Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Dr. Mary Michael Nagu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Hanang'

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. DKT. MARY M. NAGU: Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru sana kunipa nafasi hii ili nami nipate kuchangia bajeti hii ya Serikali. Nianze kabisa kwa sababu muda ukiisha unaweza hata ukasahau kuunga mkono bajeti hii au hoja ya Waziri wa Fedha, kwa hiyo, nasema kutoka mwanzo naiunga kwa nguvu zote hoja hii ya Waziri wa Fedha. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nianze kwa kuungana na Wabunge wenzangu kumpongeza na kumshukuru sana na kumuombea Mwenyezi Mungu Rais wetu Mheshimiwa John Pombe Magufuli kwa ujasiri wake huo aliouonyesha kuhusu suala la makinikia na kuibua ukweli wa uwekezaji wa kinyonyaji na uovu unaotudidimiza badala ya kutuondolea umaskini na udhalili. Rais amefanya jambo kubwa na kwa kweli hajajifanyia mwenyewe amewafanyia Watanzania. Kwa hiyo, sisi wote tumuunge mkono, tumsaidie na tuone kwamba hii economic order ya dunia inapokuja kwenye nchi yetu lazima kuwe na watu ambao wanajitolea na lazima iingie kwenye vitabu vya historia kwamba Mheshimiwa Magufuli amesaidia sana katika kuondoa economic order ya kinyonyaji. Tukifaulu hapa tujue nchi hii itakuwa imechangia mchango mkubwa sana katika uchumi wa dunia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala zima kama alivyoelekeza litakuwa kwenye sera na kwenye sheria tutakavyoziangalia hapa Bungeni. Wote ambao ni wataalamu tuziangalie kwa uzuri ili kazi hii aliyoifanya ilete manufaa kama yeye alivyokuwa anategemea. Mwenyezi Mungu atampa yeye na sisi nguvu tuwe pamoja kuona kwamba madini ambayo Mwenyezi Mungu ametupa yanaleta manufaa katika nchi yetu na kuendeleza nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nimpongeze Mheshimiwa Waziri, Naibu Waziri na Katibu wake Mkuu na watendaji wote kwa kuikalia bajeti hii. Bajeti hii imefanyiwa kazi, ina ubunifu mkubwa, imesikiliza kilio chetu ambacho kimetokana na wananchi, nawapongeza sana. Haitoshi kuwa na bajeti bali utekelezaji ndiyo utakaoleta maana kubwa. Naomba tutekeleze bajeti hii na kule kwenye Halmashauri kama ushuru hautatozwa hovyo hovyo, nawaambia kilimo, ufugaji, uvuvi utaendelea na huduma mbalimbali zitapatikana bila shida. Kwa hivyo, suala la usimamizi lazima lipewe kipaumbele. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Wizara ione umuhimu wa kilimo, ufugaji na uvuvi. Wenyewe ndiyo waliotuambia kwamba kilimo kinachangia asilimia 29.1 na viwanda vinachangia asilimia 25 na uchangiaji wake unapanda, lakini kilimo ukuaji wake unashuka na ni wao wenyewe ndiyo wameandika. Naomba tu reverse hii trend ya ukuaji wa kilimo kwenda chini kwa sababu mchango hautaongezeka kwenye Pato la Taifa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba sana, ili kilimo kiendelee tuhakikishe kwamba bajeti ya kilimo inayotengwa basi itolewe kwa wakati. Ukienda ukasaidia wakulima kupata mbegu wakati msimu wa kupanda umepita hujasaidia wakulima. Wakulima wakitaka pembejeo wakati ukifika lakini hawapati hawatafaidika. Naomba sana tuangalie ni wakati gani tunafanya mambo yote haya.