Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Yussuf Haji Khamis

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Nungwi

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. YUSSUF HAJI KHAMIS: Mheshimiwa Naibu Spika, nachukua fursa muhimu kumshukuru Mwenyezi Mungu mwingi wa rehema mwenye kurehemu waja wake wote. Nakushukuru wewe kwa nafasi hii muhimu sana kwangu.

Mheshimiwa Naibu Spika, maji ni uhai. Kila kitu duniani kama hakuna maji basi hakuna viumbe hai. Kwa hiyo, maji ni muhimu kwa maisha na maendeleo ya binadamu kwa jumla. Takriban karibu Waheshimiwa Wabunge wote wamelalamikia maji katika majimbo yao. Wananchi wanapata tabu sana, wanakunywa maji machafu ambayo siyo salama. Akinamama wanaenda umbali mrefu sana, kwa hiyo, wanakumbana na matatizo makubwa na mengi sana. Mfano, ndoa zao ziko hatarini kuvunjika, wanabakwa pia wanadumaa katika kazi za maendeleo.

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba Serikali ione kilio cha Waheshimiwa Wabunge kwa umoja wao, Serikali iongeze bajeti ya maji kwa kupunguza matatizo haya katika Majimbo yetu. Naomba nizungumzie uhifadhi wa maji ya mvua. Pamoja na matatizo makubwa tuliyonayo ya maji, lakini bado Serikali yetu haiko makini juu ya ukusanyaji wa maji ya mvua ambayo hupotea kwa wingi sana. Mvua takriban hunyesha kwa vipindi lakini mvua zinakuwa kubwa ambazo husababisha mafuriko. Wananchi hupoteza makazi yao, mashamba yao na hata kupoteza maisha.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali ingetafuta wataalam wafanye utafiti kujenga miundombinu na mabwawa ya ukusanyaji maji katika sehemu mbalimbali katika Mikoa ya Tanzania. Maji tutakayokusanya yatakuwa akiba ambayo yatasaidia jamii katika shughuli mbalimbali za kila siku.

Mheshimiwa Naibu Spika, nizungumzie mafuriko. Mafuriko yamesababisha adha na uharibifu mkubwa sana hasa kwa wakulima. Wakulima wamepata hasara kubwa sana, mazao yao ya vyakula yamesombwa na maji, mashamba yao yamekuwa kama bahari na kwa msimu huu hawavuni chochote. Kwa hiyo, hawana makazi, hawana chakula. Naomba Serikali ifanye mitaro ya kupitisha maji kwa usalama pasipo kuleta usumbufu kwa wakulima.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, nizungumzie uharibifu wa bomba za maji. Bomba nyingi za maji hupasuka ama kutoboka, lakini huchukua muda mrefu sana pasipo matengenezo. Hivyo, hupelekea maji mengi sana kupotea na haya yanasababishwa na wataalam wa maji kubaki maofisini tu.

Mheshimiwa Naibu Spika, naiomba Serikali kuwa makini katika jambo hili. Wafanyakazi wa Maji wafanye kazi kwa ufanisi kuondoa tatizo la upotevu wa maji ovyo.