Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Selemani Moshi Kakoso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mpanda Vijijini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. MOSHI S. KAKOSO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kunipa nafasi ya kuchangia bajeti hii. Awali ya yote niipongeze Serikali kwa kazi nzuri sana ya kuleta bajeti hii ili iweze kuwa ya mfano na kusaidia wananchi kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naipongeza Serikali kwa sababu imekuja na mpango mzuri. Niwapongeze Kamati ya Bajeti kwa kuja na mapendekezo mazuri ya kuishauri Serikali.

Mheshimiwa Spika, eneo ambalo nataka kuzungumzia ni suala zima la Serikali kuja na mpango wa kujenga au kuanza uchimbaji makaa ya mawe na chuma Mkoani Njombe. Eneo hili litakuza uchumi mkubwa sana kwa Serikali ya nchi yetu na itafanya maeneo haya ya ukanda wa kusini na Serikali kwa ujumla kuwa na kipato kizuri.

Mheshimiwa Spika, eneo lingine ambalo tunaishauri Serikali iwekeze kwa nguvu zote ni ujenzi wa reli ya kati. Ujenzi wa reli ya kati ni suluhisho kwa wananchi wa maeneo karibu yote ya nchi hii. Asilimia kubwa wananchi wa kada ya chini

wanatumia sana usafiri wa reli. Kwenye maendeleo, tukiboresha eneo la ujenzi wa reli ya kati tutakuwa tumesaidia sana wananchi wa maeneo ya nchi hii. Siyo tu kwa maeneo ya Dar es Salaam, lakini tutakuwa tumetengeneza uchumi wa Mikoa mingi kuanzia Dar es Salaam mpaka Mkoa wa Kigoma.

Mheshimiwa Spika, sambamba na tawi la reli la kutoka Tabora kwenda Mwanza, naamini uchumi kwenye maeneo hayo na maisha bora kwa kila Mtanzania yanaweza kupatikana kwa kiwango kikubwa sana. Niiombe sasa Serikali kwenye bajeti hii iwekeze nguvu kubwa sana kwa ajili ya kuimarisha ujenzi wa reli ya kati. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, bado kuna maboresho ambayo yamefanyika, maboresho ya Shirika la Ndege, ujenzi wa mitambo ya gesi, ni maendeleo ambayo yanategemewa sasa kwa Serikali yanaweza yakatoa suluhisho kubwa na kupata mapato makubwa ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, eneo ambalo ningependa kushauri Serikali ni kuachana na uwakala wa kukusanya kodi ya nchi ya Congo. Eneo hili tunapoteza mapato makubwa sana. Ni vema Serikali ikaangalia ule mkataba ambao tumewekeana na Congo, hauna manufaa kwetu sisi. Karibu wafanyabiashara wengi wa nchi ya DRC wamehama kutumia Bandari ya Dar es Salaam, kwa hiyo ni vizuri kwenye maeneo haya wakatazama upya ili kuweza kuongeza mapato ya Serikali.

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo, nina ushauri kwa Serikali. Ni vizuri sasa Serikali ikaangalia upya, nchi ya Zambia ni miongoni mwa nchi inayotegemea sana Bandari ya Dar es Salaam lakini bahati mbaya Zambia wanalipa ada tofauti na nchi zingine. Ni Vizuri Waziri wa Fedha akakaa na wenzetu wa Zambia wakaangalia zile tofauti ambazo zipo wakazitoa ili wenzetu waweze kutumia Bandari ya Dar es Salaam.

