Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

Hon. Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Mapendekezo ya Mpango wa Maendeleo wa Taifa unaokusudiwa kutekelezwa na Serikali pamoja na Mwongozo wa Kuandaa Mpango wa Bajeti ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2018/2019

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana kwa kunipa nafasi ili niweze kuchangia mwelekeo huu wa mpango asubuhi hii ya leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kabla sijaanza kuchangia mwelekeo huu wa mpango, naomba Nimshukuru Mwenyezi Mungu Subhanahu-Wataala ambaye ameendelea kunijalia afya njema leo hii, lakini pia niweze kumshukuru Mwenyekiti wa chama changu, Chama cha Wananchi (CUF), full-bright Profesa Ibrahim Haruna Lipumba, kwa kuendelea kushirikiana vizuri kutetea maslahi ya Watanzania na hasa katika rasilimali zetu za madini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niweze kuzungumza kidogo kwamba sisi Chama cha Wananchi (CUF) ilani zetu zote za uchaguzi kuanzia mwaka 1995, mwaka 2000, mpaka mwaka 2010 tulikuwa tunazunguka Tanzania nzima kuwaeleza Watanzania ya kwamba rasilimali za madini ya nchi hii zinatumiwa kwa kiasi kikubwa na wageni wa nje na sisi wenyewe kila shilingi 100 tunapata shilingi tatu tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, leo hii nizungumze katika Bunge lako hili kwa namna ya kipekee kabisa niweze kumpongeza Mheshimiwa Rais wetu huyu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwamba anasimamia Ilani ya Chama cha Wananchi (CUF), anasimamia itikaChama cha Wananchi (CUF), Sera ya Utajirisho kwamba madini yetu yaweze kuwanufaisha Watanzania na sisi lazima tuunge mkono kama chama imara cha siasa, CUF - Chama cha Wananchi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nianze kuchangia mwelekeo huu wa mpango kwa kusema ya kwamba viwanda kwa kiasi kikubwa sana, nilikuwa nasikiliza hotuba zote mbili, hotuba ya Mheshimiwa Waziri na hotuba ya Kamati ambazo zimezungumzia suala zima la viwanda, na tumekuwa tunazungumza sana kwamba sehemu hii ya viwanda ni sehemu muhimu sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilishawahi kusema katika Bunge hili wakati nachangia mpango mwaka wa jana na mwaka wa juzi, kwamba nchi nyingi duniani ziliweza kuendelea kupitia sekta ya viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, karne ya 15, ukisoma historia, sisi tuliosoma historia tunaambiwa ya kwamba nchi zote za Ulaya ziliweza kufanya mapinduzi ya viwanda na hatimaye wakaweza kuwa matajiri mpaka leo hii tunasema wao ndio wanaotusaidia sisi nchi za ulimwengu wa tatu. Kwa hiyo, kwa umuhimu wake hili suala ni suala nyeti sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la ajabu, tulikuwa tumezungumza wakati wa bajeti hapa kwamba wapo wawekezaji wengi wanaohitaji kuwekeza Tanzania. Kule Mtwara kuna wawekezaji wa Kijerumani na Kamati hapa imeeleza ambao wanataka kujenga viwanda vya mbolea, pale Mtwara Msangamkuu. Kule Kilwa pia kuna mwekezaji ameamua kuwekeza kwa kujenga kiwanda cha mbolea, lakini bado Serikali tunaona inasuasua kuwapa rasilimali ya gesi wale wawekezaji ili waweze kujenga vile viwanda.