Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Abdallah Haji Ali

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kiwani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. ABDALLAH HAJI ALI: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, napenda kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema na muweza wa mambo yote.

Aidha, napenda kukushukuru wewe binafsi kwa kusimamia majukumu yako kwa juhudi kubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, nikianza kuchangia katika Wizara ya Maji na Umwagiliaji ni kwamba mara kadhaa nimekuwa nikishauri juu ya mfumo mzima wa kudhibiti maji ya mvua. Nchi yetu haina uhakika wa kupata mvua za kutosha kwa kipindi cha mwaka. Aidha, baadhi ya maeneo katika nchi yetu hayapati mvua kabisa, yaani ni kame, lakini pia mvua zinazonyesha nchini kwetu bado hatujazitendea haki.

Mheshimiwa Naibu Spika, tunaambiwa kwamba Tanzania ni mabingwa wa kumwagilia bahari kwa maana kwamba mvua zinazonyesha hapa nchini na kutuletea maji mengi, tunashindwa kuyadhibiti angalau kwa kiwango kidogo na badala yake yote yanakwenda zake baharini na kupotea. Kwa kipindi kifupi maji hupotea mara moja na ukame ukarudia palepale.

Mheshimiwa Naibu Spika, ushauri wangu kwa Serikali ni kwamba Serikali ifanye juhudi ya makusudi ya kuliangalia suala la udhibiti wa maji ya mvua kwa kutafuta uwezo kwa njia tofauti ili kuweza kujenga mabwawa ya kisasa ili kuongeza na haya yaliyopo tuweze kuhifadhi maji ya mvua ili yaweze kutumika katika shughuli mbalimbali za kijamii.

Mheshimiwa Naibu Spika, dhana ya uhifadhi wa maji ya mvua ni pana sana na ina gharama sana, lakini pindi Serikali ikilikubali na kulifanikisha, litatatua changamoto nyingi za kijamii na kiuchumi. Serikali ikiwa italitilia maanani suala la uchimbaji wa mabwawa na uhifadhi wa maji ya mvua, kuna faida nyingi za kijamii na kuiuchumi ambazo zinaweza kutatua na kuondoa lawama, lakini pia na kuimarisha ustawi wa hali za wananchi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kutokana na uwepo wa mabwawa nchini, watu watapata matumizi mbalimbali ya maji majumbani kama kupikia, kufulia na matumizi mengine. Aidha, yataimarisha uchumi kwa watu kufanya shughuli za ufugaji wa samaki na kuongezea vipato vya wananchi; lakini pia kuwapatia ajira vijana. Hivyo uwepo wa mabwawa ya kutosha nchini ni ukombozi wa maisha ya watu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pia kuna changamoto kubwa ya malisho na unyweshaji maji kwa mifugo. Uwepo wa mabwawa utatupunguzia kero kubwa juu ya mifugo yetu kwa upande wa unyweshaji. Pia uwepo wa mabwawa unawasaidia wakulima katika suala zima la umwagiliaji, shughuli ambayo inawapatia faida kubwa wakulima wetu nchi nzima kwa kilimo cha mbogamboga na nyanya. Hii pia ni ukombozi mkubwa kwa wananchi juu ya upatikanaji wa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwarobaini wa kuondoa ukame na shida ya maji nchini, suala la udhibiti wa maji ya mvua kwa kujenga mabwawa ni la msingi sana. Hata hapa Dodoma mvua iliyonyesha mwaka huu; kama maji yale yangedhibitiwa, Dodoma ingekuwa ni Mkoa wa neema mwaka mzima. Ila la kusikitisha, mvua imepita na maji yamepita, nchi inarudia hali ya ukame.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali kuondokana na mazoea, tugharimike, tuhifadhi maji ili yatufaidishe kwa maendeleo.