Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Willy Qulwi Qambalo

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Karatu

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. QAMBALO W. QULWI: Mheshimiwa Naibu Spika, nijielekeze kwenye eneo la uhifadhi wa mazingira na vyanzo vya maji. Ni jambo lisilopingika kuwa vyanzo vyetu vingi vya maji vimeingiliwa na shughuli za binadamu kama kilimo, utalii, ufugaji na kadhalika na hivyo kutishia uhai wa vyanzo hivyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, chemchemi za Qangded katika Bonde la Ziwa Eyasi, Wilayani Karatu ni chanzo muhimu sana kwa kilimo cha umwagiliaji ambako zaidi ya kaya 35,000 katika vijiji saba vya Kata za Baray na Mangola wananufaika.

Mheshimiwa Naibu Spika, katika miaka ya hivi karibuni chanzo hicho kimeshindwa kabisa kuwahudumia wananchi hao baada ya maji mengi kuchukuliwa na watu wachache karibu na chanzo, wanaochukua maji yote katika mashamba yao na hivyo kusababisha zaidi ya wakulima 30,000 walioko chini ya chanzo (down stream) kutokufikiwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania Mheshimiwa Majaliwa K. Majaliwa alitembelea Bonde la Eyasi na baada ya wananchi kumlilia juu ya hifadhi ya chanzo cha Qangded, Mheshimiwa Waziri Mkuu aliagiza na kutoa Kauli ya Serikali kuwa chanzo hicho kihifadhiwe kwa umbali wa hadi mita 500 na kwamba mashine zote zilizoko mtoni ziondolewe mara moja. Kauli hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu ilishangiliwa sana na wananchi wa Bonde la Eyasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kauli hii ya Mheshimiwa Waziri Mkuu haijatekelezwa hadi leo. Bado mashine za kunyonya maji zipo mtoni na pamoja na kuwa alama za mipaka ya chanzo zimewekwa majuzi, bado mipaka (beacons) haijawekwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, huku ni kumdhalilisha Mheshimiwa Waziri Mkuu, ni kuidhalilisha Serikali. Naomba sasa Mheshimiwa Waziri atakapohitimisha hoja hii awaambie wakulima wa Bonde la Eyasi wanaotumia chanzo cha Qangded ni lini watatekeleza Kauli ya Mheshimiwa Waziri Mkuu? Wizara kwa kushirikiana na wadau wavitambue na kuviwekea mipaka na kuvitangaza vyanzo hivyo vya Qangded kuwa maeneo tengefu ili kuvilinda na kuvihifadhi vyanzo vya Qangded.