Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushuru sana kwa kunipa nafasi ili nami nichangie katika hoja hii iliyo mezani kwetu. Hata hivyo, kabla sijachangia, nataka nichukue nafasi hii kumshukuru Mwenyezi Mungu na daima nitaendelea kumshukuru kwa uponyaji ambao amefanya kwa Mheshimiwa Tundu Lissu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivi kwa sababu wale waliobahatika kumwona Mheshimiwa Tundu Lissu siku ambayo watu wasiojulikana walikuwa wamedhamiria kudhulumu maisha yake, wataamini kabisa kwamba uponyaji wake ni mpango wa Mungu. Ndiyo maana kwa kweli binafsi nikisikia tukio la kuumizwa Tundu Lissu likiongelewa kwa dhihaka, kejeli, dharau kwa kweli linanikasirisha kupindukia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, asubuhi baada ya Waziri Mkuu kujibu vizuri swali la Kiongozi wa Upinzani Bungeni, Mheshimiwa Mlinga alikuja na mwongozo na uliojaa kejeli. Mwongozo ule ulimhusisha Kiongozi wa Kambi ya Upinzani Bungeni na mauaji ya albino, jambo hili halikubaliki. Ombi au pendekezo la Kiongozi wa Kambi ya Upinzani kwa Serikali kuhusisha Wachunguzi wa Kimataifa ni pamoja na baadhi ya matendo ambayo yamekuwa yakitokea katika nchi hii na kufumbiwa macho. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Watanzania wanakumbuka na sisi tunakumbuka kwamba, Mheshimiwa Goodluck Mlinga alihusishwa na kumuua mpenzi wa mpenzi wake.

T A A R I F A . . .

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nimemsikia na huo ni mkuki kwa nguruwe kwa binadamu mchungu. Gazeti la Dira liliandika vizuri sana kwamba mpenzi wako alikusaliti, wewe na kundi la vijana wenzako mkaenda kumuua, limeripotiwa Polisi, limeripotiwa kwenye magazeti na hujakanusha hadi hivi leo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeiomba Serikali katika uchunguzi wa nani walihusika kutaka kudhulumu maisha ya Mheshimiwa Tundu Lissu, huyu ambaye alikwishatajwa kwamba alihusishwa na mauaji uchunguzi uanzie kwake.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nitakwenda kwenye hoja.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ambalo napenda kulizungumza ni kushauri Kiti chako. Jana kuna mwenzetu mmoja katika mchango wake alihusisha Bunge hili na ubaguzi. Namshukuru sana senator Ndassa kwa jinsi alivyojenga hoja yake asubuhi na kututahadharisha kwamba tusije tukaigawa nchi kwa sababu ya hisia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hili kwa sababu nakuomba kama ikikupendeza Hansard ya jana ya hotuba ya Mheshimiwa Musukuma iangaliwe kwa sababu…

TAARIFA . . .

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kimsingi sijapewa taarifa na kwa sababu hiyo naomba niendelee kukushauri. Nashauri ile hotuba yake iangaliwe kwa sababu ndani ya ile hotuba kuna maneno haya ambayo ni maneno mabaya kama yataachwa kwenye ile hotuba kwamba, wakati mnakula vizuri sisi tulikuwa kimya sasa zamu yetu mnapiga kelele. Naomba kama haya maneno yako kwenye Hansard yaondolewe kwa faida ya vizazi vijavyo. Haya maneno siyo mzuri, haya maneno ni mabaya. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, sasa niingie kwenye Mpango. Mimi simlaumu Mheshimiwa Waziri wa Fedha kwa hoja yake aliyoileta Mezani kwa sababu wajibu wetu ni kumshauri ili baadaye atuletee Mpango. Namshukuru pia Spika kwa jinsi alivyotuweka sawa asubuhi. Mheshimiwa Mpango yuko hapa kutusikiliza ili tumsaidie aweze kuchukua hoja zetu, baadaye azifanyie kazi ili tuweze kuwa sasa na Mpango wenyewe. Mimi ninachoelewa kilicho mbele yetu ni Mapendekezo tu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza napenda kuzungumza kuhusu gesi ambayo nchi hii inayo. Kamati ya Bajeti ilipata bahati ya kwenda Mnazi Bay na Msimbati. Gesi tuliyonayo ni nyingi kwelikweli, ni nyingi sana lakini hatuna uwezo wa kutumia robo tatu ya gesi tunayozalisha. Kinachotokea ni ukiritimba wa TPDC kwa sababu M&P ambao wanazalisha hii gesi wanaiuza kwa TPDC na wanaiuza kwa TANESCO Mtwara na ukiritimba huo unafanya sasa ile gesi isilete faida yoyote katika nchi.

