Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Amb Dr. Diodorus Buberwa Kamala

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nkenge

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. BALOZI DKT. DIODORUS B. KAMALA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Labda nianze kutoa tu masuala machache ya utangulizi na hii ni kwa faida tu ya wachumi na wale ambao siyo wachumi wanaweza kujifunza. Jambo la kwanza ambalo ni neutral, tunaposema Serikali inatekeleza D by D, jambo muhimu siyo nani anakusanya fedha hizi, ni kwamba fedha hizi zikishakusanywa nani anazitumia? Nani anafanya maamuzi ya kuzitumia? Hilo ndilo jambo la msingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia unapoamua kwamba unaongeza Sh.40/= kwa lita, sasa wachumi hata tungekusanya Maprofesa wa Uchumi humu kwenye ukumbi huu, wote wanaweza wakabishana; kuna wengine watasema labda bei zitaongezeka, kuna wengine watakwambia bei hazitaongezeka. Inategemea wachumi hawa walisomea Vyuo vipi na waliwaelewa vipi Walimu wao? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mmoja aliyefundishwa vizuri atakwambia kulingana na taarifa zilizowasilishwa Bungeni, Kitabu cha Mpango wa Maendeleo 2017/2018, ukikiangalia na taarifa iliyotolewa na World Bank iliyoko kwenye kitabu kile, kinakuonesha kwamba bei ya petroli mwaka 2014 kwa ujazo wa lita 1,000 ilipungua kutoka dola 905 kwa wastani mwaka 2014 mpaka dola 462. Kwa hiyo, atakwambia trend ya bei ya mafuta katika Soko la Dunia imekuwa ikipungua kutoka dola 905 kwa wastani mpaka dola 462.

Mheshimiwa Spika, mwingine atakuambia kuhusu diesel. Utauliza, je, diesel? Atakujibu kulingana na takwimu ambazo zimetolewa na World Bank kwamba nayo ilipungua bei kutoka dola 809 mwaka 2014 mpaka dola 380; na mwingine atakwambia kuhusu mafuta ya taa nayo pia yalipungua kutoka dola 407 mpaka dola 406 kwa ujazo. Kwa hiyo, atakwambia kwa kuwa trend inaonesha bei hizi zimekuwa zikipungua, hivyo, ongezeko lolote litalotokea katika masuala mengine ita-offset kile kinachotokea kwa sababu bei katika Soko la Dunia mwenendo ni kupungua sana kuliko chochote kile unachofanya kuongeza. (Makofi)

Kwa hiyo, itategemea huyo mtu alisomea wapi na anaelewa vipi kutafsiri hizi takwimu. Ukikutana na mwanafunzi wangu niliyemfundisha darasani ambaye sasa ni Naibu Waziri wa Fedha, yeye atakwambia alipofundishwa na Mwalimu mmoja aliyebobea kwenye uchumi, alimwambia unapoangalia haya masuala ya bei kuongezeka na kupungua, kuna kitu kinaitwa surplus demand na kuna kitu kingine kinaitwa consumer surplus na producer surplus.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, atakwambia siku zote unapoongeza bei most likely, consumer surplus inaweza ikabadilika, lakini katika hili inaonekana ambaye atalazimika kupunguza bei ni yule consumer surplus kwa sababu kuna ushindani katika soko hili na kama mtu hatataka kushindana, ataondoka. Sasa huu ni uchumi mwepesi ambao nisingependa kuendelea na nawakaribisha wengine wasome vitabu vya Economics Made Simple. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, naomba niseme haraka haraka kabla sijasahau kwamba bajeti hii ni nzuri na naiunga mkono kwa asilimia mia moja. Naunga mkono kwa kuzingatia bajeti nyingi ambazo nimeziona nikiwa katika Bunge hili, lakini pia na bajeti zinazotokea maeneo mengine; na ukiangalia malengo yetu manne ni kwamba bajeti hii itatusaidia kuweza kuyafikia. Malengo yetu siyo mengi, ni machache. Tunasema tunataka kujenga uchumi wa viwanda, tunasema bajeti hii itatusaidia; tunasema tunataka kujenga uchumi wezeshi, bajeti itatusaidia; tunasema tunataka bajeti hii itusaidie kuunganisha maendeleo ya viwanda na maendeleo ya watu, bajeti hii itatusaidia.

