Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

Hon. Jitu Vrajlal Soni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Babati Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki

MHE. JITU V. SONI: Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nichukue furasa hii kwanza kabisa kumshukuru Mwenyezi Mungu kwa afya na uzima. Nichukue fursa hii pia kumpongeza Waziri, Naibu Waziri pamoja na Katibu Mkuu akiongoza wataalam wa Wizara kwa kazi nzuri sana wanayofanya kusimamia sera na wajibu wao.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nishauri kama ifuatavyo:-

(i) Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki iangalie namna ya kuboresha mfumo wa utoaji wa taarifa na hasa fursa za uwekezaji ndani ya nchi yetu lakini pia fursa za Watanzania kuwekeza katika nchi za Afrika Mashariki na nchi zingine.

Leo hii Watanzania wakihitaji msaada wa kupata taarifa mbalimbali za fursa hizo za kibiashara nje za Afrika Mashariki au zingine ni ngumu kupata. Wizara iboreshe Kitengo cha Uchumi Wizarani na kuwezesha Balozi zetu zote katika Kitengo cha Uchumi ili waweze kutusaidia kufanya biashara kirahisi na kujua utaratibu wa sheria na kanuni. Nipongeze Kitengo cha Protocal kwa msaada mkubwa wanaotupa sisi Watanzania tukisafiri.

(ii) Wizara ihamasishe Watanzania kutumia fursa mbalimbali zilizopo kibiashara.

(iii) Wizara ya Mambo ya Nje ishirikiane kwa karibu na Wizara ya Elimu kuboresha mitaala ya elimu na kusaidia kupata vifaa na nyenzo za kufundishia masomo ya mahusiano ya kimataifa katika vyuo vyetu. Hali ni mbaya sana na wanaohitimu hawana viwango vya kufanya kazi waliosomea.

(iv) Wizara iangalie namna ya kuwatambua diasporas wetu hasa kwa wale waliokuwa Watanzania na sasa wamechukua uraia wa nchi nyingine (Persons of Tanzanian Origin) kwani wengi wao wamechukua uraia wa nchi nyingine kutokana na mazingira yao ya kupata huduma za kijamii kama afya, elimu, ajira na fursa zingine ambazo wasingezipata bila uraia wa huko. Nchi yetu haina utaratibu wa kisheria wa kuwa na uraia wa nchi mbili hivyo Watanzania hao walilazimika kuchukua uraia wa huko.

Pia Wizara ingeangalia utaratibu wa kisheria wapate kitambulisho kitakachowapa fursa ya kuwa watu wenye asili ya Kitanzania na waweze kuishi nchini na kuwekeza hapa kama Watanzania wengine ila wakose fursa ya kupata ajira ya Serikali, kuwa afisa au shughuli yoyote katika masuala ya ulinzi na usalama, kuchagua au kuchaguliwa (kupiga kura au kupigiwa kura).

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii itafanya hao waliokuwa Watanzania kuwa na fursa ya kuwekeza nyumbani (Tanzania) kwa urahisi sana. Nchi nyingi zimefanya hivyo na kuongeza mapato ya nchi kwa kuwapa haki hao waliokuwa Watanzania. Leo hii hawaruhusiwi kumiliki ardhi na wakitaka kuwekeza wanatakiwa kufuata utaratibu sawa na mtu asiye raia (non Tanzanian).

(v) Wizara hii iangalie namna ya kuwapatia Wabunge mafunzo mbalimbali hasa kuhusu itifaki kama walivyokuwa wanafanya miaka ya nyuma. Mafunzo haya yatolewe kwa Wabunge wote wa Jamhuri ya Muungano, Baraza la Wawakilishi na Wabunge wa EALA.

(vi) Kwa Wabunge wa EALA, muda huu ambapo bado hawajaanza kazi rasmi, wangepewa mafunzo maalum ya kuijua Afrika Mashariki, mikataba mbalimbali, nchi yetu inatarajia wafanye nini katika uwakilishi wao huko EALA pamoja na mambo mengine ambayo Wizara inaona ni muhimu wapate elimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru na kupongeza Wizara na timu nzima ya wataalam pamoja na Balozi wetu wote.