Mheshimiwa Spika, ushauri wangu ni kwamba kama mikataba ambayo Serikali iliingia na M&P ikirejewa vizuri ile gesi inaweza ikauzwa kwa makampuni mengine, inaweza ikauzwa kwa watu binafsi. Kwa kufanya hivyo uko uwezekano hata wa kupunguza mafuta ya mitambo ambayo tunaagiza kutoka nje, mafuta ya magari tunayoagiza kutoka nje na kuokoa pesa nyingi sana za kigeni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mataifa mengi sasa hivi yenye gesi magari yake yanatumia gesi. Gesi inatumika majumbani, hakuna sababu yoyote ya kutojengwa kwa vituo vya kuuzia gesi kama vile vituo vya petrol na diesel na kufanya magari yetu yakatumia gesi. Ni kitu kidogo sana tu kwa sababu katika gari utahitaji kuwa na mtungi tu kwa ajili ya gesi na kwa sababu hiyo tutaokoa pesa nyingi sana.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naishauri Serikali ifanye kila linalowezekana ili gesi ambayo inazalishwa kwa wingi itumike katika uendeshaji wa magari na maeneo mengine na ikiwezekana TPDC sasa iweze kutoa master plan ya namna ambavyo gesi hiyo itafika katika Mikoa ya Kanda ya Ziwa, Mikoa ya Kaskazini, Mikoa ya Nyanda za Juu hata na Mikoa ya Kusini ili tuweze kuokoa uharibifu wa mazingira na vilevile tuweze kuokoa pesa nyingi sana za kigeni ambazo zinatumika kwa ajili ya kuagiza mafuta. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kuzungumza ni kuhusu kilimo chetu. Zamani kahawa, pamba, mkonge, pareto na kadhalika ni mazao ambayo yalikuwa yanatuingizia fedha nyingi sana za kigeni lakini sasa hivi maeneo ambayo yalikuwa yanalima pamba zamani pamba hailimwi tena kwa sababu wakulima wanakata tamaa, maeneo yaliyokuwa yanalima kahawa hivyohivyo na kadhalika na kadhalika. Sasa tunazungumza habari ya Tanzania ya viwanda lakini Tanzania ya viwanda itapatikana namna gani kama hatuwezi kuwahamasisha wakulima wetu tukapata malighafi. Naomba mpango utakapokuja uje na mkakati mahsusi kabisa wa namna ambavyo tutabadilisha kilimo chetu kiwe cha kisasa zaidi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo kulikuwa na ule mpango wa SAGCOT ambao ulikuwa ni mradi mkubwa kabisa. Niseme wazi kabisa kwamba sipingani na mradi wa Stiegler’s Gorge wala siko kwenye hoja ya UNESCO na mambo mengine, lakini nataka kusema wataalam wametafakari namna gani mradi wa Stiegler’s Gorge na mwingiliano wa ule mkakati wa SAGCOT labda pengine ule mkakati umefutwa au namna gani. Kwa sababu yako mazao madogo madogo ukiacha haya mazao makubwa ya biashara ambayo yanaweza yakaibadilisha nchi hii. Tunaweza tukauza nje mananasi, maembe, nyanya na kadhalika na matokeo yake hivi ndiyo vitu vidogo ambavyo vinaweza vikafanya watu wa kawaida kuonekana kwamba Serikali inawajali na kipato chao kinaongezeka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nizungumze kuhusu ujenzi wa reli yetu, hili ni wazo ambalo hakuna mtu hata mmoja ambaye anaweza akalipinga, tunahitaji reli kutoka Dar es Salaam kwenda Isaka, Kigoma, Karema, Tanga na Moshi. Hoja ni hii tutaweza kwa pesa zetu? Naomba Serikali iseme fedha za kujenga reli hii tunazipataje? Hizi fedha shilingi trilioni 16 kwa ajili ya ujenzi wa reli kuzibeba peke yetu kama nchi maana yake ni kuacha shughuli nyingine za huduma kwa jamii, ni lazima zitaathirika.

Mheshimiwa Spika, kwa sababu hiyo nasema kama walivyosema wenzangu tusione aibu hata siku moja kushirikisha private sector. Wako watu duniani kama Serikali ikidhamiria miradi hii mikubwa tunaweza tukaingia nao ubia ikafanywa vizuri kabisa. Kwa sababu hii reli lazima iwe ya kibiashara kama sisi tutaamua kukopa reli ifike mpaka hapa Dodoma halafu tushindwe kuiendeleza lazima kama nchi tutafakari hizi fedha tutazirejesha namna gani kwa sababu ikifika Dodoma itakuwa ni ya huduma tu haitaweza kuwa ya biashara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, lazima Mpango utakapokuja Waziri Dkt. Mpango atuambie ni maeneo gani ambayo yanaweza yakanyanyua uchumi ambayo tunaweza tukashirikiana na private sector. Eneo kwa mfano la ujenzi wa barabara, wamesema wenzangu wengine Mheshimiwa Adadi amesema kuna barabara nyingine ambazo Serikali haihitajiki kujenga sasa, kuna watu binafsi wanaweza wakajenga halafu wakaingiza road toll. Kwa hiyo, hii sheria ya PPP tusiiweke tu kwenye vitabu, tuangalie namna ambavyo itafanya kazi kwa manufaa ya nchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo napenda kulisema kuhusiana na hilo, tusiwanyanyapae wafanyabiashara. Wafanyabiashara wanalalamika na wanalalamika kwa sababu inaonekana kana kwamba Serikali inataka kurudi katika ukiritimba wa Serikali yenyewe kufanya biashara. Miradi ya ujenzi sasa inakwenda JKT inarudi Serikalini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni lazima tuhakikishe kwamba tunai-boost private sector kwa sababu Serikali ndiyo yenye pesa ifanye ubia na private sector ili wananchi waweze kunufaika kwa sababu private sector kwa kiwango kikubwa ndiyo inayotoa ajira kwa watu wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru.