Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Lolesia Jeremia Maselle Bukwimba

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Busanda

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. LOLESIA J. BUKWIMBA: Mheshimiwa Naibu Spika, nianze maelezo yangu kwa kumpongeza Mheshimiwa Waziri kwa hotuba yake aliyowasilisha Bungeni. Nimpongeze Mheshimiwa Naibu Waziri na watendaji wote wa Wizara. Sera ya Taifa inasema kuwa umbali wa kupata maji safi na salama usizidi mita 400 kutoka kwenye makazi. Hali halisi kwa sasa bado ni changamoto kwani wananchi wanasafiri umbali mrefu sana kilomita moja na zaidi kwa baadhi ya maeneo.

Mheshimiwa Naibu Spika, vile vile Ilani ya CCM ya mwaka 2015 – 2020 inasema hadi kufikia mwaka 2020 zaidi ya asilimia 70 ya wananchi vijijini watakuwa wanapata maji safi na salama. Leo ni mwaka 2017 ni miaka mitatu tu kufikia 2020 lakini utekelezaji hauonekani kabisa. Nimeangalia bajeti, fedha zilizotengwa katika mkoa wangu zimeelekeza tu katika kuboresha miji. Majimbo yaliyopo vijijini, sijaona mpango wowote. Je, tutawezaje sasa kufikia malengo ya asilimia 70 wakati kila bajeti hakuna mpango wowote?

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati wa majumuisho ningependa kufahamu mpango wa kupeleka maji katika Jimbo la Busanda. Kwanza tumezungukwa na Ziwa Victoria, naomba nipate mpango wa Serikali wa kutoa maji Ziwa Victoria kwenda Jimbo la Busanda.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la pili, naishauri Serikali iunde Wakala wa Maji Vijijini. Hii itasaidia utekelezaji wa miradi ya maji vijijini kama ilivyo REA. Miradi mingi ya maji vijijini tunaona inasuasua sana hasa ni kutokana na kutokuwa na usimamizi mzuri. Ni imani yangu kwa usimamizi kupitia Wakala wa Maji Vijijini utawezesha ufanisi katika utekelezaji wa miradi ya maji vijijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la tatu ni juu ya ongezeko la fedha kufikia shilingi mia kutokana na manunuzi ya petrol/diesel. Fedha hii ipelekwe kwenye Mfuko wa Maji. Vile vile tunaomba asilimia 70 ya fedha hii ilenge kuboresha miradi ya maji vijijini. Hii ni kutokana na ukweli kwamba katika bajeti iliyopita fedha hizi za Mfuko zilipelekwa kuboresha maji mijini.

Mheshimiwa Naibu Spika, tukumbuke kuwa zaidi ya asilimia 70 ya wananchi wanaishi vijijini. Tukiboresha maji vijijini tutapunguza changamoto mbalimbali za magonjwa yatokanayo na maji machafu (water borne diseases). Vile vile tutainua uchumi unaopotea kwa kufuata maji umbali mrefu.

Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya maelezo yangu naunga mkono hoja.