Mheshimiwa Spika, kubwa tunasema ili bajeti hii iweze kutekelezeka, tunahitaji watu wenye uwezo wa kuisimamia vizuri na tunaona sasa tunaye Rais ambaye anaonesha yuko tayari kusimamia na ameanza na makinikia. Kwa hiyo, tusiwe na wasi wasi na jambo hili. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kuna mambo ya kuzingatia ili tuweze kufanikiwa vizuri. Siwezi kuyataja yote, nitataja machache. La kwanza ambalo lazima tulizingatie, chakula ni uchumi, chakula ni ushindani. Lazima tuongeze nguvu zetu za kuhakikisha tunasimamia vizuri Sekta ya chakula. Ukiangalia takwimu tulizonazo, taarifa iliyotolewa na Benki Kuu inaonesha mwaka 2014 wastani katika Wakala wa Hifadhi ya Chakula, zilipanda mpaka wastani wa tani 455,000. Ilipofika mwaka 2017 zimepungua mpaka wastani wa tani 86,000 kwa mwezi, Januari, 2017 zilipungua.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kutoka tani 455,000 wastani wa hifadhi ya chakula ndani ya ghala kwenda mpaka tani 86,000 lazima zote tukubali kwamba kuna tatizo. Kwa hiyo, lazima tuelekeze nguvu zetu za kuongeza wastani, kwa sababu tunapozungumza uhaba wa chakula kwenye nchi au chakula kilicho kwenye nchi tunaangalia chakula kilichoko kwenye ghala la Taifa na maghala mengine ya watu binafsi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, unapoona kwenye ghala la Taifa inapungua kutoka wastani wa 455,000 kwa mwezi hadi 86,000 kwa mwezi, maana yake kuna tatizo ambalo hatuwezi kulifumbia macho, lazima tulishughulikie. Lengo letu kwa kuwa sitaki kusema mengi, tulenge kuongeza wastani wa chakula kwenye ghala letu la Taifa kutoka tani 86 kwa mwezi hadi kuelekea tani 500,000 kwa mwezi.

Mheshimiwa Spika, ukisoma kitabu cha Mpango wa Maendeleo kimeeleza vizuri kwamba chakula ni muhimu na lazima tujielekeze katika kuongeza hiyo hifadhi. Ili tuweze kufanya hivyo yapo mambo mengi ya kufanya. Moja, ni lazima tutoe uhuru kwa wakulima wetu kuwa na uhuru wa kulima na kuamua wapi wauze mazao yao bila kuwekewa masharti. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, South Sudan sasa ni mwanachama wa Afrika Mashariki, wana soko kubwa la kupenda kununua mazao yetu, lakini mara nyingi tumekuwa tukizuia wakulima wetu kwenda kuuza mazao popote wanapotaka wakati inatolewa bei kubwa. Kwa kufanya hivyo, tunawaondolea uhuru wa kuuza popote na tunawazuia kwenda kwenye mabenki kukopa ili kuongeza uzalishaji. Ndiyo maana nasema, lazima tuongeze uhuru kwa mkulima. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia lazima tuachane na kutoa vibali vya upendeleo. Kule Mtukula ukienda unakuta kuna baadhi ya watu, wengine tunao Bungeni humu, sitapenda kuwasema, wengine wanapata vibali vya kupeleka mazao nje cha nchi, wengine hawapewi vibali.

Mheshimiwa Spika, nilijaribu kufuatilia hili, nikagundua inahusisha Waheshimiwa wazito tu. Ni uchafu gani huu? Sasa sitawataja majina yao humu, lakini niwaombe tu waache kwa sababu wale wakulima wadogo wadogo na wao wanayo haki ya kuuza mazao yao kokote kule. Kwa hiyo, jambo hili liangaliwe.

Mheshimiwa Spika, napenda kwa haraka haraka kuzungumzia hoja nyingine ambayo inahusu suala la kuondoa ugonjwa wa mnyauko wa migomba. Kule Kagera tunao ugonjwa unaosumbua sana, tumejitahidi kupambana nao lakini wataalam wetu wa MARUKU wakubali kwamba wameshindwa. Serikali iongeze fedha ili tuweze kuondoa ugonjwa huu kabisa kuliko kudhibiti tatizo la uzalishaji.

Mheshimiwa Spika, jambo lingine ambalo ningependa kulizungumzia ni kwamba ukiangalia taarifa ya hali halisi ya uchumi…

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa mzungumzaji)

Mheshimiwa Spika, ahsante. Kama muda umekwisha, mengine nitachangia kwa maandishi, lakini naunga mkono hoja.