Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

Hon. Lathifah Hassan Chande

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hali ya Uchumi wa Taifa Kwa Mwaka 2016 na Mpango wa Maendeleo ya Taifa kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018

MHE. LATHIFAH H. CHANDE: Mheshimwa Mwenyekiti, ahsante kwa kunipa nafasi hii na mimi niweze kuchangia mjadala huu wa bajeti. Kwa kuwa Wabunge wengi hapa wameongea hili suala la makinikia naona ni vema na mimi niweze kuligusia kidogo pia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, suala la wizi wa madini ya nchi hii vilevile suala la mikataba mibovu ya madini na suala ya sheria mbovu za madini imekuwa ni kilio cha wapinzani kwa miaka mingi sana na Watanzania kwa ujumla. Na kwa kuwa Serikali hii hii ya CCM ndiyo iliyolea huo wizi kwa kipindi chote hicho kwa kuleta mikataba mibovu ya madini na sheria mbovu za madini, basi Serikali hiyo ya CCM pamoja na Wabunge wake wa CCM wanawajibu wa kuwaomba msamaha na kuwaomba radhi kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningeomba kuchangia mjadala huu wa bajeti iliyoletwa hapa. Naunga mkono maoni ya Kambi Rasmi ya Upinzani na ningependa kuanza kwa kuongelea juu ya miradi ya maendeleo. Serikali inapaswa ielekeze pesa nyingi katika miradi ya maendeleo ambayo ina wananchi wengi (labour intensive), kama vile sekta za uvuvi, kilimo, na sekta za ufugaji. Kwa nini nasema hivyo, nasema hivyo kwa sababu hizi ni sekta ambazo zina shughuli ambazo ni endelevu na haziitaji watu walioandaliwa skilled labour.

Vilevile tofauti na hivyo leo hii Serikali inajinadi kwamba imetoa ajira kwa wananchi wengi lakini hizo walizozitoa siyo ajira bali ni vibarua ambavyo havina mwendelezo wowote. Kwa sababu wameelekeza pesa nyingi kwenye miradi ya maendeleo ambayo ni capital intensive ambapo ili iweze kufanikiwa hiyo miradi lazima itumike mitaji ya kuwezesha kununua mashine na mitambo na pesa nyingi zinaelekezwa kwenye kuwalipa wasimamizi na wataalam ambao wengi wao siyo Watanzania ni wananchi kutoka nchi nyingine tofauti, hilo la kwanza. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pili ningependa kuchangia juu ya Sera za kikodi. Sera za kikodi kwa mfano, Serikali ya Awamu ya Tano ilikuwa na nia njema ya kutaka kukusanya madeni ya kodi ambayo yalikuwa yamelimbikizwa kwa muda mrefu, hiyo ni nia njema kabisa ya Serikali ya Awamu Tano. Lakini sasa sera ya kikodi imeonesha mapungufu pale ambapo Serikali ilitaka wadaiwa hawa walipe madeni yote haya ya kodi ndani ya muda maalum bila kuangalia athari za kiuchumi ambazo zingeweza kujitokeza, matokeo yake wanafanyabiashara wengi wao wakiwa wenye makampuni makubwa walilazimika kwenda kwenye taasisi za kifedha na mabenki mbalimbali kukopa pesa ili waweze kulipa hayo madeni ya kodi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande mmoja walifanikiwa kulipa madeni haya ya kodi lakini kwa upande mwingine walishindwa kurejesha ile mikopo kwenye hizo taasisi za kifedha na kupelekea sekta ya fedha kudorora na hadi baadhi ya mabenki kufungwa. Sasa sera za kikodi zinapaswa zielekeze na ziweze kuzingatia maeneo mengine ya uchumi ambayo yanaweza yakaathiriwa kwa njia moja au nyingine pale ambapo ikiwa njia za kutekeleza hilo, hata kama ni nia njema lakini pia liangaliwe. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna suala lingine ni kuhusu sera za kifedha. Sera za kifedha zinatakiwa zielekezwe katika kuhakikisha kwamba ukuaji wa uchumi unakuwa shirikishi yaani inclusive economic growth kwa ajili ya kuweza kutoa ule utata uliko kwamba sasa hivi kwenye makaratasi na takwimu ina……

(Hapa kengele ililia kuashiria kwisha kwa muda wa Mzungumzaji)