Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Juma Kombo Hamad

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Wingwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. JUMA KOMBO HAMAD: Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa fursa hii ya kuchangia angalau kwa uchache.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza niwashukuru viongozi wangu wa Kambi ya Upinzani kwa kutupa maelekezo mazuri na kutuongoza na kufikia kwenye ufanisi hadi leo tumo na tunaendelea kujadili katika Bunge hili la bajeti. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, sote humu tunakumbuka kwamba katika dunia hii nchi yoyote hata zile ambazo zimeendelea, tukielekea kwenye uchaguzi kitu cha mwanzo wagombea Urais wanachokijadili ni suala la kuongeza ajira kwa wananchi wao hususani kwa vijana. Pili wanajadili mkakati imara na madhubuti wa kuondoa umaskini. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niungane na msemaji aliyepita hivi punde, Mheshimiwa Silinde kwamba bado Mheshimiwa Mpango katika hotuba hii hajatuonyesha mkakati imara wa Serikali namna gani na kwa njia zipi ataondoa tatizo la ajira kwamba ni kwa namna gani atawaajiri vijana wa Kitanzania. Pia ni mkakati gani atakaoutumia katika kuhakikisha umaskini uliokithiri wa Watanzania unapungua kwa kiwango fulani. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika hili nina imani, suala hili mara nyingi linajitokeza hapa Bungeni, dada yangu pale Mheshimiwa Angellah Kairuki ana jawabu lake moja mara zote huwa analizungumza kwamba tunafanya uhakiki na baada ya kumaliza uhakiki tutaajiri vijana wa Kitanzania kwa kiasi fulani. Hebu wakati wa kufanya majumuisho, Mheshimiwa Waziri wa Fedha na Mheshimiwa Kairuki mje basi mtueleze ni lini sasa mtawaajiri vijana wa Kitanzania. Tunaenda kwenye mwaka wa pili sasa wa Rais John Pombe Magufuli bila vijana wa Kitanzania kupewa ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili ambalo napenda kulizungumza ni mfumo wa kodi ambao tunauendeleza Tanzania. Miongoni mwa mambo ya Muungano suala la Wizara ya Fedha siyo suala la Muungano lakini kodi ni suala la Muungano, kwa maana ya TRA. TRA ipo na inakusanya kodi kwa maslahi ya nchi nzima ya Tanzania kwa maana ya Zanzibar na Tanzania Bara. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa masikitiko makubwa ni sahihi kabisa kwamba Zanzibar haifuati mfumo wa kodi wa kilimwengu kwa maana ya mfumo wa kuthaminisha bidhaa kwa ajili ya kodi, ni sahihi kwamba Zanzibar mfumo huu imeukataa na haiufuati. Haiufuati kwa sababu ya uchumi wake mdogo na population ya Wazanzibar ni ndogo, uchumi wa Zanzibar hauwezi kuulinganisha na uchumi wa Tanzania Bara. Tanzania Bara ina mchango mkubwa katika kufanya uchumi wa Zanzibar hauendi mbele kwa sababu ya mfumo mbovu wa kodi tunaouendeleza Tanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka kusema kwamba suala la Mtanzania yeyote kutoka Zanzibar na kitu pengine cha shilingi milioni moja, kwa mfano tv akalipishwa kodi pengine laki moja na nusu Zanzibar, anakuja kutumia katika matumizi yake ya kawaida lakini anafika Tanzania Bara bandarini anaambiwa alipe difference, hii sio sahihi. Mheshimiwa Waziri wa Fedha ipo haja sasa ya kutafuta namna bora ya mfumo wa kodi ili kuhakikisha kwamba wajasiriamali wadogo wadogo wa Zanzibar wana-enjoy soko la Tanzania Bara. Leo anatoka mjasiriamali na mzigo wake mdogo wa shilingi pengine milioni moja au moja na nusu anakuja kutafuta riziki Tanzania Bara, lakini mzigo ule Zanzibar kalipia kodi pengine shilingi laki mbili, lakini akifika Tanzania Bara anaambiwa lipia tena laki mbili tukiwa na dhana eti ni difference, hii siyo sahihi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tena mdogo wangu mmoja alizungumza kule kwamba hata zile bidhaa zinazotoka ndani ya nchi, zinazozalishwa Tanzania Bara au Zanzibar lakini zikivuka kutoka Tanzania Bara kuja Zanzibar au kutoka Zanzibar kwenda Tanzania Bara pia zinalipishwa kodi. Hata Afrika Mashariki tumeandaa utaratibu wa kusameheana kodi kwa bidhaa ambazo zinazalishwa ndani ya Afrika Mashariki, leo iweje ndani ya Tanzania moja tuna mifumo ya ajabu ya kulipishana kodi? Mheshimiwa Waziri wa Fedha hii siyo sahihi.
(Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi nitoe ushauri tungekuwa na mfumo kwamba basi kama tuna difference tungekuwa na baadhi tu ya bidhaa au aina fulani ya bidhaa au thamani fulani ikifikia ndiyo suala la difference hapa mnalizingatia. Siyo sahihi kwamba mjasiriamali ana mzigo wake mdogo anakuja kutafuta riziki Tanzania Bara au mjasiriamali anaondoka hapa na mzigo wake mdogo kwenda Zanzibar tuwe na mfumo wa ajabu wa kodi ambao unadumaza upande mmoja wa Muungano. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu Tume ya Pamoja ya Fedha, ni sahihi kwamba Zanzibar stahiki yake kwa mujibu wa sheria ni asilimia 4.5. La ajabu la kwanza, Mheshimiwa Mpango, ipo haja sasa kuufanyia review ya mfumo huu wa asilimia 4.5 na kuuangalia upya kwa sababu ulipitishwa miaka 40 nyuma. Uchumi wa nchi hizi unabadilika, lakini uchumi wa Tanzania Bara siyo uchumi wa Zanzibar, uchumi wa Zanzibar ni uchumi wa bidhaa, uchumi wa Tanzania Bara umejitawanya katika mambo tofauti tofauti. Sisi kule Zanzibar hatulimi korosho, ufuta wala pamba, uchumi wetu unategemea bandari na bidhaa kutoka nje. Inapofika mahali kwamba suala la mfumo wa Tume ya Pamoja ya Fedha kutokuwepo…

