Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, awali ya yote, nianze mchango wangu kwa kuniwezesha kuchangia Wizara hii muhimu kwa ustawi wa wananchi wetu. Katika nchi yetu, tatizo la upatikanaji wa maji safi na salama bado ni sugu sana. Hata hivyo, bado Serikali haijaonesha nia thabiti ya kupambana na janga hili. Ndiyo maana hadi leo katika bajeti ya Serikali haioneshi umuhimu wa Sekta ya Maji ingawa sera inamtaka mwananchi kupata maji kwa umbali wa mita 400, lakini hadi sasa kwenye Halmashauri zetu tatizo la maji bado ni kubwa sana. Bajeti ya Wizara ya Maji haiwezi kujibu tatizo la maji nchini, kwani fedha zilizotengwa ni kidogo sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, Skimu ya Umwagiliaji ni muhimu sana kwa Taifa letu kwa hivi sasa, kwani kilimo cha kutegemea mvua kimepitwa na wakati hasa ukizingatia hali ya mabadiliko ya tabianchi. Serikali bado haijaonesha umuhimu katika sekta hii, kwani miradi mingi ya skimu ya umwagiliaji haijapewa kipaumbele, ndiyo maana hata pale mradi unapotekelezwa chini ya kiwango, Serikali haioneshi nia ya kufuatilia hatma ya miradi mingi ya umwagiliaji.

Mheshimiwa Naibu Spika, mfano, katika Wilaya ya Liwale kuna miradi mitatu ya umwagiliaji ambayo kati ya hiyo mradi wa Ngongowele umekufa kabisa japokuwa umeshatumia zaidi ya shilingi bilioni moja. Mradi huu sio watu wa Kanda wala Wizara walioonesha nia ya kujua hatma ya mradi huu na miwili iliyobaki bado nayo inasuasua.

Mheshimiwa Naibu Spika, fedha za Mfuko wa Maji mgao wake bado ni wa kiupendeleo. Sijui ni vigezo gani vinatumika kugawa miradi inayofadhiliwa na mfuko huu. Mfano, katika Halmashauri yangu ya Liwale, sasa ni miaka miwili mfululizo fedha hizi hatujawahi kupewa katika mradi hata mmoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, Liwale ni Wilaya ya zamani sana, lakini hali ya upatikanaji wa maji vijijini ni duni sana na wala sijaona juhudi za Serikali katika kukabiliana na shida hii.

Mheshimiwa Naibu Spika, mradi wa kutafuta chanzo mbadala wa maji katika Mji wa Liwale uliokuwa chini ya ufadhili wa Benki ya Dunia, fedha kiasi cha shilingi milioni 200 zilitolewa mwaka 2014, lakini hadi leo mradi huu umekwama bila maelezo yoyote toka kwa wahusika. Fedha za mradi huu zinaendelea kutumika bila kufikia lengo la kutolewa kwake. Hali ya upatikanaji wa maji katika Mji wa Liwale ni mbaya sana. Namwomba Mheshimiwa Waziri aje Liwale ajionee mwenyewe jinsi watu wa Liwale wanavyoteseka juu ya maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyosema kwenye mgao wa fedha za Mfuko wa Maji nchini, miradi ya maji vijijini nayo inakumbwa na mgao usiozingatia haki katika kuwafikia wananchi wetu. Katika Jimbo la Liwale hadi leo miradi hii imekamilika katika vijiji vitano tu kati ya vijiji 79. Hii ni ile miradi inayofadhiliwa na Benki ya Dunia. Je, ni vigezo gani vinatumika katika kugawa miradi hii? Katika kitabu cha bajeti, Liwale haijatajwa popote kuhusu miradi ya maji vijijini wala mjini.