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaamini viwanda vikijengwa pale Mtwara Msangamkuu wananchi wengi wa Mtwara watapata ajira, wananchi wa Kilwa kule kikiwepo kiwanda watapata ajira na umaskini utaweza kuondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sana katika mwelekeo huu wa mpango kwamba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha hotuba yake atueleze kwa nini mpaka leo wale wawekezaji wanaotaka kuwekeza viwanda vya mbolea pale Msangamkuu, Mtwara Vijijini ambapo ni karibu kabisa yaani ni pua na mdomo katika Jimbo langu la Mtwara Mjini, lakini pia kule Kilwa bado mpaka leo Serikali inasuasua kuwapa wale wawekezaji gesi waweze kujenga viwanda vya mbolea ili kuweza kuondokana na umaskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kuzungumzia suala la umeme REA. Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Dkt. Mpango, amezungumza hapa kwa kiasi kikubwa kwamba umeme unaotumika mikoa ya kusini unatoka Mtwara Mjini, viwanda vya kusindika ile mitambo vimejengwa Mtwara Mjini, lakini jambo la ajabu nimekuwa ninazungumza sana, kwenye Mabunge yako yote nimekuwa nazungumza hili; kwamba pale Mtwara Mjini kwenyewe ambapo ndipo mitambo yote ya kusindika umeme ipo, bado kuna maeneo mengi haujapelekwa mtandao wa umeme ikiwemo kule Mbawala Chini, Naulongo, Mkunjanguo na maeneo mengine ambamo pia tulisema kwamba mule mnapita kitu kinachoitwa mkuza wa gesi, lile bomba la gesi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo tumelia sana kwa muda mrefu katika Bunge hili na Mheshimiwa Waziri akiwa anaahidi kwamba atapeleka umeme kule kote. Sasa ni jambo la ajabu sana kwamba kila mwaka tuwe tunarudia na kurudia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo ninaomba katika Mpango huu ambao unaandaliwa, hili suala la kuhakikisha ya kwamba umeme wa REA unasambazwa basi usambazwe kwenye maeneo yote kwa sababu wananchi wa maeneo yale ambapo ni vijiji ambavyo viko mjini lakini bado tunaita ni vijiji kwa sababu vinahitaji kupita umeme wa REA uweze kwenda kule; Tunaomba Serikali ihakikishe ya kwamba inapeleka na sio kila mwaka kupiga dana dana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vipo vijiji vingi pia kule Mtwara na Lindi, bado, na wakandarasi wenyewe waliopewa ukiwauliza wanatuambiwa huko sisi hatuna bajeti, bajeti yetu sisi ni kutoka kijiji hiki tunaingia vijiji vya Tandahimba, Newala na wapi, lakini bado tunahitaji wananchi wale waweze kupelekewa umeme. Ili tuweze kuondokana na umaskini lazima kila kijiji, hata kama kipo mjini, basi umeme uweze kufika. Tunaomba sana hili Mheshimiwa Waziri aje atueleze mpango huu wa maendeleo ameliwekaje mwaka huu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ninataka nilizungumze hapa ni suala la kilimo. Katika Mkutano wa Bunge wa bajeti, wakati tunapitisha Bajeti ya Wizara ya Kilimo nilizungumzia suala zima la korosho. Kulikuwa na suala la mboleo, nilieleza wakati ule na nilimnukuu mtaalam mmoja anaitwa Kunz, mwaka 1988/1989 katika kitabu chake cha Managerial, alisema kwamba failure to plan is planning to fail, kwamba ukifeli kupanga maana yake unapanga kufeli. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilizungumza suala la mbolea, kwamba walisema kwamba watagawa mbolea bure kwa wakulima wetu wa korosho lakini halikupangwa lile; na hapa leo kwenye mwelekeo huu wa Mpango bado sijaona pia kama limepangwa. Kilichotokea wakulima wamelanguliwa mbolea badala ya kuuziwa shilingi 20,000 wakanunua mbolea mfuko mmoja shilingi 100,000, 150,000 wengine mpaka shilingi 200,000 baadhi ya maeneo, ni kwa sababu Serikali ilishindwa kupanga sawasawa suala hili la kugawa mbolea bure kwa wakulima wa korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na korosho ndilo zao ambalo linaingiza pesa nyingi Serikalini kuliko zao lolote. Linaanza zao la korosho then inakuja tumbaku. Kwa hiyo, ninaomba