TAARIFA

Mheshimiwa Mwenyekiti, jawabu limetoka, tena limetoka kwa watu wa CCM kule nyuma kwamba Makunduchi wanalima korosho, lakini mbili/ tatu za kula wenyewe, sisi tunazungumzia zao la biashara.(Makofi)

Mheshimiwa Mattar ni rafiki yangu, umerogwa na nani? (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika suala la Tume ya Pamoja ya Fedha, nikuombe Mheshimiwa Waziri wa Fedha utakapokuja kuhitimisha ulitolee majibu suala hili kwa sababu limechukua muda mrefu na hili ndiyo mwarobaini wa kukuweka wewe salama. Mheshimiwa Mpango nataka nikuhakikishie kwamba Wazanzibari hawatokuelewa bila suala hili kupata ufumbuzi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka nimhakikishie Mheshimiwa Mpango na tuna ushahidi kwamba hata hiyo asilimia 4.5 kwanza haifiki kikamilifu, ikifika ni asilimia 2.5 au 3.5 lakini pia hata huo mrejesho wenyewe hauendi. Mheshimiwa Mpango hadi sasa hivi Zanzibar inakudai mrejesho tena karibuni wa shilingi bilioni 30, Mheshimiwa Mpango umerogwa na nani? Yaani wewe huna haya wala aibu? Yaani Zanzibar leo inaikopa huna aibu? Kwa uchumi ule mdogo unakuja kuikopa Zanzibar? Hili Mheshimiwa Mpango inabidi uje utujibu ni lini fedha hii utairejesha Zanzibar? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho, naomba nizungumzie suala la madini. Hili suala limezungumzwa kwa mapana yake. Mimi nataka kuzungumza kitu kimoja kwamba ili Watanzania wawaelewe CCM na wafute ile dhana inayosambaa kwenye mitandao kwamba CCM ni ukoo wa panya, baba mwizi, mama mwizi na mtoto mwizi ni kwa waliohusika kupelekwa mahakamani. Hii ni kwa sababu viongozi walioshutumiwa wote walikuwa viongozi waandamizi wa CCM, majanga haya yanafanywa viongozi hao ni viongozi wakuu wa CCM, ni Mawaziri, Makatibu Wakuu na kadhalika, tuone sasa viongozi wale wanapelekwa mahakamani, wamechunguzwa na wamechukuliwa hatua stahiki kwa sababu tayari ripoti mnayoita ya kisayansi imethibitisha kwamba viongozi hawa wamehusika kwa namna moja au nyingine. Hapo ndiyo msemo huo tutau- delete sasa kwenye mitandao kama CCM ni ukoo wa panya kwamba baba mwizi, mama mwizi na viongozi wengine wezi. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ahsante sana.