Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

Hon. Leonidas Tutubert Gama

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Songea Mjini

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 - Wizara ya Maji na Umwagiliaji

MHE. LEONIDAS T. GAMA: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nichukue nafasi hii nikushukuru kwa kunipa nafasi ya kuzungumza, kwanza kabisa nianze kwa kushukuru.

Mheshimiwa Naibu Spika, wiki hii ndiyo nimeingia Bungeni baada ya kuwa kwenye matibabu nchini India kwa muda wa zaidi ya mwezi mmoja. Kwa hiyo, naomba nichukue nafasi hii nimshukuru sana Mwenyezi Mungu kwa kunijaalia matibabu mema, afya njema na sasa kurudi salama. (Kicheko/Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, pili, nashukuru sana Uongozi wa Spika, Naibu Spika, Katibu wa Bunge, pamoja na timu nzima ya Watumishi wa Bunge kwa huduma nzuri walizotupatia za kwenda matibabu India na kurudi salama. Mwisho, nampongeza sana Mheshimiwa Rais kwa kukubali maombi ambayo vile vile yalipitia Wizara ya Afya, yalipitia pia kwa wataalam kutoka Hospitali ya Taifa, Muhimbili ya kunipa kibali kwenda kupata matibabu na sasa nathibitisha kwamba nimerudi salama na niko tayari kuitumikia nchi yangu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, naomba nifanye kazi moja ya kuwaomba Waheshimiwa Wabunge; pamoja na maombi yenu ya kuniombea, nataka nishauri Waheshimiwa Wabunge wote tujenge tabia ya ku-check afya zetu, kwa sababu ni kweli ukinitazama nilivyo, huwezi kuamini kama afya yangu ilitetereka, lakini ni kwa sababu ya kujenga tabia ya kuangalia afya yako, wataalam wanaweza kukwambia bwana wewe unajiona mzima, lakini sio mzima. Kwa hiyo, napenda nichukue nafasi hii niwaombe Wabunge wote tujenge tabia hiyo ili kuhakikisha afya zetu zipo katika mazingira mazuri zaidi. (Makofi/Kicheko)

Mheshimiwa Naibu Spika, la pili, naomba nichukue nafasi hii niunge mkono juhudi kubwa zinazofanywa na Serikali yangu ya Awamu ya Tano chini ya Rais wetu mpendwa, Dkt. John Pombe Magufuli na Wizara mbalimbali ikiwemo Wizara ya Maji. Kazi inayofanywa na Serikali ni nzuri sana, inatia moyo na inaonesha dhahiri kwamba tunakokwenda inaelekea tunakwenda vizuri. Nawapongeza sana Mheshimiwa Waziri na Naibu Waziri; kazi yao wanayoifanya ni nzuri sana, tunawapongeza, tunaomba waendelee hivyo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niseme kidogo upande wa maji hasa kwa upande wa Wilayani kwangu. Wilayani Songea nina Kata 21. Katika Kata 21 kuna SOUWASA wanahudumia Kata 11 na Kata 10 zinahudumiwa na Halmashauri, ukiangalia mazingira ya Songea huwezi kutazamia kwa nini tuwe na tatizo la maji? Kwa sababu tuna mito ya kutosha, tuna mabonde ya kutosha, hali nzuri ya hewa na mvua ya kutosha. Kwa hiyo, maana yake naiomba sana Wizara ya Maji, hebu tujipange vizuri tuone namna gani tunaweza kuboresha huduma za maji katika Mji wa Songea. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivi sasa Halmashauri inatoa asilimia 46 tu ya kiwango cha maji kinachotakiwa kwa wananchi wa Songea, lakini wenzangu wa SOUWASA walijenga bwawa kubwa kwa ajili ya kukusanya maji, kwa ajili ya kuhudumia Mji wa Songea. Lile bwawa bahati nzuri limekamilika, lakini mpaka sasa kuna watu wanadai fidia zaidi ya miaka sita hawajapata fidia zao, naomba Wizara iniambie kuna mpango gani wa kuwalipa fidia hawa wananchi ambao wametoa maeneo yao na kuwezesha kuweka bwawa la maji na hivi sasa bwawa lile limeshaanza kufanya kazi?

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kweli siyo busara kwa watu ambao wametoa eneo ambalo linachangia huduma za maji Mjini Songea, lakini hawapati haki yao waliyostahili. Naomba Wizara…

(Hapa kengele ililia kuashiria kuisha kwa muda wa mzungumzaji)

Ahsante sana. Naunga mkono hoja.