Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Jumaa Hamidu Aweso

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Pangani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. JUMAA H. AWESO: Mheshimiwa Mwenyekiti, nikushukuru kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia bajeti iliyokuwa mbele yetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote kwanza naomba nimpongeze Dkt. Mpango kwa namna ya mpango wa bajeti alivyoipanga imepangika kweli kweli, bajeti ipo bomba. Nataka nimwambie Mheshimiwa Mpango wali wa kushiba siku zote unaonekana kwenye sahani. Na naunga mkono kama mimi Mbunge kijana kwa sababu bajeti hii imeenda kujibu matatizo ya wakulima, imeenda kujibu matatizo ya wafugaji, lakini pia imeenda kujibu matatizo ya wavuvi. Ni watu wenye sifa tu ya miembe ndio wanaweza wakapinga bajeti hii. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kupinga si dhambi na ni jambo jema, lakini si kupinga kila kitu. Na ukisoma aya za Qurani Mwenyezi Mungu anasema; “waama bi neemati Rabbikka fahadith” (zielezeeni neema za Mwenyezi Mungu kwa kushukuru). Watanzania tulikuwa tunamuomba Rais ambaye ataweza kuleta maendeleo katika taifa letu. Unaweza pia usijue kusoma, lakini pia picha ukashindwa kuiona? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ndugu zangu Wabunge tutapata laana kubwa kwa Mwenyezi Mungu kama tutampinga Mheshimwia Rais Dkt. John Pombe Magufuli. Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli ni jembe tena limekuja wakati mwafaka. Tulitumie ili tuhakikishe kwamba tunaenda kulima na kupanda kwa uhakika katika nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mimi katika Jimbo langu la Pangani tulikuwa na mabadiliko ya tabianchi bahari inakula Mji wa Pangani, lakini kwa muda mfupi leo tunatengenezewa ukuta wa bahari. Kulikuwa na maeneo ambayo hayajawahi kuona umeme leo wanapata umeme. Mungu atupe nini atupe gunia la chawa tujikune? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama nilivyosema awali, bajeti ni nzuri lakini naomba nishauri katika maeneo yafuatayo:-

Mheshimiwa Mwenyekiti, ujenzi wa barabara ni kichocheo kikubwa cha maendeleo katika Taifa. Lakini pia inaweza kuchochea ajira katika maeneo katika jamii yetu na hata katika kuboresha huduma za kijamii. Tunaona maeneo mbalimbali ambayo yalikuwa hayana barabara leo yamepatiwa barabara maendeleo yake ni makubwa. Niombe fedha zilizotengwa katika bajeti hii ili kuhakikisha kwamba zinafika kwa haraka ili miundombinu ya barabara katika maeneo mbalimbali ya Taifa letu iboreshwe.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa mfano katika Jimbo langu la Pangani tulikuwa na changamoto ya barabara, lakini katika bajeti hii tumetengewa fedha kwa ajili ya kuanza ujenzi. Naiomba Serikali fedha zile ziende ili kuhakikisha kwamba barabara ya Tanga - Pangani - Saadani inajengwa ili wananchi wangu wa Pangani waweze kupata maendeleo kwa kasi kubwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini suala la pili, ni suala zima la upatikanaji wa maji. Nchi yetu ina vyanzo vingi vya maji lakini maeneo mengi bado kumekuwa na tatizo la maji. Naomba niseme anayelala na mgonjwa ndiye anayejua mihemo ya mgonjwa. Sisi katika Jimbo la Pangani bado tunakuwa na changamoto kubwa ya maji. Tuna Mto Pangani ambao unapita katikati ya mji lakini bado wananchi wangu wanatatizo la maji. Niombe bajeti hii iende ikatatue tatizo la maji kwa wananchi wa Pangani ili twende kuwatua ndoo wananchi wale wa Pangani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sina maneno mengi sana ya kusema, lakini kubwa kwa kumalizia nataka nizungumze tunapozungumzia uchumi wa viwanda lazima tuangalie afya za watu wetu. Hauwezi ukalima, hauwezi ukazalisha pasipokuwa na afya. Tunaona maeneo mbalimbali bado kumekuwa na changamoto ya vituo vya afya, na hata Zahanati. Niombe Serikali katika bajeti hii kuhakikisha kwamba inatenga fedha hizo zifike kwa haraka ili kuhakikisha kwamba vituo vya afya na zahanati vinajengwa na vifaa tiba vinapatikana ili wananchi wetu waweze kupata maendeleo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo ahsante sana na Mwenyezi Mungu awabariki sana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.