Mheshimiwa Spika, sehemu nyingine ambayo ningependa kuzungumzia sana ni kwenye sekta ya kilimo, kwenye sekta ya kilimo, ni eneo pekee ambalo tukiwaboreshea wakulima wa nchi hii watakuwa na nafasi ya kutoa mchango mkubwa sana wa pato la Taifa. Tunaomba sana Serikali iangalie kuweka mazingira mazuri yatakayowasaidia wananchi kupata pembejeo zenye bei nafuu. (Makofi(

Mheshimiwa Spika, tunapowawezesha wakulima, tumewawezesha wananchi karibu wote wa nchi yetu. Ni vema sasa Serikali ikaja na mkakati wa kusaidia hawa wakulima wadogo, wavuvi na wafugaji ili iweze kuwawekea mazingira ambayo yatakuwa rafiki kwenye uzalishaji kwa gharama nafuu na kuwawekea miundombinu ambayo itawasaidia sana katika kuboresha shughuli za kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sambamba na hilo ili nchi iweze kwenda vizuri Serikali sasa iangalie uwezekano wa kuweza kusaidia wakulima wakubwa. Ni vema tukaangalia hata Taasisi za Serikali tulizonazo, tukawekeza kwenye Jeshi la Magereza, Jeshi la JKT, tukawawezesha waweze kuzalisha kilimo kikubwa, wakalima mashamba makubwa ambayo kimsingi kwanza yatatatua tatizo la njaa, lakini bado watakuwa na ziada ya kuweza kuzalisha hata kuuza nchi za nje na kuleta pato la Taifa. Kwenye eneo hili tukifanya vizuri tutakuwa tumewasaidia sana Watanzania walio wengi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, eneo lingine naishauri Serikali, dhamira ya Serikali ni kupeleka umeme vijijini. Naomba Serikali sasa ipeleke umeme vijijini na iangalie maeneo yote ya nchi. Tusije tukawa na maeneo ambayo mengine yananufaika na sehemu nyingine hakuna. Ni vizuri umeme vijijini ukapelekwa kwenye maeneo yote hasa kwenye mikoa ile ambayo iko pembezoni. Nafurahi Mheshimiwa Waziri wa Fedha na yeye ametoka kwenye maeneo ya pembezoni, anajua mazingira jinsi yalivyo. Naomba sana Serikali iweze kuangalia maeneo hayo ili iweze kuwasaidia wananchi.

Mheshimiwa Spika, suala la barabara. Nchi yetu

ilikuwa na dhamira ya dhati kuhakikisha Mikoa yote inaunganishwa. Namwomba sana Waziri wa Fedha aangalie sasa uwezekano wa kuunganisha mikoa ambayo bado haijaunganishwa kwa barabara za lami. Mkoa wa Rukwa uunganishwe na Katavi, Mkoa wa Katavi na Kigoma, Mkoa wa Tabora na Kigoma, Mkoa wa Katavi na Tabora. Tunahitaji maeneo yote hayo yaweze kuunganishwa ili yaweze kutoa mchango mzuri kwa pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, haya maeneo yalisahaulika. Kwenye bajeti hii tunaomba sasa dhamira ile ya Serikali iweze kuonekana. Mheshimiwa Waziri wa Fedha anajua mazingira yalivyo na anakotoka. Tayari Mkoa wa Kigoma hauna mawasiliano na Mkoa wa Kagera, Mkoa wa Kigoma hauna barabara za lami na Mkoa wa Katavi; Mkoa wa Kigoma bado hauna mawasiliano na Mkoa wa Tabora sambamba na Katavi na Tabora. Tunaomba ile miradi iliyopangwa iweze kusimamiwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mwisho nisisitize zaidi huduma ya maji vijijini. Tunaomba sana, fedha ambazo zinapatikana kwa michango ambayo tutaichangia hasa ile Sh.40/=, tuielekeze iende kutatua tatizo la maji. Katika maeneo haya tutakuwa tumewasaidia sana wananchi hasa akinamama walio wengi vijijini. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba na kuishauri Serikali iangalie mazingira haya kuyaboresha na tupeleke hii miradi iweze kwenda kuwasaidia wananchi kwenye maeneo hayo ili waweze kufanya shughuli za uzalishaji kwani bila kuwa na maji uwezekano wa kupata nafuu ya kuzalisha ni mdogo sana...

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Spika, naunga mkono hoja. Ahsante.