Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA:Mheshimiwa Mwenyekiti, nakushukuru kwa kunipa nafasi. Nami niungane na Wabunge wenzangu kuwapongeza Mawaziri wa Wizara hii, Mheshimiwa Lukuvi na Naibu Waziri Mheshimiwa Mabula kwa kazi nzuri wanazozifanya na kwa kweli wanastahili pongezi, tunawapongeza sana. Pia nimpongeze Ndugu yangu Katibu Mkuu Dkt. Yamungu Kayandabila na Naibu Katibu Mkuu Dkt. Kusiluka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sasa hivi tunashuhudia mabadiliko makubwa sana kwenye Wizara hii. Zamani tulikuwa na urasimu mkubwa sana wa kutoa huduma. Ukifika pale Wizarani sasa hivi unaona kabisa mabadiliko ambayo yamefanywa. Kwanza kuna sehemu imeandaliwa kwa ajili ya watu kupewa huduma na eneo lile sehemu kubwa tatizo la mteja linashughulikiwa kidigitali, kwa hiyo tunapongeza sana Wizara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile tunaona jinsi Wizara hii inavyozingatia ugatuaji. Wamepunguza shughuli nyingi makao makuu wamepeleka kwenye ngazi ya kanda na ugatuaji kwenye ngazi ya kanda si wa madaraka tu wamepeleka na fedha na rasilimali watu, kwa hiyo nawapongeza sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vile vile kwenye Wizara hii sasa tunaona jitihada ambazo zinafanywa kuziwezesha Mamlaka ya Serikali za Mitaa. Mheshimiwa Waziri amesema nini atakifanya kuziwezesha mamlaka ya Serikali za Mitaa waweze kuandaa hati wao wenyewe. Mheshimiwa Waziri tunampongeza na tunamwombea kwamba awe na nguvu zaidi na hekima ili aweze kutuletea mazuri zaidi ya hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na pongezi hizo nina mchango ufuatao mwingine. Kwanza kuhusu suala la usimamizi wa ardhi na huduma za upangaji miji na vijiji. Suala hili ni mtambuka na suala hili ni muhimu. Pamoja na mazuri yote yanayofanywa katika ngazi ya Wizara bila kuwa na watendaji wa kutosha katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa haya mazuri yote ambayo yamekuwa yameandaliwa na Wizara kule chini hayataonekana. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna changamoto kubwa ya watumishi wa sekta hii kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa. Kama nilivyosema suala hili mtambuka na Mamlaka ya Serikali za Mitaa ina nafasi kubwa sana katika utekelezaji wa yale ambayo yamepangwa Wizarani. Ili shughuli ya ardhi ishughulikiwe vizuri kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa ina vitengo vitano, lazima kuwe na mthamini (valuer), lazima kuwe na mpima (surveyor), lazima kuwe na afisa ardhi vile vile kunahitajika mrasimu ramani na town planner. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, hali ya watumishi katika Mamlaka ya Serikali za Mitaa ni ya kutisha. Kwenye jimbo langu la Nanyamba kwenye hao wote walioorodheshwa hapa hawapo. Kuna surveyor msaidizi tu ndiye anayeendesha ile idara. Sasa utakuta yote yanayoamuliwa na baraza huyu mtu peke yake hawezi kutekeleza na mwezi Agosti anastaafu. Kwa hiyo, akistaafu mwezi Agosti ile ofisi tunafunga kabisa. Kwa hiyo nashauri, huko nyuma Serikali iliona tatizo la wahasibu kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa, Wizara ya Fedha ikaomba kibali cha jumla ikaajiri wahasibu wengi ikapeleka kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa, kila Mamlaka ya Serikali za Mitaa ilipelekewa wahasibu watano.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba Wizara ya Ardhi iombe kibali cha jumla cha kuajiri watumishi watakaopelekwa kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa ili kibali hiki kikipatikana waajiriwe vijana ili wapelekwe kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa. Vijana wasomi wapo mitaani, kwa hiyo naomba Mheshimiwa Waziri aombe kibali cha jumla ili watumishi wapatikane, ili haya mazuri ambayo anayafanya kwenye ngazi ya Wizara yakafanywe kule kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa. Tusipofanya hivi itakuwa kule juu mnafanya vizuri lakini huku chini kuna malalamiko mengi na kama anavyoona kwamba gharama za watu binafsi au kampuni binafsi (private sector) bado ni za juu na wananchi wetu bado hawawezi kuwatumia. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu wa pili unahusu urejeshaji wa fedha za kodi ya matumizi ya ardhi (retention) kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa. Mimi ni Mjumbe wa Kamati ya LAAC, hoja hii imesimama kwa muda mrefu sana. Nina taarifa hapa ya CAG ya 2015/2016, CAG anasema vizuri kabisa kwamba asilimia 80 ya makusanyo ya kodi ya matumizi ya ardhi hayakurudishwa kwa halmashauri husika shilingi bilioni 6.7. Taarifa ya CAG inasema hivyo, na CAG ali-test kwenye halmashauri 71 akakuta biloni 6.7 hazijarejeshwa. Je, kwenye halmashauri zilizokaguliwa 171 kuna shilingi ngapi ambazo hazijarejeshwa?

