Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango na Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakupa shukurani kwa kunipa fursa hii na mimi niungane na Waheshimiwa Wabunge kuwapongeza Mawaziri walioteuliwa na kumshukuru Mheshimiwa Rais kwa kuwateua watu ambao nafikiri wataongeza kasi yake ya kuendesha nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, uchumi ni siasa na siasa ni uchumi na uchumi ambao unategemewa ni ule ambao una mipango mizuri au mpango mzuri. Waheshimiwa Wabunge mtakubaliana na mimi kwamba mpango wa miaka mitano ambao unatekelezwa kila mwaka ni mpango mzuri ambao tumeupitisha na kilichobaki sasa ni utekelezaji. Kwa hiyo, mpango ni mzuri na aliyeuandaa ni Mpango huyu Mheshimiwa Waziri, na ninajua alivyohangaika na kuja na mpango huu mzuri kwa kweli kwa hilo nampongeza. Na azma ya Taifa kupitia mpango wa miaka mitano unaotekelezwa klia mwaka kwa vyovyote vile ni kufikia dira ya 2025. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, Mheshimiwa Mpango watu wengi wanakutegemea na nina hakika umefanya hivyo kuona kwamba dira yetu ya 2025 inataka nini na kuona mipango hii kila mwaka kama inatupeleka kule. Na mpango huu unatekelezwa kupitia bajeti ya klia mwaka na azma yetu ni kuwa na uchumi wa kati na wa viwanda, sasa katika mipango hii kuna vipaumbele vilishaonyeshwa na ni kiasi gani cha uchumi kitakuwa ambacho kinatufikisha kule ambako tulitegemea kwenda. Kama tunaenda kwa mpango wetu uchumi wa mwaka huu ungekuwa unakuwa kwa 8% mpaka 10% kufidia kule ambako nyuma tulikuwa hatujafikia kule tunakotakiwa na inawezekana kwa sababu miaka iliyopita tulishafika 8% na zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ilivyobaki sasa ni kuangalia kwanini sasa uchumi unakuwa kwa 6.8% ambayo ametuletea sisi ambayo sio 8%, na kazi yetu Waheshimiwa Wabunge ni kuonyesha mapungufu yako wapi na kuishauri Serikali ifanye nini kusudi tusonge mbele na mimi nitatumia muda wangu zaidi katika kuonyesha tufanye nini ili tupige hatua. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, wanaotekeleza mpango huu sio Serikali peke yake, sekta binafsi na wananchi kwa ujumla tunapaswa kutekeleza mpango huu. Tutakachouliza kwa Serikali na ninachoomba kwa Serikali ni kuiwezesha sekta binafsi na wananchi kusaidiana na Serikali kutekeleza mpango huu utufikishe mbele na kwa upande wa Serikali unachangia kupitia bajeti ya Serikali, kwa hiyo, tuseme kwa kiingereza tuwe na consistency ya kukusanya mapato bila kuua uchumi. Mimi ndio ushauri wangu kama VAT inapunguza production angalieni! Kama VAT inapunguza ajira angalieni! (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninataka niwaambie hakuna shamba linalovunwa bila ya kupanda, hakuna uchumi utakaokuwa bila investment au uwekezaji haiwezekani. Kwa hiyo, tuangalie kama uwekezaji unakwenda kwa principal ambayo tunataka uchumi wetu ukue. Kuna jambo ambalo siku zote nimelishauri na hata mimi mwenyewe nimejitahidi ni kuweka One Stop Center kwa ajili ya investors ili wasihangaike hangaike na kupoteza muda. Muda ukishakwenda haurudi ndugu zangu.

