Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Salim Hassan Turky

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpendae

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. SALIM HASSAN TURKY: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante na mimi nashukuru kupata fursa leo ya kuweza kuchangia. Awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu kwa kutujalia afya, sote tu wazima na tupo katika Bunge hili tukijenga Taifa letu. Pia nachukua fursa hii kumpongeza Rais wetu kwa kufanya maamuzi magumu ya kuongoza Taifa hili na kwa kweli anastahili kila sifa kwa nia yake njema ya kutaka kuifanyia Tanzania ya leo iwe ya viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya hayo sasa nataka niingie kwenye Mpango. Huu Mpango ni mzuri sana lakini kwa kweli heading yake ina matatizo tena ina matatizo makubwa sana. na matatizo yake Mpango unasema ni maendeleo ya Taifa lakini nikitazama tafsiri ya taifa siikuti Taifa bila ya Zanzibar. Katika mpango huu hakuna sehemu hata moja iliyotaja Wazanzibar na kwa kweli Mpango huu kwa njia moja au nyingine umetudhalilisha Wazanzibar kama vile hatustahili kupangiwa chochote katika Taifa letu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo, kama ni kosa basi nafikiri lirekebishwe kwa kuandikwa kwamba Mpango wa Maendeleo wa Tanzania Bara au uandikwe Mpango wa Taifa basi na Taifa la Zanzibar liwekwe katika Mpango huu lakini zero hakuna chochote. Hakuna mahali ilipoandikwa Pemba, Unguja wala Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hili sijui kama limefanywa kwa makusudi na kama limefanywa kwa makusudi basi naomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha awatazame sana watendaji wake kwa sababu yeye ni msimamizi wa sera pengine hakuwa na time nzuri ya kusoma, lakini kwa kweli hili limetuangusha sana Wazanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka niseme kwamba kuna watendaji wa Serikali ambao kwa kweli hawaitendei haki Zanzibar na hasa katika mambo ya kufanya biashara baina ya Zanzibar na Bara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Kamati zilizopita tulipata bahati ya kutembelea mipaka yetu, tulikwenda mpaka wa Sirari tukaona wafanyabiashara wadogo sana kila mfanyabiashara ana baiskeli ya rally nzuri madhubuti, lakini kazi yake yeye akiamka asubuhi anasukuma baiskeli kupita boarder anakwenda zake Kenya anachukua dumu la mafuta analeta, akimaliza kinachotakiwa Kenya anakichukua kwa baiskeli anaenda zake anapeleka na hakuna anayemuuliza kwa sababu ni mwananchi anayeishi maeneo yale, kwa hivyo, biashara hiyo inafanyika kwa baiskeli lakini unaweza kukuta ikifika jioni basi canter zima mtu kapenyeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sisi upande wa Zanzibar, leo miaka saba mimi nipo katika Bunge hili, kuna jambo moja dogo sana ambalo linatudumaza sisi Wazanzibar nalo ni lile la longroom pale Dar es Salaam. Wafanyabiashara wanaokuja sasa hivi kama mnavyojua Zanzibar inasifiwa kitalii, tuna utalii wa nje na wa ndani. Hawa watalii wa nje wakija kutembea Zanzibar mtu akinunua chochote Zanzibar akifika longroom pale akionesha risiti anaambiwa hapana tuoneshe na document ya importation ya kitu hiki, hivi kweli tunatendewa haki jamani Wazanzibari na Waziri wa Fedha upo? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili ninaomba sana lishughulikiwe kama wewe kweli ni muumini wa haki basi hili naomba ulisimamie Wazanzibar wasinyanyaswe pale. Mtu akija na tv moja ni biashara ni sawa sawa na mtu ambaye amenunua Morogoro akaja Dar es Salaam. Sasa leo ninashangaa leo watu wakienda wakinunua kitu kidogo Zanzibar akipita pale inakuwa kesi kubwa sana. Kwa hivyo, hilo ninaomba safari hii angalau tuhakikishe adha hii hii ndogo basi iishe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukiacha hilo, tunazungumzia uhusiano wa mapato baina ya wananchi kulipa mapato na Serikali kupokea mapato. Lakini TRA ilipoanzishwa kulikuwa na kauli mbiu inatumika kwamba sisi ni partners katika maendeleo ya nchi yetu, sasa hivi tafsiri hiyo inaondoka. TRA sasa hivi wamekuwa ni watu wa bunduki, watu wa kutumia nguvu, wanaingia kila mfanyabiashara anatafirika. Wewe mwenyewe ulitoa tafsiri katika mwaka uliopita ulisema maduka 4,000 yamefungwa, hiyo ni kwa sababu ya ukali wa TRA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, yako mambo yanazungumzika, Serikali hii ilipoingia madarakani, Serikali iliyopita ililegeza mambo mengi sana, ninyi mmeingia mmekaza, mna haki ya kufanya hivyo, hakuna tatizo. Lakini kwa nini mnawaadhibu hawa kwa awamu iliyopita na awamu hiyo wewe Waziri, Rais wetu, sote tulishiriki, tulikuwemo katika Serikali iliyopita. Na sote kama kuna makosa yalitokea basi sisi pia ni wakosa wa Serikali iliyopita. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Serikali hii ilishaamua kwamba twende vingine, basi tukubaliane kwamba twende kwa mwendo tunaotakiwa. Sasa tusiambiwe kwa makosa ya Serikali iliyopita, Serikali hii naiheshimu sana na tunataka tufanye kazi kwa pamoja na tuitekelezee kila wanachokitaka, tutakaza miguu tutafuata. Sisi private sector tunaamini kabisa mpango wa Rais wetu Dkt. Magufuli wa kutaka kuendeleza viwanda ni mzuri sana na utafuzu kwa nguvu zote, na yeye ana nia njema kabisa, lakini watendaji wetu wanatuangusha. Naomba Mheshimiwa Waziri hili ulisimamie kwa nguvu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo nalo ni muhimu, wakati wa awamu zote zilizopita, biashara baina ya Bara na Visiwani, sisi Visiwani tunaitegemea Bara kwa asilimia 90 kwa maisha yetu ya kila siku Zanzibar. Unachosema wewe sisi tunanunua Bara ndiyo tunapeleka Zanzibar. Lakini awamu zote zilizopita kulikuwa na ulegevu fulani pale bandarini Wazanzibari waweze kuleta bidhaa zao ziuzike, sasa hivi awamu hii imetu-tag sisi Wazanzibari ni wezi, hatutaki kufanyiwa biashara, biashara yetu ni kuiba tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa kutokana na fursa ambazo tulikuwa tukipewa na awamu zilizopita, naiomba awamu hii kwa sababu wamekaza kamba sasa wakubaliane na hii hoja ambayo naiomba kwako wewe Waziri kwa kupitia Mwenyekiti.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni kwamba mazingira ya kufanya biashara Zanzibar na Bara ni mawili tofauti kabisa katika East Africa nzima. Sisi leo kama tutaagiza mzigo kutoka nje, tukauleta Zanzibar, basi tutalipa kodi pale, tutaushusha mzigo Zanzibar, utaenda zake godown, atakuja mteja ataununua mzigo ule utapakiwa tena kutoka godown utakuja bandarini utapakiwa katika vyombo utakuja Bara, utapakuliwa, utakaguliwa, halafu upakuliwe tena ndiyo ufike sokoni, angalia safari zako hizi zote zilizopita, ni gharama mno kwa kufanya biashara Zanzibar.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Zanzibar kama tunavyojua, miaka yote nenda rudi ndicho kituo cha kufanya biashara na sisi sote nguvu zetu tuko katika kuendeleza Zanzibar iwe kituo cha biashara. Na hili nataka niombe sana Serikali yetu, tusione kwamba Wazanzibari ni wakorofi, tuone ni ndugu zetu ambao tunataka tushikamane nao, leo uchumi wa Zanzibar ukikua ndiyo uchumi wa Bara unakua. Haiwezekani uchumi wa Zanzibar ukawa mzuri wa Bara ukawa chini. Bado BOT ndiyo regulator wetu, haiwezekani uchumi ukawa wa upande mmoja na wa upande mwingine usiwe, uchumi wetu utakuwa chini tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kutokana na hilo, naomba sana hizi tozo za TRA kwa maana ya duty, sales tax na nini zilizoko katika Muungano wetu, kwa Zanzibar tufikiriwe angalau tushushiwe. Kwa Zanzibar, kama Dar es Salaam ni 25 percent, basi Zanzibar iwe 25 percent lakini database ile ile ikubalike. Mtu akishalipa kodi pale basi sawa iwe mzigo ule kutoka Zanzibar kuja Bara iwe ni rahisi wala hakuna matatizo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hivi tunavyofanyiana ni sawasawa na mfanyabiashara mkubwa kumuua mdogo. Uchumi wa Zanzibar huwezi ukaulinganisha na uchumi wa Bara. Kwa maana hiyo, mtazame kwamba katika kutekeleza ni kwamba lazima kila mtu alipe kodi kwa uhakika wake na uhalali wake. Basi sasa tuangalie kodi zetu nazo ziwe rafiki kwa pande zote mbili. Hiyo inakuwa ni double taxation.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo naomba sana Wizara ya Fedha ilitazame ni kwamba awamu iliyopita ukienda TRA kodi watu walikuwa wakilipa basi mara nyingi sana ni ile kodi ya chini kabisa mtu ndiyo bei anayotiliwa analipa, ukiingia sokoni bidhaa zinauzika, au analipa kodi bei ambayo hata katika database haipo, lakini inapitishwa watu wanalipa.

