Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Janet Zebedayo Mbene

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ileje

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. JANET Z. MBENE: Mheshimiwa Mwenyekiti, ninakushukuru kwa kunipa nafasi ya kuchangia suala hili ambalo liko mbele yetu la mwongozo wa maandalizi ya mpango wa bajeti kwa mwaka 2018/2019.

Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kwanza kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa fursa hizi, nataka kushukuru sana na kuipongeza Serikali kwa jinsi ambavyo wamekuwa wakiendesha shughuli za kimaendeleo kiasi kwamba Tanzania sasa hivi, imekuwa ikiendelea kwa kasi na kwa kweli hata takwimu tunazopata kutoka IMF na Mashirika mengine ya Kimataifa, Tanzania tunafanya vizuri sana kiuchumi, hata kwa Afrika Mashariki inasemekana sisi tunakuwa mara nyingi zaidi kuliko hata wanavyokua jirani zetu Kenya, ambao kwa muda mrefu wamekuwa wakiongoza katika ukuaji wa uchumi kwa Afrika Mashariki. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naipongeza Serikali kwa juhudi za kufanya yote haya na vilevile kwa kusimamia mfumuko wa bei na kuweka katika hali ambayo ni nzuri na inayowezesha sasa biashara na uwekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nampongeza Mheshimiwa Rais Maguafuli kwa juhudi zake anazofanya katika kuhakikisha kuwa mapato yote yanayotakiwa kupatikana yanapatikana na juhudi hizo zinafanywa pamoja na Wizara ya Fedha. Nimpongeze Mheshimiwa Waziri wa Fedha, Naibu wake, Katibu Mkuu na watendaji wake kwa jinsi ambavyo wamepanga mpango huu kwa njia ambayo kwa kweli inatoa matumaini na mwelekeo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi niiombe Serikali kuwa kwa jinsi ambavyo tumepanga mipango yetu na jinsi ambavyo tumeweka vipaumbele vyetu, basi tuhakikishe kuwa tunasimamia vipaumbele hivi na tunasimamia utekelezaji wa miradi ambayo tumejiwekea ya kipaumbele ili Taifa letu likue. Tumekuwa kwa muda mrefu tukiona miradi ya kielelezo ikiletwa Bungeni na kuoneshwa katika mipango, tunaomba sasa tuoneshwe inaanza kufanyiwa kazi. Miradi ya Mchuchuma na Liganga, miradi ya maeneo maalum ya uwekezaji, miradi ya kupanua bandari kwa sababu tunajua bila bandari kuwa imara na yenye kuwezesha usafirishaji wa mizigo na kupokea mizigo tutakuwa hatuwezi kuendelea na tutashindwa kupata mapato tunayoyategemea.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu imebarikiwa kuwa na madini, vito vya thamani sana, vito hivi namshukuru sana Mheshimiwa Dkt. Magufuli kwa kuanza kuona jinsi gani ambavyo Tanzania na yenyewe sasa inufaike na vito ambavyo viko nchini kwetu kama Almasi, Tanzanite, Dhahabu na madini mengine ambayo ni muhimu sana katika kutuletea uchumi na kutuletea maendeleo ya haraka. Sasa haya yote yafanyike katika utaratibu ambao umewekwa katika mipango hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kupongeza vilevile Serikali kwa suala zima la bomba la mafuta la kutoka Uganda kuja Tanzania, huu nao ni uwekezaji muhimu kwetu lakini yote tunataka kusema tuhakikishe kuwa tunazingatia masuala yanayohitajika kifedha au kitaalam yafanyike kwa wakati. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tuna miradi ambayo ingekuwa imeshaanza sasa hivi tungekuwa tuko mbali. Tunasisitiza sana kilimo, kilimo ndiyo uti wa mgongo na kweli ni kilimo ndiyo kitakachotuwezesha kufikia maendeleo tunayoyahitaji kwa sababu kinaajiri watu wengi, kilimo kinasaidia vijijini, kinasaidia nchi nzima kwa chakula, lakini vilevile kwenye viwanda vyetu hatuwezi kwenda bila kilimo.

