Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Maftaha Abdallah Nachuma

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Mtwara Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. MAFTAH A. NACHUMA: Mheshimiwa Naibu Spika, baada ya kumshukuru Mwenyezi Mungu, nashukuru ofisi na kiti chako kwa kuendelea kutenda haki juu ya mijadala ya Bunge. Katika Wizara hii ya Maji na Umwagiliaji naomba kuchangia mambo yafuatayo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mradi wa Maji Mtwara Mjini umekwama kwa nini? Ni muda mrefu hivi sasa Mtwara Manispaa haina maji ya kutosha na Serikali ilianzisha mradi wa kutoa maji Mto Ruvuma hadi Mtwara Mjini ili kuondoa tatizo la maji. Bajeti ya 2016/2017 Mheshimiwa Waziri alisema tayari fedha zimetengwa, usanifu umekamilika na taratibu za kutafuta mkandarasi zinafanyika.

Mheshimiwa Naibu Spika, jambo la kushangaza ni kwamba mpaka leo ukiuliza unapata majibu ya Mheshimiwa Waziri kuwa hakuna pesa na pesa zilitarajiwa kutoka Exim Bank ya China. Kwa nini tunadanganya umma wakati pesa hakuna? Kwa nini tumechukua maeneo ya wananchi kwa miaka mitatu hivi sasa bila kuwalipa fidia juu ya mradi huu? Kwa nini mpaka leo Serikali haina majibu ya kina juu ya suala hili?

Mheshimiwa Naibu Spika, kila siku wananchi ambao maeneo yao yamechukuliwa wanapiga simu na wanasema wamechoka, Serikali haioni kama wananchi huwa wamechukuliwa maeneo yao na kuwazuia kufanya shughuli za kimaendeleo kama vile kilimo na hatimaye kuwadumaza wananchi wa Mtwara? Mradi huu unapelekea wananchi wa Mtwara waone kuwa wanaonewa kwa kutowalipa fidia.

Mheshimiwa Naibu Spika, Miradi ya Maji Nchini; Mheshimiwa Waziri kwenye kitabu chake cha bajeti ametaja miradi mingi itakayotekelezwa kupitia bajeti hii lakini cha ajabu mradi wa kutoa maji Mto Ruvuma/Mtwara haupo kwenye orodha hii, huku ni kututenga wana Mtwara.

Mheshimiwa Naibu Spika, Maji Mbagala. Mkoa wa Dar es Salaam upande wote wa Mbagala ambako kuna watu wengi kuliko maeneo yote hakuna mtandao wa DUWASA/ DAWASCO, hali hii haikubaliki. Watu wa Mbagala wanahitaji maji safi na salama. Jambo la ajabu kuna bore holes Kimbiji ambako ni karibu na Mbagala lakini mtandao hakuna.

Mheshimiwa Naibu Spika, majadiliano na China (Exim) yanaendelea mpaka lini? Mheshimiwa Waziri anasema ili mradi wa Mtwara uanze majadiliano yanaendelea, kila mwaka anatoa kauli hii. Naomba kuuliza majadiliano haya yatakwisha lini? Kuendelea huku hakuna mwisho ili tuwapatie maji safi na salama kutoka Mto Ruvuma? Sisi Waheshimiwa Wabunge wa Mtwara Mjini na Nanyamba tumeongelea sana suala hili na Serikali haitoi majibu ya kina badala yake inasema tu fedha hakuna. Haya ni majibu rahisi wakati wananchi wamezuiwa maeneo yao.

Mheshimiwa Naibu Spika, Pesa Ndogo Zilizotengwa kwa ajili ya Mtwara Manispaa. Kutokana na mradi wa kuleta maji kutoka Mto Ruvuma kukwama mwaka 2015/2016 na 2016/2017, nilitarajia mwaka huu wa fedha Wizara ingetenga fedha kwa ajili ya mradi huu. Hata hivyo nasoma bajeti ya Mheshimiwa Waziri ukurasa wa 147 pesa zilizotengwa hazihusishi fidia na gharama za mradi huu mkubwa, bado Wizara haioneshi kama Wanamtwara wana umuhimu wa kupata maji safi na salama.