La pili ni kwamba, pale sasa hivi huu uchumi unaokuwa kwa 6.8 unatokana na sectors ambazo sio za watu wengi, wamesema wengine. Kwa hiyo, ndugu zangu tuangalie ni sekta zipi na bila mjadala na wengi wamesema kwamba sekta ambayo itaifanya viwanda vifanye kazi nchi hii ili vipate malighafi na chakula kwa wafanyakazi ni sekta ya kilimo, Mheshimiwa Mpango angalia bajeti ya mwaka juzi na mwaka jana kama tunaongeza bajeti ya kilimo bila ya kutafuta visababu sababu. Bila ya kilimo kama walivyosema wengine ndugu zangu hatuwezi kwenda popote kwa sababu malighafi itatokana na kilimo lakini kilimo ndicho kinachoajiri watu wengi nchi hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sio hivyo, hata wafanyakazi wa viwandani baadaye watapata chakula chao wapi? Ni kutokana na kilimo. Lakini sio hivyo, leo utaona ajabu, mimi ni Mwenyekiti wa Kamati hiyo ambayo Mheshimiwa alitaja asubuhi kwamba unaona Songea na Kusini kule bei ya mahindi ni shilingi 25,000 kwa gunia lakini Serengeti na Maswa ni shilingi 80,000 mpaka 100,000 na zaidi. Kwa nini kuna tofauti hii? Lazima kuna tatizo na ndilo ambalo tunapaswa kuliangalia. Mimi siamini kama uchumi umerudi kwenye ujamaa, huu ni uchumi wa soko lakini Serikali lazima i-regulate, ione kwamba bei ya Kusini inapanda na ione kwamba bei ya chakula kule Kaskazini inashuka na tulimwambia Mheshimiwa Waziri kwa nguvu zote na nilitegemea ametekeleza kwamba hakikisha NFRA iweze kwenda kununua mahindi kule ili bei kidogo ipande na ipeleke kule ili bei kidogo ishuke kwa chakula. Lakini hatujui kama amefanya hiyo ripoti kama sekretarieti inaleta itakuwa imefika kwako. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mheshimiwa Waziri alipaswa aeleze ame-act namna gani na hapo ndipo ambapo tunaleta matatizo, lakini kwa kilimo lazima kuwe na tija. Tija ya kilimo inatokana na pembejeo na zana, lakini ukiwa umelima sana hamna soko ni sawasawa na kutupa shilingi chooni. Lazima tuwe na masoko, lakini kazi ya masoko ya kilimo haiko kwenye Wizara ya Kilimo, iko kwenye Wizara ya Viwanda na hatujawahi kusikia viwanda ikiongelea masoko ya mazao ya kilimo hata siku moja. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini sio hivyo, namna ambavyo Wizara ya Viwanda inaweza kutengeneza masoko ya mazao ya kilimo ni kuanzisha viwanda vitakavyoongeza thamani ya mazao ya kilimo, hilo ndilo soko la uhakika. Kwa hiyo, tuangalie bajeti kama inafanya hivyo, kama hivyo vipaumbele tunaviweka kama inavyotakiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kwamba Mwenyezi Mungu ameijaalia Tanzania. Tuna rasilimali nyingi, tuna madini, tuna vito, tuna ardhi na tutakachoweza kufanya nchi hii iendelee ni kuongeza thamani ya rasilimali hizi. Sasa wamesema kwamba kuna mfumko wa bei, kuna mfumko wa bei nzuri na mfumuko wa bei mbaya. Kama mfumko wa bei unatokana na credit squeeze au kuondoa money kwenye circulation hiyo sio nzuri sana. Mfumko wa bei unapaswa kupungua kwa kuongeza uzalishaji na chakula nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lazima tu-manage hayo mambo, tunataka au hatutaki lazima tuya-manage. Sasa sio mfumko wa bei tu kuwa chini ndiyo sifa, umetokana na nini? Tujue kwa nini hakuna hela kwenye circulation, na kama hakuna hela namna ya kuwekeza ndani ya nchi ni kutokana na mikopo au equity. Hamna namna nyingine, kutokana na hela yako mwenyewe au kutokana na mikopo. Angalieni wenye hela kama wanawekeza, angalieni mabenki kama yanatoa