Kwa hiyo, tunataka kusisitiza suala la kilimo lipewe kipaumbele kama vile ambavyo miundombinu na miradi mingine inapewa kipaumbele, umwagiliaji kwa kutumia maji, tuhakikishe kuwa yale mambo yote muhimu ambayo yanawagusa wananchi moja kwa moja yanafanyiwa kazi na yanapewa kipaumbele. Kwa hiyo, kilimo, mbolea, maji, utaalam, mitaji ni vitu ambavyo lazima vishuke kwa wananchi wengi kwa ujumla vijijini ili tuweze kuhakikisha kuwa na wao wanafaidi hili suala zima la maendeleo ya haraka tunayoyapata hapa Tanzania. Maana maendeleo yako huku juu lakini bado hayajashuka chini kwa kuonesha jinsi ambavyo umaskini unapungua lakini watu wanaendelea kuwa na kipato, wanajiajiri na mwisho wa yote ufanisi unakuwa mkubwa kwa nchi nzima. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala zima la utekelezaji wa sera ya viwanda. Tumekuwa tukizungumza sana kwa sasa hivi tunataka kujikita kwenye uchumi wa viwanda lakini tuna maeneo ambayo yalitengwa, ambayo kama yangetumika vizuri tungekuwa na maendeleo ya haraka zaidi ya viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nazungumzia masuala ya maeneo maalum kwa ajili ya uchumi yaani SEZ au Export Processing Zones ambazo zilishatambuliwa na zimeshawekwa nchi nzima, tungehakikisha kuwa tunaanza japo na mbili kila mwaka au moja kila mwaka tuhakikishe kuwa sasa tunaeneza viwanda nchi nzima ili kuwe na uwiano wa maendeleo katika Taifa zima.

Kwa hiyo, ningependa sasa kusisitiza kuwa hilo suala la viwanda tuanze kwa kutumia yale maeneo ambayo tulikuwa tumeshayaweka na kwa kiasi kikubwa sana tutumie sekta binafsi.

