Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Mussa Bakari Mbarouk

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Tanga Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. MUSSA B. MBAROUK: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na mimi nichukue fursa hii kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutuwezesha kukutana katika Bunge letu hili tukajadili mambo ya nchi yetu na hususani Mpango huu wa Maenedeleo wa 2018/2019. Baada ya hapo vilevile pia bado niendelee kushukuru chama changu kwa nafasi niliyoipata. Lakini mimi nianze kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ukweli usiopingika kwamba Serikali yetu imekuwa na mipango sana. Lakini katika mipango hii mingi imekuwa haina tija, na nianze kwa kutoa mfano, tulikuwa na mpango wa MKUKUTA One, Two and Three lakini mpaka leo hatujui mpango ule umeashilia wapi. Umetajwa hapa asubuhi MKURABITA bado una matatizo, lakini pia palikuwa na Big Result Now hatuelewi imeishia wapi, lakini palikuwa na Kilimo Kwanza, watu wakakopeshwa matreka leo hii taarifa tulizozipata kwenye Kamati yetu imebidi baadhi ya matrekta yakamatwe kwamba watu wameshindwa kulipa.

Lakini pia palikuwa na mpango wa shilingi milioni 50 za vijana kila Wilaya hatujui umeashilia wapi, lakini vilevile palikuwa na mabilioni ya JK nayo haya tukiulizana sijui nani aliyepata. Lakini kama hilo halitoshi bado palikuwa na Mpango wa MMEM wa ujenzi wa shule za msingi na sekondari MMES, lakini bado palikuwa na mpango wa kujenga vituo vya afya kila kijiji nao hatujui umeashia wapi. Sasa napata taabu nkuona hii mipango tunayoipanga yote kwanini haina tija Watanzania wanatuelewa vipi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo mimi nilikuwa nashauri tu Serikali ni bora iwe na mpango mmoja ambao utakuwa unafuatiliwa na kufanyiwa tathimini kila baada ya mwaka mmoja na nusu kuona kwamba faida iliyopatikana kutokana na mpango huo ni ipi na kama hakuna faida basi mipango tuiache, lakini jambo lingine tumekuwa kukisema kilimo ni uti wa mgongo wa Taifa letu na 75% ya Watanzania wanaishi vijijini wamejiajiri wenyewe kupitia kilimo, lakini tujiangalie kama Taifa ni kweli tunathamini kwamba kilimo ni uti wa mgongo wa Taifa letu? Haiingii akilini kwamba kilimo ni uti wa mgongo wa Tifa letu lakini ni theoretically sio practically. Kwa hiyo, mimi niseme tu lazima kama kweli tumeamua kuwa kilimo ni uti wa mgongo wa Taifa tujue vilevile kwamba kilimo ndio kitakachotoa material ya kwenda katika Tanzania ya viwanda. Sasa kama kilimo chenyewe tumekipuuza leo tunajadili hapa masuala ya mahindi kukosa bei. Wananchi wameweza kufanya kazi kubwa sana bila ya kuwezeshwa na Serikali kwa mfano katika Mkoa ninaotoka mimi hatutumii pembejeo sisi tunalima kutokana na ardhi ambayo ipo na ina rutuba by nature. Lakini leo mahindi yamerundikana hayana bei wananchi wameshindwa kusomesha watoto wao, wananchi wanashindwa kuendeleza nyumba zao za kisasa. Serikali ndio inayozuia mahindi hasiuzwe nje ya nchi, sasa tujitazame tunafanana na nchi za wenzetu?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mahindi yana soko kwamba yanahitajika Southern Sudan, mahindi yanahitajika Kenya, mahindi yanahitajika maeneo ya Ethiopia huko, lakini sisi bado tunazuia mahindi yasiuzwe. Mimi niishauri Serikali tuondoe kikwazo kwa uuzaji wa mahindi, kama Serikali wakala wake wa chakula ameshindwa kununua mahindi haya tuwaache wafanyabiashara wenye uwezo, wanunue mahindi wauze katika nchi za nje. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama hilo halitoshi pia vilevile mazao kukosa bei mi naweza nikasema ni Serikali haikutaka kutafuta bei ya soko la mahindi. Kwa hiyo, lazima wananchi waache watafute soko wenyewe, haiingii akilini kwa sababu kwa mfano yupo mfanyabiashara mmoja wa mabasi anaitwa Sumry ameamua kuachana na biashara ya mabasi imeingia kwenye kilimo. Sasa hivi kweli anaweza akaamua kulima mahindi ya kula yeye mwenyewe binafsi, kwa ekari ya zaidi 10,000 au 15,000 alizokuwa nazo! Ni wazi anaamua kuingia kwenye kilimo afanye kilimo cha biashara, amevuna mahindi wanamwambia asiyauze, hapa hukumsaidia bali unamrudisha nyuma katika umaskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kama hilo halitoshi, ushauri wangu niseme pamoja na kuwaachia wananchi kutafuta masoko ya mahindi lakini basi tuwawezeshe kama tunaweka vikwazo hivi angalau tuwape mashine za kusaga unga sasa badala ya kupeleka mahindi ghafi, makapi ya mahindi yapaki kuwa vyakula vya mifugo kama ng’ombe wa maziwa lakini wauze unga angalau tumekuwa tumewasidia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, laini lingine nije katika suala loa uvuvi bahari kuu. Mimi ninatoka Tanga, Tanga tuna bahari kuanzia Jasini karibu na Kenya mpakani huko mpaka Kipumbwi karibu na Mkoa wa Pwani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Tanzania tumejaaliwa bahari kutoka Jasini mpaka Msimbati lakini ukiwatazama wavuvi wa ukanda wa Pwani ni maskini wa kutupwa hohehahe. Badala ya Serikali kuwasaidia imewarundikia kodi lukuki na ushuru mbalimbali, mimi niseme tu wavuvi tuwasaidie kwanza kwa kuwaondolea hizi ushuru na kodi mbalimbali, kwa mfano, mashua moja inachukua wavuvi 25 mpaka 30 lakini wavuvi hawa 30 kila mmoja anatakiwa awe na leseni ya uvuvi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa nini kwenye basi anayekuwa na leseni dereva peke yake turn boy hana leseni wala kondakta hana leseni, kwa nini kwenye vyombo vya uvuvi isiwe mwenye leseni nahodha peke yake?

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivi tuulizane Waheshimiwa Wabunge katika meli kubwa zinazokukuja kutoka nje kwa mfano ile meli iliyokamata na samaki waliyoitwa samaki wa Magufuli hivi wale watu wa mazingira waliwakamata wakawauliza mpaka mabaharia kwamba walikuwa na leseni ya uvuvi, kwa nini tunawaacha watu wa nje wanufaike tunawakandamiza Watanzania wazalendo wenzetu wadhalilike na waendelee kuwa maskini?

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naishauri Serikali iondoe...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)