mikopo kwa ajili ya uwekezaji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, zamani nilivyokuwa viwandani nilikuwa kwenye bodi ya benki moja. Ilikuwa inatoa hela kidogo sana kwenye kilimo na ilikuwa inatoa hela kwenye biashara nyingi. Kwa hiyo zile hela zikawa zinakwenda kuzungusha vitu ambavyo havitokani na production ndani ya nchi yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, tuangalie hayo mambo na mimi mwenyewe na Mheshimiwa Mpango kama unataka tunaweza tukakaa pamoja, tukaangalia hayo mambo tutayafanyaje? Na fahari yangu ni wewe ufanye vizuri na kufanya kwako vizuri ni kufanikisha uchumi wa nchi hii. Serikali imefanya makusudi kuweka uwekezaji na Wizara ya Fedha pamoja, sasa usiuzuie uwekezaji ukawa mdogo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala lingine ambalo tunapaswa kuwa na kipaumbele ni miundombinu kwa sababu bila miundombinu soko haliwezi kufikika na pembejeo haziwezi kufika kwenye kilimo. Lingine jamani ni kwamba tuone ajira kama inapungua nchi hii au inaongezeka, vijana ni wengi na nguvu kazi ni nyingi, kama ajira haiongezeki maovu yataongezeka ndani ya nchi yetu na hilo lita-affect uchumi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa nataka nisisitize kwamba jamani One Stop Center iko kule Rwanda tukaiangalie, tuilete Tanzania na halafu tuweke ile Logistic Centre pale Kurasini ndipo tutaona demand kubwa ni ya nini halafu tunawekeza na mengine yote ambayo tunaweza kuyafanya ili uchumi wetu uweze kupiga hatua. Serikali ijaribu kuona kwamba private sector jamani inakuwa na confidence, Serikali iweze kuona kwamba private sector iwekeze na wakipata faida watoe kodi, bila kodi na wao hawawezi kuendelea kuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninaomba tuangalie upya kama sera inatekelezwa vizuri kwa sababu kuwa na sera nzuri si jambo la muhimu sana ni kuwa na sera ambayo inatekelezeka na inatekelezwa. Kwa kweli huu ni uchumi wa soko na private sector kama walivyosema wengine ndiyo engine na hiyo engine isipokuwa inafanyiwa maintenance kila wakati na kuangalia mahitaji yao itabaki Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo moja nataka nilisahihishe, mahali ambapo private sector haifiki, Serikali lazima iende. Kwa hiyo, kama shipping haiendi vizuri kwa kuwaachia private sector peke yake sioni ajabu kama Serikali inakwenda pale. Kwa hiyo, Serikali haiendi sana kwa ajili ya faida, Serikali inaenda kwa ajili ya mahitaji. Kama wananchi wanahitaji jambo na sekta binafsi haiendi lazima Serikali iende, kwa hiyo makampuni ya Serikali lazima yaendelee kuwepo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hivyo ndugu zangu tukosoe Serikali lakini tukosoe kwa namna ambayo tunaishauri na tunasaidiana nayo kufanya uchumi wa nchi hii kushamiri na nina hakika ni rahisi kutoka katika ukuaji wa uchumi wa asilimia 6.8 kwenda 8 mpaka 10.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nilifanya thesis yangu ya kuondoa umaskini na kukuza uchumi. Wakati nilipofanya nafikiri ni mwaka 2002 au 2003, niliona kwamba kukua kwa uchumi kwa asilimia 11 ndiyo mahali ambapo tuna uhakika na kuondoa umaskini wa Tanzania. Inaweza kuwa chini, inaweza kuwa juu zaidi lakini asilimia 11 ndiyo ukuaji wa uchumi ambao utatuhakikishia Tanzania kupiga hatua mbele kiuchumi na kupunguza umaskini na kuongeza ajira na kuleta maisha mazuri kama dira yetu inavyosema.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.