuwa zikiisemea barabara hii iwekwe lami, lakini mpaka leo katika Jimbo langu kazi hii ya kuweka lami haijaanza. Niombe sana katika Mpango ujao basi litekelezwe hili kwa sababu barabara hii inasaidia wananchi kusafirisha mazao ya kilimo lakini inasaidia vilevile huduma mbalimbali kwa Wilaya ya Ludewa na kuendelea mpaka Ziwa Nyasa huko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la elimu, tunahamasisha viwanda lakini tusipowapa elimu watu wetu hapa tunarudisha umanamba. Vijana hawa wataingia kwenye viwanda hivi watafanya kazi ya kupanga vitu kwenye maboksi na hatutajivunia kwamba vijana wetu wamepata ajira, itakuwa wamepata ajira lakini watakuwa wamepata ajira ya kijungujiko na yenye manung’uniko. Watakuwa watu wa kuhangaika tu kukunja mashati kuweka kwenye mifuko, tuwape elimu vizuri ya ufundi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika elimu ya ufundi ambayo tunapaswa kuwapa vijana hawa iko elimu inaitwa industrial maintenance. Katika industrial maintenance vijana watajifunza mambo yanayohusiana na marekebisho ya mitambo mbalimbali ndani ya viwanda. Leo hii VETA mtaala wanaotumia kufundisha, wanafundisha watu kutengeneza vigae vya moto wa mkaa, ndiyo ataenda kufanya kazi kiwandani huyo…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)