Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango

Hon. George Malima Lubeleje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpwapwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Fedha na Mipango

MHE. GEORGE M. LUBELEJE: Mheshimiwa Mwenyeiti, nami nikushukuru kwa kunipa nafasi ili nichangie hoja ya Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mipango.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Mheshimiwa Naibu Waziri, Katibu Mkuu, pamoja na Watendaji wote wa Wizara hii kwa kazi nzuri wanazofanya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze na suala la miradi ya maendeleo. Katika bajeti ya mwaka jana, hii ambayo sasa tunamalizia mwaka wa Serikali tarehe 30 mwezi Juni, Serikali imetuahidi kwamba asilimia 40 ya bajeti yake itakwenda kwenye maendeleo. Mpaka leo hii fedha ambazo zinapelekwa kwenye Halmashauri ni kidogo sana, hazitoshi kabisa na kuna miradi ambayo haijatekelezwa, viporo ni vingi mno.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano, mwaka jana Bunge tumeidhinisha fedha za miradi ya maendeleo, shilingi bilioni 791.99 lakini hadi Machi mwaka huu fedha ambayo imetumika ni shilingi bilioni 18 na miradi ni mingi katika nchi hii na katika Halmashauri zetu. Nimuulize Mheshimiwa Waziri wa fedha, hii asilimia ya fedha iliyobaki ambapo miradi haijakamilika, mtaleta lini fedha zote ili tukamilishe miradi hiyo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano Jimbo langu la Mpwapwa kuna miradi mingi ya maji ambayo haijakamilika. Kuna visima vitatu sasa ni mwaka mmoja tangu vimechimbwa, hakuna cha pump, hakuna cha bomba ambalo limewekwa. Kuna vituo vya afya viwili ambavyo vimeanza kujengwa zaidi ya miaka 10 havijakamilika ni kwa sababu ya ufinyu wa bajeti. Kwa hiyo, naishauri Serikali, TRA wanakusanya vizuri sana mapato, niwapongeze sana TRA lakini pamoja na mapato, tudhibiti fedha za Serikali ili fedha zote ziende kwenye miradi ya maendeleo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la pili ni kuhusu TRA kukusanya kodi ya majengo ya Halmashauri za Wilaya, Manispaa na Majiji. Nataka kupata maelezo, hii kodi ya majengo walikuwa wanakusanya Halmashauri wenyewe kuna sababu gani za msingi ikahamishiwa TRA? TRA watakwenda mpaka kwenye grass root, mpaka chini nyumba za mbali kwenye vijiji huko kukusanya? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama wamekusanya kwa sababu Mamlaka ya Serikali za Mitaa ilikuwa imetenga kama Halmashauri thelathini ndiyo TRA ikusanye, tupate maelezo, TRA wamekusanya kiasi gani na hizo Halmashauri zimeshapelekewa fedha kiasi gani kwa sababu Halmashauri hizi zina miradi ya maendeleo. Kwa hiyo, nataka nipate maelezo kwa nini suala hili limekwenda TRA. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni kuhusu vyanzo vya mapato vya Halmashauri za Wilaya. Halmashauri za Wilaya zina hali mbaya sana, hasa mapato ya ndani kwa sababu vyanzo vingi vimechukuliwa na Serikali Kuu na fedha toka Serikali Kuu zinazopelekwa kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa ni kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Waziri wa Fedha awarudishie baadhi ya vyanzo vya mapato Mamlaka ya Serikali za Mitaa, Halmashauri za Wilaya, Miji, Manispaa na Majiji ili wakusanye wenyewe kwa sababu hali ni mbaya. Wanashindwa kuendesha Halmashauri zao kwa sababu vyanzo vingi vimepelekwa kwenye Halmashauri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini kuna madeni ya ndani, wenzangu wamezungumzia pamoja na kulipa deni la nje ambalo ni lazima tulipe kwa sababu bila kulipa huwezi kupata mkopo tena lakini haya madeni ya ndani kwa mfano wakandarasi kama wasipolipwa barabara haziendelei kutengenezwa na madeni ya ndani ni pamoja na hao wazabuni wanaohudumia kwa mfano shule. Wilayani kwangu kuna wazabuni watatu wanahudumia chakula katika shule za sekondari, Mpwapwa High School, Shule ya Maza Girls’ na Shule za Berege, wanadai zaidi ya shilingi milioni 300 hawajalipwa mpaka leo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, siyo Halmashauri ya Mpwapwa tu ni maeneo mengi katika nchi hii, wazabuni hawalipwi sasa kama hawalipwi watahudumia shule hizi na wanafunzi wanatakiwa kupata chakula? Hivi leo wazabuni wanaohudumia vyakula katika shule wakigoma si shule zitafungwa? Kwa hiyo, naomba Mheshimiwa Waziri wa Fedha walipe wazabuni hawa ili waendelee kuhudumia hizi shule zetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo lingine ni wastaafu, wanalalamika pamoja na kuwa wanawalipa kila mwezi, lakini fedha ni kidogo waongeze fedha, wawe wanapata angalau fedha za kutosha badala ya hii Sh.100,000/= sijui Sh.200,000/=. Nataka niwaambie hapa wengi tumeshastaafu na tunakwenda kwenye uzee na sisi wengine tumefika kwenye uzee, mtu unatoka kwa mfano Rudi, Malolo unafuata Sh.100,000/= wakati nauli tu peke yake ya kwenda na kurudi ni Sh.30,000/= unapata nini hapo? Kwa hiyo, nashauri hiki kipato cha wastaafu kiongezwe ili waweze kupata fedha za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru sana kwa kunipa nafasi hii ila ninachoomba tu ni kwamba Serikali ijitahidi kupeleka fedha za miradi ya maendeleo katika Halmashauri otherwise miradi mingi itakwama. Sisi ni Wabunge wa kuchaguliwa na tumeahidi katika Ilani ya Uchaguzi kutekeleza miradi mbalimbali, tusipotekeleza mwaka 2020 wananchi hawaturudishi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana na naunga mkono hoja.