Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Oran Manase Njeza

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbeya Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. ORAN M. NJEZA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana.

Kwanza nianze kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Wizara nzima ya Fedha kwa mwongozo mzuri wa mpango wa mwaka 2018/2019 na kweli unatuonesha mwelekeo mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi naomba nijikite zaidi kwenye vipaumbele vile vinne vya mpango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kipaumbele cha kwanza kinaelezea kuhusu viwanda vya kukuza uchumi na ujenzi wa msingi wa uchumi wa viwanda na mimi naona hiki ni kipaumbele kizuri sana; lakini ningependa zaidi kuona kwamba hiki kipaumbele kinajikita zaidi kwenye kilimo kwa sababu viwanda vyetu, uchumi wetu wa Tanzania kwa kiasi kikubwa utategemea kilimo ambacho kinaajiri zaidi ya asilimia 75 ya Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, namuomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja na mpango wake kwa mwaka huo pamoja na bajeti, uangalie ni namna gani utajikita kuinua kilimo Tanzania kwa sababu hiki kilimo ndio kitatupelekea kupata malighafi kwa ajili ya viwanda vyetu. Nalizungumzia hilo la kilimo kwa sababu kubwa ambayo imejitokeza hivi karibuni. Wakulima kwa kiasi kikubwa wamezalisha sana mazao, hasa nafaka. Hata hivyo leo hii ukiangalia bei ya nafaka hasa mahindi na mbaazi ziko chini sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa Serikali ijaribu kuangalia ni namna gani iwasaidie wakulima yale mazao wanayoyazalisha bei iweze kuwa inaeleweka, kuwe na price stabilization. Vilevile kuwe na masoko ya uhakika. Tusipokuwa na masoko ya uhakika, bei ya mazao yetu isipoeleweka kwa kweli nchi yetu itakuwa katika hali ambayo sio nzuri na uchumi wetu utakuwa katika hali mbaya kwa sababu bei zetu za mazao ukilinganisha na wenzetu sisi zipo chini sana. Kwa hiyo, ningeomba hapa Serikali iangalie jinsi gani ambavyo tutaanzisha masoko ya mazao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jana nimesikiliza kwenye taarifa ya habari walikuwa wanazungumzia kuhusu commodity exchange market. Ikianza mapema hiyo nafikiri inaweza kutusaidia sana kuhakikisha kuwa mazao yetu yanakuwa na bei inayoeleweka na vile vile kunakuwa na masoko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kilimo kinahitaji zaidi pembejeo, napenda niishukuru Serikali kwa mpango wake wa kuagiza mbolea kwa jumla (bulky procurement); hii imesaidia sana kiasi ambacho mbolea leo za DAP bei imeteremka karibu nusu. Kwa kule kwetu DAP inanunuliwa kwa shilingi 51,000 kwa mfuko wa kilo 50 na Urea inanunuliwa kwa shilingi 41,000 kwa mfuko, hayo ni mafanikio makubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hizi mbolea kushuka bei namna hiyo bado ninaona kuna njia ambazo zinaweza kusaidia mbolea ikashuka zaidi; kama tukiboresha zaidi miundombinu ya barabara na miundombinu ya reli. Kwa sehemu ambazo tuko ukanda wa reli ya TAZARA, kama TAZARA ikiboreshwa, bei ya mbolea inaweza kushuka zaidi. Kwa hiyo, ninaomba katika hiki kipaumbele cha kufunganisha uchumi na maendeleo tuangalie zaidi ni namna gani wananchi wanaweza kufaidi bei ya pembejeo zikawa chini zaidi kwa kuboresha huduma za miundombinu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nafikiri vilevile Serikali iliangalie suala la afya, hasa miundombinu ya afya. Wananchi wamejenga zahanati nyingi, wamejenga vituo vya afya na bado vipo kwenye mtambaapanya wakitegemea kuwa Serikali itakuja kumalizia. Katika huu mpango unaokuja katika hii bajeti inayokuja ninapendekeza kipaumbele kiwe kumalizia hizi zahanati na vituo vya afya ambavyo kwa kiasi kikubwa wananchi wameshajenga na wengine bado wanaendelea kujenga. Kwa hiyo, upendeleo uwe kwa wananchi wale ambao wameshafikia hatua nzuri, tuweze kuwatia nguvu ili waweze kuendelea kuchangia katika ujenzi wa nchi hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ni suala la maji. Maji kwa wananchi wetu hasa vijijini na mijini ni muhimu sana, kwa hiyo, tunapoangalia maendeleo tuangalie ni namna gani hii miundombinu ya maji hasa kwa vijijini itaweza kuboreshwa. Kwa kiasi kikubwa Serikali imewekeza sana kwenye miundombinu, imetoa hela nyingi sana kwa ajili ya miundombinu ya maji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini hii miundombinu sehemu nyingi likiwemo Jimbo langu la Mbeya Vijijini bado haifanyi kazi. Ukiangalia kwa kule Mbeya Vijijini tulipata miradi ya vijiji kumi na miradi ile asilimia 80 ya pesa ilishakwenda, lakini mpaka leo ni mradi mmoja tu ndiyo umekabidhiwa. Sasa katika hii bajeti, iangalie ni namna gani hii miradi iweze kukamilika ili tuweze kuanzisha miradi mingine.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile katika miradi ya maji ninapendekeza kwa kule Mbeya tungeanza na vyanzo vingine mbadala. Kuna chanzo cha Mto Kiwira, naomba kipaumbele kiwepo cha chanzo cha Mto Kiwira kwa ajili ya kupeleka maji Wilaya yetu ya Mbeya hasa Jimbo la Mbeya Vijijini, nafikiri itatukomboa kwa kiasi kikubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo linaweza kutusaidia katika mpango mzima wa maji nafikiri ni kuunganisha hizi mamlaka; mamlaka za maji mijini na mamlaka za miji midogo (clustering). Kwa hiyo, napendekeza katika mpango wa bajeti unaokuja tuhakikishe kuwa Mamlaka ya Maji Jiji la Mbeya inaunganishwa na Mamlaka ya Maji Mbalizi, lakini vilevile na miji midogo mingine ya Mbeya Vijijini iweze kuunganishwa ili kupata maji ya uhakika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lingine ambalo ni kipaumbele ni suala la ujenzi wa mazingira wezeshi, nafikiri hili ni muhimu sana kwa sababu unapojenga uchumi kusipokuwa na mazingira wezeshi kutakuwa na changamoto nyingi sana ili kufikia malengo yetu. Pendekezo langu hapa ni kwamba tungeangalia ni namna gani wakati tunaendelea na ujenzi wa reli ya standard gauge na ile miradi mingine ya kimkakati vile vile tuboreshe na reli yetu ya TAZARA.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na kuboresha reli ya TAZARA tunaomba vilevile tujenge bandari kavu ambayo itasaidia kwa mizigo inayoenda nchi za nje; Zambia, Malawi, Kongo, na nchi nyingine zinazotuzunguka ambazo tuna ushindani nazo kwa bandari za Beira Msumbiji, Afrika Kusini na Angola.

Tukiboresha hii TAZARA na tukajenga bandari kavu na pia tukajenga reli ambayo itatuunganisha sisi na wenzetu wa Malawi kuanzia pale Mbeya na hii reli vilevile itatusaidia kuboresha huduma za meli mbili ambazo zimeshaundwa na zimeshaanza kufanya kazi kwenye Ziwa letu la Nyasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika ujenzi wa mazingira…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)

Nashukuru sana, naunga mkono hoja.