Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Mendard Lutengano Kigola

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mufindi Kusini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. MENDRAD L. KIGOLA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru sana kwa kunipa nafasi na mimi niweze kutoa mchango wangu katika haya maeneo mawili Hali ya Uchumi na Bajeti ya Serikali.

Kwanza kabisa nianze kumpongeza Waziri wa Fedha pamoja na Naibu Waziri na cabinet nzima ya Wizara ya Fedha kwa bajeti nzuri mliyoiandaa ambayo Watanzania tunaipokea kwa mikono miwili. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, labda nianze kwanza na masuala yanayohusiana na jimbo langu ambao kwenye jimbo langu tuna kazi kubwa ya ujenzi wa Hospitali ya Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi ambayo mpaka sasa hivi Halmashauri ya Wilaya ya Mufindi hatuna hospitali. Na bahati nzuri sana kwenye kamati zetu za madiwani vikao vya madiwani kwa pamoja tumesharidhia kwamba hospitali hiyo itajengwa katika Kata ya Igowole na bahati nzuri kata ile wameshatoa eneo kubwa sana. Na eneo lile tutajenga Makao Makuu ya Halmashauri pamoja na hospitali.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Waziri katika fedha zake atusaidie katika ujenzi ule ambao kwenye plan tumeshauanza mwaka huu. Na kama halmashauri tumeshatenga shilingi milioni 100 ambayo inasaidia kuendeleza katika ujenzi huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la pili, naiomba Serikali watu wa Mgololo ambao walikuwa wanafanyakazi katika Kiwanda cha MPM watu wale walikuwa wanadai madai yao kati ya Serikali na Mwekezaji; bahati nzuri ile kesi ilienda mahakamani na imeisha na hukumu imetoka. Ninaomba kwa sababu wameshinda na wanatakiwa walipwe kama shilingi bilioni 18, naomba Serikali iwalipe wale wafanyakazi wamepata mateso ndani ya miaka karibu karibu kumi na moja, lakini hatima yake sasa hivi ilishafikia, sasa naiomba Serikali iweze kuwalipa ili wananchi wale watokane na matatizo ambayo wameyapata kwa muda mrefu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niongelee masuala ya maji, tuna mradi mkubwa sana pale Sawala ambao ni mradi wa Serikali na ni muda mrefu sana, ni miaka sita sasa na mkandarasi tulikuwa tumempata. Yule mkandarasi alijenga matenki ya maji na system ya maji, lakini bado mradi ule haujaisha. Wananchi wa Kata ya Mtwango, Vijiji vya Sawala, Rufuna, Kibao wanapata shida sana ya maji. Na Serikali ilishaahidi kwamba mwaka huu inaweza kutimiza ahadi hiyona ikamaliza. Kwa sababu ujenzi ulianza, naiomba Serikali katika bajeti hii. Bahati nzuri nimeona kwenye bajeti mmetenga shilingi bilioni mbili basi itumike vizuri ili tuweze kumaliza mradi ule na wananchi wa Sawala waweze kupata maji vizuri.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nitoe pongezi kubwa sana kwa Serikali hii ya Mheshimiwa wetu mpendwa Dkt. John Pombe Magufuli, Rais wetu amefanya vitu vingi sana ndani ya mwaka mmoja. Kila mtu anavijua na bahati nzuri Wabunge wenzangu wamesema mara mbili mara tatu wanarudia rudia na mimi napenda nirudie; kwa mikono miwili nampongeza sana Rais wetu John Pombe Magufuli kwa kazi yake anayoifanya nzuri na sisi Watanzania wote kwa pamoja lazima tumuunge mkono na tumuombe kwa Mwenyezi Mungu aweze kufanya kazi yake vizuri. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashangaa sana, kuna watu wengine wanatoa maeneno ya kupinga. Kwanza Rais wetu ni doctor. Wewe huwezi kuwa ukampinga doctor bila reason, lazima uwe na fact za kumpinga. Sasa huyu anaonesha kwa vitendo kwamba tukisema tuorodheshe vitu alivyofanya ndani ya mwaka mmoja kwa mtu mwenye akili timamu lazima atakubaliana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kitendo tu kile cha kuanza kusema elimu bure amefanya na tumeona, kitendo cha kusema kununua ndege amenunua ndege tumeziona kwa macho siyo kwa kuambia tu tumeona kwa macho. Waheshimiwa Wabunge tulikuwa tuna tatizo kubwa sana ya madawati kwa kushauriana Wabunge pamoja na Rais wetu madawati amepeleka kwenye shule zetu na maswali tumepunguza. Mheshimiwa Rais alisema kwamba kujenga majengo pale Universty of Dar es Salaam wanafunzi walikuwa wanapata shida sana mabweni, amejenga. Sasa kuna watu hapa kama hatumpongezi hata Mungu atatushangaa. Lazima tumpe haki yake. