Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Joseph Michael Mkundi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Ukerewe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. JOSEPH M. MKUNDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Mabaraza ya Ardhi; migogoro mingi ya ardhi inachangiwa sana na muundo wa Mabaraza haya ya Kata hasa kutokana na kutawaliwa sana na rushwa. Hii inasababishwa na kukosekana kwa mafunzo ya mara kwa mara na hivyo wajumbe kukosa weledi katika kutafsiri sheria hata kufikia maamuzi jambo ambalo linaishia kugombanisha jamii. Pia wajumbe wa mabaraza haya hata Makatibu wa Mabaraza kutokuwa na pato lolote kunapelekea vitendo vya rushwa. Hivyo nashauri yafuatayo:-

(a) Kutolewe mafunzo ya mara kwa mara kwa mabaraza haya (semina) ili kuwaongozea uelewa na uzoefu Wajumbe wa Mabaraza ya Kata. Jambo hili litawawezesha kukabili kesi zinazojitokeza kwenye maeneo yao.

(b) Kutolewe ruzuku kwa ajili ya kuendesha mabaraza ya ardhi ya Kata, kukosekana kwa ruzuku kunasababisha mazingira magumu sana ya uendeshaji na hivyo kujenga mazingira ya rushwa.

(c) Halmashauri zipewe nguvu/mamlaka ya kuyavunja mabaraza haya pale inapothibitika kuwa yamekiuka maadili. Kwa hali ilivyo hivi sasa, kuna urasimu mkubwa katika kuchukua hatua kwa Mabaraza ya Ardhi. Jambo hili limepelekea matatizo yetu na bado wajumbe hawa wanakuwa na jeuri kwa kuamini kuwa si rahisi kuchukuliwa hatua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Baraza la ardhi Wilaya, katika ngazi ya Wilaya Mabaraza yetu yanakosa wataalam. Mfano, katika Halmashauri ya Wilaya ya Ukerewe, kuna mrundikano mkubwa wa kesi kutokana na kukosa Mwenyekiti wa Baraza. Mara kwa mara Wilaya imekuwa inapata huduma ya Mwenyekiti ambaye haishi pale na matokeo yake anahudumia mara moja kwa mwezi na kwa muda usiozidi masaa sita. Hili limepelekea kuwepo kwa kesi za mipaka miaka miwili zisizofanyiwa maamuzi. Ombi, Baraza la Ardhi la Wilaya ya Ukerewe lipangiwe Mwenyekiti wa Baraza ambaye atakuwepo muda wote ili kupunguza migogoro ya ardhi hasa ikizingatiwa kuwa eneo katika Wilaya hii ni dogo na hivyo kuwa na migogoro mingi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu vifaa vya upimaji; kuwe na utaratibu mzuri wa kupatikana kwa vifaa vya kupima ardhi ili mipango mizuri ya matumizi ya ardhi iwezekane.