Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi

MHE. SHABANI O. SHELIKINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, asante sana kwa kunipa nafasi hii na mimi nichangie hotuba iliyoko mbele yetu. Kwanza nimpongeze Waziri na Naibu Waziri kwa kazi kubwa wanayoifanya kwani Watanzania wanaiona kazi yao kubwa lakini sisi hatuna cha kuwalipa ila Mwenyezi Mungu mwenyewe ndio atajua cha kuwalipa. (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba nijikite moja kwa moja kwenye ujenzi wa nyumba za bei nafuu. Mimi niko kwenye Kamati ya Ardhi, Maliasili na Utalii, tulitembelea wakala wa kuuza vifaa vya ujenzi na ujenzi wa nyumba za bei nafuu. Kwa kweli inasikitisha sana kama kweli Serikali ina nia ya dhati kujenga nyumba za bei nafuu basi wawezeshe wakala wale, kwani wakala wale vifaa vyao wanauza bei nafuu sana, just imagine kigae kimoja kinauzwa Sh.500/= halafu ukiuliza unaambiwa bado wako kwenye utafiti. Kwa nini sasa Serikali isitenge mafungu ya kutosha kuwawezesha wakala wale ili wakasambaa kwenye mikoa hadi wilayani sambamba na hayo waendelee kufundisha vijana wetu ili waweze kupata elimu na kujiajiri? (Makofi)

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuna huu mtandao wa ILMIS. Huu mtandao ni mzuri sana lakini nimuombe Mheshimiwa Waziri Lukuvi huu mtandao usiishie Dar es Salaam tu, huu mtandao uende kwenye majiji makubwa kama Mwanza, Arusha, Tanga, Mbeya na majiji mengineyo hapa Tanzania, kwani mpango huu ni mzuri ambao utarahisisha kabisa hata ile kazi ya kupata hati au kubaini kiwanja cha mtu. Pia ikiwezekana nimwombe Mheshimiwa Lukuvi kwa heshima na taadhima mtandao huu hebu auzambaze kwa haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niingie kwenye upimaji wa ardhi. Kama Mheshimiwa Rashid Shangazi alivyosema kwamba Lushoto kuna uhaba sana wa ardhi na watu wa Lushoto wako tayari kupimiwa ardhi lakini wanapohitaji kupimiwa ardhi basi kunakuwa na figisufigisu nyingi sana. Nashindwa kuelewa tatizo liko wapi? Ukizingatia Wilaya ya Lushoto pamoja na kwamba ni ya milima, milima lakini ina watu wengi sana ambao wana uhitaji, wanahitaji hati ili waweze kukopa benki, wanahitaji pia na hati za kimila. Kwa hiyo tatizo liko wapi Mheshimiwa Lukuvi kwa wananchi wa Lushoto? Hivi kwa nini wanapata tabu kiasi hicho? Wanapohitaji kupimiwa au kupata hati inakuwa ni shida kubwa sana kiasi kwamba mpaka wawapigie watu magoti? Nashindwa kuelewa kwa ajili gani inakuwa hivyo?

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hayo huyu mtu wa shamba, mwekezaji shamba la Mnazi, huyu mtu anasema ameishika Serikali kwa hiyo hatambui viongozi zaidi ya yeye na pesa zake. Kwa hiyo nimuulize Mheshimiwa Lukuvi tatizo liko wapi hapa na yeye ameshikwa? Eeh tunataka kujua kwa sababu mtu huyu anatusumbua sana kiasi kwamba sijui yeye anajiamini vipi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nimwombe Mheshimiwa Lukuvi, nawaamini sana na dada yangu Mheshimiwa Mabula, naamini hii ni issue ndogo sana mpaka kesho naamini taarifa hii tutaipata. Tunataka mtu huyo tumjue ni nani na ana uwezo gani katika nchi hii? Mheshimiwa Lukuvi najua kazi yake, natambua uwezo wake naamini hili sasa limefika kwake sasa. Tunahitaji ardhi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo wananchi wa Lushoto kama Mheshimiwa Shangazi alisema kwamba wanahitaji sana kupima ardhi lakini kunakuwa na tabu moja kubwa sana. Sasa sijajua kwamba pale hakuna vifaa au wataalam hakuna? Mheshimiwa Lukuvi mimi ndiyo maana nikampongeza sana kwa sababu naamini kazi yake na sidhani kabisa kwamba kazi hii itamshinda. Naomba sasa wananchi wa Lushoto waweze kupata hati kwa mapema na wapimiwe kwa haraka iwezekanavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante sana.