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza wakati anaingia madarakani alisema nchi hii ni tajiri, na sisi tunakubaliana alisema ina maziwa, ina mito, ina madini na akasema atadhibiti vizuri ile mianya ya ufisadi amefanya. Sasa mtu anaposisima anapinga maneno haya mazuri na anafanya kwa vitendo itakuwa ni wa ajabu. Juzi hapa tumeona katika ripoti sipendi sana nirudie Watanzania wengi sana tumeshangaa katika ripoti ile, na ripoti kweli imesikitisha kwamba fedha nyingi sana zilikuwa zinapotea lakini sasa hivi ameanza kudhibiti vizuri na bahati nzuri hata wale ambao alikuwa wanahusika na wafadhili wale wawekezaji wanakubaliana kwamba lazima wakae wazungumze lakini sisi lazima tukubaliane nalo. Sasa isionyeshe tena watu wengine wanapinga kitu ambacho kinaeleweka. Na zile hela tukipewa tunajua kabisa tukisema kwamba Tanzania itafikia uchumi wa kati, tukilipwa zile fedha lazima uchumi wa kati tutafikia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunasema nchi hii ni ya viwanda, viwanda haviwezi kujengeka kama hatuna fedha. Lakini bahati nzuri sana ukikusanya mapato ya kutosha unaweza ukapanga mipango na ikapangika na kama huna fedha huwezi ukapanga mipango ikapangika. Lakini Rais wetu anatusaidia kutafuta fedha/vyanzo vya mapato. Hicho ni chanzo cha mapato tayari kwa sababu kudai madeni, kuziba mianya ni sehemu ya chanzo cha mapato cha kukusanya fedha ili tuweze kupata fedha nyingi tuweze kuendeleza miradi yetu ambayo inatukabili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, juzi, juzi hapa amesema ujenzi standard gauge, na tukijenga kweli standard gauge Tanzania hii lazima uchumi utakuwa wa kati. Kwa sababu mizigo yote ambayo inasafirishwa kwa njia ya barabara ambayo barabara zinaharibika kila siku, mizingo mizito ikasafirishwa kwenye reli halafu wasafirishaji wa abiria tukasafiri kwenye barabara za kawaida. Barabara zitaweza kudumu wa muda mrefu sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho naomba nisizitize sana, Serikali imeahidi kupeleka umeme kila kijiji na kwenye Jimbo langu la Mufindi Kusini katika vijiji vyote 88 na bahati nzuri walisema watapeleka katika vitongoji vyote; wamesema watapeleka, naomba Serikali kwenye bajeti hii mwaka 2017/2018 ifanye kama ilivyokuwa imepangwa hili litatusaidia sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile kwenye masuala ya maji bahati nzuri Waziri wa Maji alisema tuandike proposal inahusiana na matenki yale nane ambayo yalikuwa bado hayajangwa ambapo lilikuwepo tanki la maji pale Igowole, Nyololo, Itandula, Idunda, Ihomasa na Sawala amesema atamalizia. Naomba afuate kama tulivyomwandikia proposal ile ambayo tumempelekea ili wananchi wa jimbo langu la Mufindi Kusini ili waweze kupata maji bila matatizo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, la mwisho niwashukuru sana wafadhili wanaonisaidia ufadhili maji katika Jimbo langu Mufindi Kusini akiwepo Mr. Fill na Mama Jully mpaka sasa hivi tunavyoongea wako Mufindi, wale wanatusaidia sana kuchimba maji katika Jimbo langu la Mufindi Kusini na sasa hivi wameniahidi kwamba watasaidia kuchimba maji katika shule za msingi na Sekondari.

Kwa hiyo, wawekezaji hawa mimi nawapongeza sana na nawaomba Wizara ya Maji iwa-support hawa wafadhili. Pale wanapohitaji msaada basi watoe msaada ili waweze kupata moyo kuendelea kutoa msaada wa maji katika nchi yetu ya Tanznaia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho kabisa naunga mkono bajeti ya Serikali kwa asilimia mia moja kwa sababu ni bajeti ambayo inaeleweka, kila mmoja anai-support na sisi tunawaombea kwa utekelezaji mwema, ahsante sana. (Makofi)