Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. Joseph Roman Selasini

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Rombo

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. JOSEPH R. SELASINI: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kunipa dakika tano na mimi niseme machache kuhusu Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kutumia muda wangu vizuri, niseme tu kwamba naunga mkono kwa asilimia mia moja hotuba ya Kambi, hotuba ya Mheshimiwa Lema na hotuba ya Mheshimiwa Peter Serukamba. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, niseme jambo ambalo kwa kweli ningelizungumza kwenye briefing wakati tukitengeneza ratiba ya Mkutano huu wa Bajeti. Bajeti ni kuhusu mapato na matumizi, kwa muda wa siku 90, Wabunge tunakaa hapa kupanga matumizi lakini tukimaliza hizo siku 90 tunapewa siku moja au mbili kuzungumza habari ya mapato. Kwa jinsi hii sioni ni namna gani sisi Wabunge tunaishauri Serikali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, uzoefu wa Mabunge mengine ukienda Bunge la Kenya hapa, juzi Kamati ya Bajeti ilikuwa Finland, ukienda Bunge la Uingereza muda wa kujadili vyanzo vya mapato katika nchi ni mkubwa sana Bungeni kuliko muda wa kujadili matumizi. Sasa sisi tunajadili matumizi ambayo hatujui tutayapata wapi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, Mama Makinda alianza vizuri na Bunge la Tano, aliunda Kamati ile tuliita Chenge One ilitoa mawazo, ilitoa mapendekezo namna ya kuongeza vyanzo vipya vya mapato lakini sisi kila mmoja wetu analalamika, kila mmoja wetu anataka mradi lakini ukweli ambao tunauona sasa hivi Mheshimiwa Mpango tunamwonea pesa zipo wapi? Kwa hiyo, lazima tuamue, Bunge litengeneze ratiba inayofaa tupate muda wa kutosha kuweza kuishauri Serikali kuhusu vyanzo vya mapato, hilo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la pili ambalo napenda kulisema ni kuhusu vyanzo ambavyo tayari tunavyo. Bunge lililopita tulifanya uamuzi wa makusudi kunyang’anya property tax kwenye Halmashauri na kuwapa TRA. Kwa mfano Jiji la Dar es Salaam walikuwa wameweka maoteo ya Sh.33,100,000,000/=, lakini katika uhalisia wamekusanya shilingi bilioni 6.5 tu ina maana shilingi bilioni 26.59 hazikukusanywa na TRA, jambo ambalo Halmashauri na Majiji wangeachiwa kukusanya zile fedha pengine zingepatikana fedha za kutosha kwa ajili ya miradi ya maendeleo ambayo Hazina imeendelea kutoa pesa kwa ajili ya Jiji. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana tuufikirie huu uamuzi wa kuchukua chanzo hiki cha mapato kutoka Majiji na Halmashauri na kukipeleka TRA, tuwarudishie Majiji na Halmashauri ili fedha ambazo zingeenda kwenye miradi ya maendeleo kwenye Majiji na Halmashauri kutoka Hazina zisiende na pengine haya majiji yanaweza kusaidia Hazina katika mambo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la mwisho ambalo napenda kuchangia ni kuhusu Tume ya Mipango. Ni ushauri wa Kamati ya Bajeti, ni ushauri wa wengi hapa, Tume ya Mipango irudi Ofisi ya Rais au iundiwe Wizara. Sababu ni kwamba Tume ya Mipango imeenda imejificha pale Hazina hakuna anayeitambua sasa Waziri na Naibu Waziri na wengine wako busy kwa ajili ya kutafuta fedha kwa ajili ya mipango mingine kwa ajili ya kuhakikisha bajeti inaenda vizuri lakini Tume ya Mipango imesahauliwa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, habari za kwenye corridor Mheshimiwa Waziri ni kwamba Katibu Mkuu wa Hazina amekuwa so powerful kiasi kwamba hakuna mtu anayemsikiliza, kwa hiyo Tume imebaki inaeleaelea tu pale. Tume kama chombo cha kutunga sera za uchumi, kusimamia sera za uchumi, kusimamia hii miradi ya maendeleo kimebaki kinaelea pale.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ni ombi langu kwa Mheshimiwa Rais aone uwezekano wa kuitoa Tume ya Mipango Hazina, aiundie Wizara au airudishe kwenye Ofisi yake kama ilivyokuwa zamani ili Tume iwe huru katika kupanga sera za uchumi za nchi na kuzisimamia vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema haya, nakushukuru sana.