Mheshimiwa wenyekiti, tumekuwa tuna tatizo la Deni la Taifa limekuwa likiongezeka sana kwa kipindi cha miaka miwili, mitatu. Linaongezeka kwasababu tunataka kufanya kila kitu sisi wenyewe. Hebu tuangalie uwezekano wa kushirikisha sekta binafsi. Wao wachukue ile miradi ambayo ni mikubwa inayohitaji hela nyingi, vilevile ambayo inataka ufanisi mkubwa kuiendesha basi tuingie ubia na sekta binafsi au tuwaachie wao waiendeleze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunazungumzia mashirika ambayo hayafanyi kazi vizuri na yanakuwa mzigo kwa Taifa, hebu tuangalie sasa uwezekano wa kuziachia sekta binafsi wayaendeshe yale mashirika ambayo hayafanyi kazi vizuri ili Serikali isiwe na mzigo wa kuendelea kuyalisha na kuyahudumia wakati yenyewe hayarudishi kitu chochote kwa Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile nizungumzie suala zima la Tanzania sasa hivi tunajulikana kuwa tumepiga hatua kubwa sana na pengine tunaongoza kwenye financial inclusion (matumizi ya mitandao kwa ajili ya miamala ya fedha). Hebu tutumie fursa hiyo sasa kuhakikisha kuwa hiyo teknolojia hiyo inatumika katika kuwasaidia wakulima, wanawake, vijana vijijini kwetu ili na wao sasa waanze kunufaika. Kwa mfano, kupata mitaji, kupata taarifa pamoja na masuala mazima ya miundombinu muhimu ya umeme itakayowekwa katika maeneo yetu ya vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hili suala la sekta binafsi kwa kweli naliona kama ni suala ambalo lingetukomboa sana, sijui kwa nini bado Serikali yetu haijapenda sana kutumia PPP katika kuendesha shughuli zake. Jamani tuangalie mifano, tujifunze mifano ya wenzetu nchi nyingine. Ukienda Malaysia sasa hivi kila kitu kinafanywa kwa kutumia PPP, hebu tuanze japo kidogo eneo moja tuanze kusema hapa tuachie private
sector waendeshe na tutaona jinsi ambavyo inatupunguzia mzigo wa madeni, kwa sababu inabidi sasa mitaji itoke kwenye private sector.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu suala la kodi napongeza sana masuala ya ukusanyaji wa mapato, lakini bado kuna sehemu kubwa sana ya wananchi ambao wako kwenye sekta isiyo rasmi ambao bado hatuwatambui katika kutozwa kodi. Sasa hivi nimeona katika mpango kuna suala la urasimishaji wa wananchi katika masuala ya ujasiriamali na hivi. Ningependa vilevile kupongeza hilo likafanywe na Halmashauri zetu. TRA sidhani kama wataweza kwa sababu hawawatambui hawa watu, hawajui walipo lakini ikifanywa kwenye Halmashauri zetu wanawajua kabisa vijana gani wanazalisha nini, wako wapi, wafanyabiashara wadogo wako wapi, vikundi gani viko wapi, hiyo itarahisisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kutoa rai Serikali itumie Halmashauri zetu ili kwanza na wao pia wapate mapato lakini vilevile itarahisisha hili zoezi zima la kuwarasimisha watu hawa ambao tunataka kuwaingiza katika mfumo usiokuwa rasmi.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mambo mengine yalikuwa ni haya masuala ya bajeti yetu izingatie yale maeneo ambayo yanawagusa wanawake na vijana. Huko nyuma tuliwahi kuzungumzia masuala ya gender gudgeting, sasa sijui yaliishia wapi. Najua nitajibiwa kuwa unavyozungumzia hivi na wenyewe wamo, lakini hili suala bila kutambua moja kwa moja na kuiwekea mikakati na fedha itakuwa vigumu. Tuangalie maeneo ambayo yanawaathiri sana akina mama na vijana au na watoto. Masuala ya vifo vya akina mama wanapojifungua, masuala ya vifo vya watoto wa mwaka mmoja mpaka miaka mitano, yote ni masuala yanayogusa wanawake sasa kama Serikali ikijielekeza kuweka miundombinu inayofaa kwa hospitali, vituo vya afya kwa ajili ya hawa akina mama tutajikuta watoto wetu na akina mama wanapona. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile ukija kwenye suala la maji, najua Serikali imefanya makubwa sana juu ya maji na bado inaendelea kufanya. Maji ni suala ambalo ni la gender moja kwa moja. Wanaohangaika na maji ni akina mama na watoto wao. Watoto wa shule wanabebeshwa ndoo za maji asubuhi kabla hawajaenda shule hii ni kwasababu hatuna miundombinu mizuri ya maji na maeneo mengine yana maji mengi yanachohitaji ni miundombinu tu. Kwa hiyo, nafikiri Serikali iangalie zaidi suala la gender budgeting siyo kwa sababu ya wanawake per se, lakini kwa sababu ndio kitu sahihi kukifanya na kitaturahisishia maendeleo yetu katika vijiji vyetu.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tukija kwenye suala la elimu vilevile tuangalie hayo, watoto wa kike wengi pamoja na kuwa wanakwenda shule lakini hawamalizi kwa sababu ya miundombinu isiyofaa, ambayo haizingatii mazingira yao. Tunaiomba Serikali ijielekeze katika mabweni ya watoto wa kike, iangalie kuwa shuleni kuna maji ya kutosha, kuna vyoo vya kutosha kwa ajili ya watoto wa kike na huduma nyingine ambazo watoto wa kike wanazihitaji kwa sababu ya maumbile yao.

Kwa hiyo, hivi ni vitu ambavyo huwezi kuviepuka ukasema haya mambo ya wanawake, hapana! Bila kuyazingatia na kuyaweka kwenye bajeti utajikuta bado kila siku yale maeneo ambayo yanahusu wanawake na watoto yako nyuma.(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba niishie hapo kwa rai ambazo nimezitoa kwa Serikali nikiamini watachukua maoni haya na kuyaingiza katika mipango yao ili kila kitu ambacho tumekizungumza hapa kikafanyiwe kazi kama ambavyo mpango ulivyoonesha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ninashukuru sana na naendelea kupongeza Serikali kwa juhudi zote ambazo inazifanya. Ahsante.