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo naomba Mheshimiwa Waziri afanye jitihadi za makusudi kwa sababu ukiangalia ile Sheria ya Fedha za Serikali za Mitaa ya Mwaka 1982 inasema miongoni mwa vyanzo vya mapato vya halmashauri ni pamoja na kodi hii hapa. Vile vile kuna waraka ulitolewa na TAMISEMI kuhusu hiyo asilimia 30.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa hiyo kama kuna maelekezo mapya, kama hizi fedha hazitolewi basi waraka utolewe ili kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa wasiweke kama vyanzo vya mapato. Kwa sababu sasa hivi kuna maelezo mengi, ukiuliza unaambiwa kwamba Wizara haipewi fedha kutoka Hazina, lakini pili kuna maelezo mengine yalitoka katikati pale kwamba Mamlaka ya Serikali za Mitaa haziwezi kupewa mpaka ilete mpango wa matumizi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hii inashangaza kwa sababu Mamlaka ya Serikali za Mitaa wakati inapoandaa bajeti kuna kitu kinaitwa Medium Term Expenditure Frame Work (MTEF) inaonyesha activities zote ambazo zitafanywa na council kwa mwaka husika na fedha ambazo zitahusika. Kwa hiyo, sioni sababu ya kuwaambia Mamlaka ya Serikali za Mitaa walete tena mpango wa matumizi wakati kuna MTEF wa halmashauri husika. Kwa hiyo naomba hizi fedha wapewe ili waweze kutekeleza majukumu yao ambayo yapo kisheria. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, niende kwenye suala la CDA. Nichukue nafasi hii kumpongeza Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa maamuzi mazito aliyoyafanya ya kuivunja CDA, lakini pia kufutwa kwa hati miliki ya CDA na kupeleka majukumu yake kwenye Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hapo awali nikiwa mtumishi niliwahi kufanya kazi Manispaa ya Dodoma na Mheshimiwa Waziri wakati huo alikuwa Mkuu wa Mkoa wangu, aliona jinsi ambavyo CDA ilikuwa inaendeshwa kwa ubabe, ilikuwa inatengeneza kero. Tulikuwa tunatafuta eneo la kujenga sekondari lakini kuna siku alituita Mheshimiwa Lukuvi ofisini kwake tukakaa masaa matano, CDA hawataki kutoa eneo kwa ajili ya ujenzi wa sekondari. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, watoto wa Dodoma sasa hivi wanahangaika wanakwenda shule ya Mnadani, Shule ya Lukundo, ile Shule ya Sechelela mbali kabisa na nje ya Dodoma. Kata ya Kilimani hii hapa Uzunguni ikaamuliwa kwamba shule ya sekondari ya kata ijengwe Ntyuka watoto wale wanaumia kila siku kupanda ule mlima lakini kwa ubabe wa CDA kwamba hawawezi kutoa lile eneo na maeneo ambayo sisi tuliona kama Manispaa kwamba ijengwe sekondari wamepewa watu wengine tu wamejenga mahoteli na shughuli zingine. Kwa hiyo, namshukuru Mheshimiwa Rais kwa uamuzi wake wa kuivunja CDA na nashauri sasa Halmashauri ya Manispaa ya Dodoma ichukue majukumu hayo mazito na iyatekeleze.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini nina ushauri wa aina mbili kwa Wizara. Kwanza wale watumishi wa CDA wote wasirundikwe Manispaa, watakuwa na subortage kwa Mkurugenzi wa Manispaa ili aonekane kwamba hafai.

Naomba watumishi wale wasambazwe kwenye Mamlaka zingine za Serikali za Mitaa na cream iletwe Dodoma ili waweze kuchapa kazi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, lakini na sasa hivi Mamlaka ya Manispaa ya Dodoma iwezeshwe kutekeleza yale majukumu kwa sababu tukiwalaumu tu kwamba hawawezi wale kwa muda mrefu hawajafanya shughuli za ardhi, shughuli hizi walikuwa wanafanya CDA, kuna madeni, kuna viwanja ambavyo hawajapewa wenyewe waliolipia. Kwa hiyo shughuli hii sasa itafanywa na Manispaa. Kwa hiyo lazima tuwape muda manispaa waweze kuchukua majukumu hayo; tuwawezeshe, tusiwalaumu mapema ili waweze kutekeleza majukumu haya mazito kwa urahisi na hatimaye tuweze kuendeleza makao makuu ya nchi yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimalizie kwa kuunga mkono hoja na nakushukuru kwa kunipa nafasi.