Awamu hii Ma Sha Allah imekuja vizuri sana mna- collect kodi vizuri sana, lakini kilichotokea, watu badala ya kutazama database bei za chini au za kati, wamekwenda kuzivamia za juu kabisa. Kilichotokea ni mfumuko wa bei kwa Tanzania nzima, vitu vyetu sisi vimekuwa ghali. Na kama unajua soko la Kariakoo ndiyo centre ya kulisha; Burundi, Rwanda na Kongo wote wananunua Kariakoo, bidhaa nyingi sana pale. Na ninaamini karibu asilimia 30 mpaka 40 ya kodi inatokana na Kariakoo. Lakini leo maduka yale yote yamekufa kwa sababu ya kodi kutozwa namna hiyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ombi langu kwa Seriikali yangu ni kwamba hizi tozo tusitafute hiyo njia ya panya isiwepo, lakini hizi kodi angalau zitazame pale database bei ya chini. Kitakachofanya sasa hivi biashara hizi zinakuwa tena kwa nguvu sana, lakini sio Tanzania, watu wanakwenda kununua Kenya, soko hili la Rwanda, Burundi, Kongo, sasa hivi mambo yote watu wanakwenda kununua Mombasa, Nairobi, ndipo inapofanyika biashara hii. Tulioumia ni sisi Watanzania, biashara imeanguka kwetu, kwa hiyo hili nalo litazamwe.