kwamba mpango wetu wa safari hii upange sawa sawa, kwamba ni kiasi gani cha mbolea kitapelekwa kwa wakulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini jambo la ajabu katika korosho pia, nilikuwa napitia taarifa za masoko ya dunia; bei ya korosho soko la dunia, kilo moja ni dola 29. Ukijumuisha, ukigawa kwa pesa yetu ya Kitanzania ni sawa sawa na almost kama shilingi 49,000; shilingi 50,000 hivi kwa kilo moja, katika soko la dunia. Kama Bandari ya Mtwara itatumika sawa sawa, ukisafirisha korosho kutoka Bandari ya Mtwara mpaka soko la dunia, bei ya korosho haizidi kilo moja shilingi 2,000. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo, ninaomba sana, pamoja na kwamba tunajigamba, na tunashukuru kwa kweli kwamba Serikali imejitahidi kuongeza bei ya korosho kwa wakulima, hivi sasa ni shilingi 3,800 mpaka 3,850, lakini bado mkulima angeweza kupata bei kubwa zaidi ya hii kutokana na umuhimu na unyeti wa zao la korosho duniani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba sana Serikali ihakikishe inatafuta wanunuzi wa korosho ili korosho yetu hii iweze kuingiza pesa nyingi zaidi ya hizi ambazo tunazipata Hazina, lakini kwa wananchi wetu waweze kuondokana na umasikini, hasa maeneo ya Mtwara na Lindi pamoja na Pwani na maeneo mengine wanayolima korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la ajabu sana nilikuwa napitia taarifa pia za kimtandao kwamba hata katika zile nchi ambazo zinalima korosho duniani, Tanzania haipo. Afrika kuna Côte d’Ivoire, imewekwa Afrika Kusini, imewekwa Thailand na nchi nyingine, Tanzania sisi tunajulikana kwamba hatulimi korosho wakati wanunuzi waliopo Thailand, wanunuzi waliopo India wanakuja kununua korosho Tanzania. Hili linapoteza pia thamani na pato zaidi. Kwa sababu hawa wanunuzi wa kule nchi za nje wanakwenda kununua kule kwenye nchi ambazo zimewekwa kwenye taarifa mbalimbali za kidunia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaomba hili mlizingatie, ni jambo la muhimu sana ambalo ninaomba kuchangia katika huu Mpango ni sekta ya utalii nchini. Ninaomba kuzungumzia suala zima la sekta ya utalii nchini…

T A A R I F A

MHE. MAFTAHA A. NACHUMA: Mheshimiwa Mwenyekiti, siipokei taarifa kwa sababu kadandia gari kwa mbele. Nilichozungumza ni kwamba katika orodha ya nchi zinazouza korosho duniani Tanzania haipo, ndiyo taarifa iliyopo pale. Sasa yeye anazungumza yawezekana kwamba hajasoma sawasawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niendelee kwa sababu kanipotezea muda bure tu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ninaomba kuchangia katika huu mwelekeo wa mpango ni sekta ya utalii nchini. Sekta hii ya utalii nchini ni sekta muhimu sana na taarifa ambayo tulipewa hapa Bungeni, tulielezwa ya kwamba Tanzania ina vivutio vingi sana, ukiondoa Brazili inayofuata ni Tanzania. Hata hivyo nikapitia mpango wa Wizara ya Maliasili na Utalii, kuna pesa ambazo wameziweka zinaitwa pesa za REGROW, wamekopa Benki ya Dunia kwa ajili ya kuendeleza sekta ya utalii kule Nyanda za Juu Kusini. Sasa ninaomba sana zile pesa dola milioni moja ambazo zimekopwa Benki ya Dunia kwa ajili ya kuendeleza utalii Nyanda za Juu Kusini basi zifike kule Kusini pia ili sekta hii ya utalii iweze kutangazwa sawasawa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, na katika hili, pale Mtwara Mjini tuna eneo la Mikindani. Mikindani kuna majengo ya kale sana. Sasa nimeangalia taarifa hapa sijaona mpango uliowekwa sawasawa juu ya sekta ya mambokale katika utalii kwamba