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ukiangalia madini yanakua kwa asilimia 13, uchukuzi na mawasiliano unakuwa kwa asilimia kubwa sana, lakini ukiangalia mchango wao kwenye pato la Serikali ni mdogo sana. Hicho ndiyo kielelezo kwa nini umaskini wa Tanzania haupungui kwa sababu kule kwenye kilimo, ufugaji na uvuvi ambapo kwa kiasi kikubwa ndipo walipo wananchi wote wa Tanzania hakujapewa uzito. Kwa hiyo, Watanzania hawataondokana na umaskini kama hatutawakazania. Naomba sana hili mlitambue, mmetuonyesha wenyewe kwenye takwimu. Kwa hiyo, naomba sana muone kwamba ili kuondokana na matatizo ya wakulima, kwanza tuhakikishe kwamba wanapata pembejeo, huduma za ugani, masoko na wanapata viatilifu kwa wakati ili mazao yao yasiliwe na wadudu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kitu kimoja, kilimo na ufugaji hautaendelea kama migogoro ya wakulima na wafugaji itaendelea. Nataka niwaambie kwamba hifadhi zinajulikana narudia, kilimo mahali wanapolima panajulikana kwa sababu mazao yanaonekana, wafugaji hawaoni maeneo yao kwa sababu ng’ombe akirudi nyumbani, hamtajua kwamba hilo ndiyo eneo la wafugaji. Naomba mtenge bajeti ya kwenda kutenga maeneo ya wafugaji na wakulima nao hawatapata hasara kwa sababu kama wafugaji wanajua maeneo yao katika kila Wilaya, hawatakuwa na sababu ya kupeleka ng’ombe kwenye mashamba ya watu, hawatakuwa na sababu ya kupeleka mifugo kwenye hifadhi, naombeni sana mfanye hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naomba niongelee habari ya maji, akina mama ndiyo wanaolima mashambani, wakitumia masaa mengi kutafuta maji maana yake muda wa kuwa shambani unapungua. Naomba ile tozo ya shilingi 50 iende kwenye suala la maji. Nampongeza Mheshimiwa Waziri ameonyesha maeneo ambayo yanaongeza bajeti ya maji lakini sehemu hiyo sio ya uhakika. Kama Mfuko wa Maji ukipata tozo hizi kutoka kwenye mafuta au mahala pengine mtakapoamua, tutakuwa na uhakika wa bajeti ya maji na maji ndiyo uhai kama alivyokuwa amesema Mbunge aliyetangulia kuongea. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba vilevile kuongelea ujenzi wa vituo vya afya na zahanati vijijini. Ndugu zangu wananchi wamejitolea kujenga madarasa, zahanati mpaka kwenye lenta na vituo vya afya. Serikali ione basi pale ambapo wananchi wamechangia na yenyewe ichangie. Mahitaji ni mengi, vipaumbele mkiviweka sawasawa, nina hakika bajeti hii itakuwa mkombozi wa Mtanzania na tutaendelea kuona manufaa na umasikini utaendelea kutoweka. Mheshimiwa Waziri utaweka historia kama bajeti hii itatekelezwa. Mheshimiwa Waziri tutaona ulivyotumia nguvu yako kama bajeti itakwenda ilivyopangwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bajeti iliyopita ilitoka kwa sehemu ndogo sana, umeeleza na tumeelewa hatuna ugomvi na wewe lakini sasa hivi kazana na ukusanyaji wa kodi. Hakuna mtu ambaye atakuwa na hiari ya kulipa kodi. Kuna maeneo ambayo tukiyasahihisha kodi itaongezeka na mapato ya Serikali yataongezeka. Kule ambako mmeondoa hizi tozo za ushuru mpeleke nguvu zenu kama kwenye madini, utalii na maeneo ambayo kuna fedha. Tukifanya hivyo ndugu zangu tutakuwa tumejielekeza na tutakuwa na mkakati mzuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba Watanzania tuwe wamoja wakati huu wa vita, vita inataka umoja na mshikamono, vita inataka umakini mkubwa. Msifikiri hao watu watakuwa tayari kurudisha hayo ambayo wametaka kuyachukua, watatudanganya danganya na sisi tuone wapi tunadanganywa. Naomba suala hili la makinikia tulishughulikie wote, Rais ameshaonyesha njia, wataalam na wananchi kwa pamoja na ikiwezekana nchi nzima irindime kuwa na maandamano ili dunia nzima ione kwamba Tanzania ina watu wajasiri wakiongozwa na Rais wao anayepita kwa ujasiri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nawashukuru sana kunipa nafasi hii na Mwenyezi Mungu ambariki Rais wetu, Mwenyezi Mungu ambariki Waziri wetu wa Fedha na Naibu wake na Naibu wake na Watendaji wao na Mwenyezi Mungu abariki Bunge hili na naomba bajeti hii iweze kutekelezeka. Narudia tena, naunga mkono kwa nguvu zote bajeti hii na kwa moyo mmoja.