Serikali imejipangaje kutangaza mambokale ili iweze kuwaingizia pesa Serikali ya Tanzania, lakini wananchi kwa ujumla kwa kupata ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mikindani kuna majengo na vivutio vingine vingi vya kale, lakini vivutio vile vimeachwa kwa wazungu, watu wanaoitwa Trade Aid ndio wanaokarabati, ndio wanaotangaza na kukusanya pesa wakati Serikali hii ina shida ya pesa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nilikuwa naomba sana kwamba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kuhitimisha mpango sekta hii ya utalii iangalie sekta ya mambo kale na hasa hasa utalii katika maeneo haya ya Mikoa ya Kusini ya Mtwara na Lindi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ambalo ninataka kulizungumza ni suala hili la miundombinu. Tunaishukuru Serikali kwa kiasi kikubwa imekuwa ikijenga miundombinu, imekuwa ikijenga barabara lakini pia imeweza kuleta pesa za kutosha pale Mtwara Mjini na linajengwa gati linajengwa la mita 300.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niombe sana, sambamba na upanuzi wa Bandari uliopo Mtwara Mjini hivi sasa tunaomba swala la reli hili ambalo imekuwa Serikali imekuwa ikizungumza kila mwaka, kila siku, reli ya Kusini, ili Mtwara corridor iweze kufunguka, iweze kufungua uchumi wa ukanda ule wa Kusini lazima hili suala la kujenga reli kutoka bandari ya Mtwara kwenda Mchuchuma na Liganga kule kwenye makaa ya mawe iweze kuwekwa kwenye bajeti ya mwaka huu, pesa ziweze kutengwa ili sasa uchumi wa Kusini na Watanzania uweze kusheheni. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, reli hii ilikuwepo miaka ya nyuma lakini iliondolewa, sijui iliondolewa kwa sababu gani. Sasa tunaomba sana, kwa sababu kuna mkakati unaitwa Mtwara corridor wa kufungua Kusini mwa Tanzania ili Tanzania yetu sasa iweze kweli kuwa ni Tanzania ya uchumi. Bandari yetu inavyojengwa kama reli ikijengwa mizigo ikiletwa pale tunaamini ya kwamba bandari itaingiza pesa nyingi na bajeti yetu itakuwa haisuisui tena kwa sababu ya makusanyo. Tusiangalie sana Bandari ya Dar es Salaam, tutanue Kusini, tutanue Mtwara corridor kama tulivyokuwa tunaahaidi siku zote. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho, naomba nizungumze suala zima la ardhi. Wakati tunapitia bajeti hapa, Mheshimiwa Waziri wa Ardhi alizungumzia mipango mikakati, na tunashukuru kwa kweli pale Mtwara Mjini tumezindua mpango kabambe wa ardhi. Hata hivyo kuna mambo ambayo yalizungumzwa na kuahaidiwa katika Bunge lako hili Tukufu, suala la kulipa fidia kwa maeneo ambayo Serikali ilichukua. Kwa mfano, Mtwara Mjini eneo la Mji Mwema, Serikali ilihaidi kwamba mpaka mwezi wa nane mwaka huu itakuwa tayari imelipa fidia. Jambo la ajabu wanaleta taarifa kwamba Serikali imeshindwa kuwalipa wale watu wa Mji Mwema wakati wale watu wamechukuliwa ardhi tangu mwaka 2013, ni jambo la ajabu sana. Tunazungumza ndani ya Bunge, tunapanga ndani ya Bunge wananchi wanasikia halafu baadaye Serikali inasema haina pesa kupitia UTT, UTT wameghairi kulipa. Ni jambo la ajabu kwa kuwa tunazungumza, tunapitisha kwenye bajeti lakini utekelezaji wa haya mambo ya msingi unakuwa hakuna.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo nilikuwa naomba Mheshimiwa Waziri atakavyokuja atueleze kwamba mkakati upoje kuhusiana na sekta hii ya ardhi ambayo bado ina changamoto nyingi; Tanzania pamoja na jitihada kubwa zinazofanywa na Waziri wa Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nikushukuru sana kwa kunipa nafasi ahsante sana.