Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

Hon. Augustino Manyanda Masele

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mbogwe

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Hotuba ya Mheshimiwa Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania wakati wa Kufungua Bunge la Kumi na Moja

MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru sana kwa kunipatia nafasi hii mchana huu ili na mimi niweze kuchangia hotuba ya Mheshimiwa Rais wetu mpendwa Dkt. John Pombe Magufuli aliyoitoa hapa Bungeni tarehe 20 Novemba, 2015. Waswahili husema, ada ya muungwana ni vitendo, Mheshimiwa Rais kauli hii ameenda nayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, Rais alipokuja hapa Bungeni alizungumzia mambo mbalimbali na kutoa mwelekeo wa Serikali yake itakavyofanya kazi. Baada ya hapo tumeona hakika kwamba anafanya kulingana na jinsi anavyosema. Tunampa hongera sana. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, niwashukuru wananchi wa Jimbo la Mbogwe kwa kuniamini kwa mara ya pili niwawakilishe katika Bunge hili. Nasema ahsate sana na naahidi sitawaangusha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu imempata kiongozi na imempata muungwana ambaye hakika anajua matatizo ya nchi hii. Sisi Wabunge na wananchi kwa pamoja tunachotakiwa kufanya ni kumuunga mkono moja kwa moja ili aweze kufanya kazi zake na tufanye lile ombi lake la kumuombea kwa Mwenyezi Mungu ili amtie moyo na nguvu aweze kuzitekeleza ahadi zote alizoziahidi na kuitendea haki Ilani ya Uchaguzi ya chama chetu, Chama cha Mapinduzi. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Rais kwenye kampeni zake na katika kauli zake amekuwa akisisitiza sana juu ya suala la kuwa na nchi yenye viwanda. Nchi yetu ili iwe na viwanda ni muhimu kuwa na umeme wa uhakika. Jambo hili linawezekana kwa sababu ameweka jembe katika Wizara hii, Waziri Mheshimiwa Profesa Muhongo ambaye kila mmoja ni shahidi wa kweli juu ya utendaji kazi wa mtu huyu. Mtu huyu tumuombee kwa Mungu aweze kutimiza ndoto zake juu ya taifa hili. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, viwanda haviwezekani bila ya kuwa na umeme wa uhakika. Ukiwa na umeme wa uhakika utakuwa na uwezo wa kuweza kuvutia wawekezaji wa viwanda kutoka ndani na nje ya nchi. Kwa ajili hiyo ndugu yangu Mheshimiwa Muhongo Mungu akutie nguvu uweze kuitendea haki nchi hii. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nchi yetu ya Tanzania kijiografia ni nchi ambayo imebarikiwa na Mwenyezi Mungu. Tunazo rasilimali mbalimbali, tunayo bahari, ardhi ya kutosha, anga la kutosha, maliasili za kila aina na wanyama wa kila aina. Kwa ajili hiyo, utajiri huu tukiutumia vizuri na tukienenda sambamba na Rais wetu, hakika tutafika haraka kwenye Tanzania ya watu wenye maisha ya kipato cha kati. Tunachotakiwa kufanya ni kupiga kazi na kushirikiana kwa pamoja kupiga vita rushwa na aina mbalimbali za uzembe.
Mheshimiwa Naibu Spika, suala la viwanda bila mawasiliano haliwezekani. Kwa maana hiyo, niiombe Serikali itilie mkazo ujenzi wa bandari katika bahari zetu, katika maziwa yetu na kuimarisha reli. Reli ndiyo usafiri wa uhakika wa kuweza kusafirisha mizigo mingi inayotoka nje ya nchi na inayotoka ndani ya nchi kwenda nje ya nchi. Ili reli yetu iweze kufanikiwa kufanya kazi zake vizuri basi ni vizuri tukawa na treni, ikiwezekana kama umeme utakuwepo ziwepo reli za umeme. Maana umeme ukishakuwa wa uhakika maana yake tutakuwa na treni zinazoendeshwa kwa umeme, zitapunguza muda wa kusafirisha bidhaa mbalimbali kutoka Bandari ya Dar es Salaam na kwenda katika nchi za jirani. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, pia niishauri Serikali itekeleze kwa wakati ujenzi wa reli ya kutoka Isaka - Msongati - Kigali nchini Rwanda. Kwa sababu nchi yetu iko vizuri kijiografia na wenzetu hawa wa Rwanda, Burundi, Mashariki ya Congo tumepakana nao. Kwa maana hiyo uchumi wa nchi hizi unaweza ukainufaisha nchi yetu kwa uzuri sana.
Mheshimiwa Naibu Spika, nije katika suala zima la elimu. Nchi yetu ili iweze kuendelea kwa uhakika ni vizuri tukawa na vijana wasomi ambao watahusika katika uendeshaji wa viwanda. Kwa maana hiyo suala la teknolojia ni jambo la muhimu na la msingi sana. Kwa maana hiyo, watu wa COSTECH, kwa maana na Commission for Science and Technology tunatakiwa tuwape nguvu na kuwapa kipaumbele ili waweze kutoa vijana ambao watakuwa wameelimika vizuri na katika vyuo vikuu mbalimbali masomo ya sayansi tuyape kipaumbele. Tutakapokuwa na wasomi wazuri hata viwanda vitakuwa vinaweza kuajiri watu ambao wana weledi wa kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe tu mfano, katika nchi hii migodi imekuwa inafanya kazi vizuri kutokana na wataalamu wa Kitanzania lakini management tu ndiyo unaweza ukakuta wamepata kutoka nje. Kwa mfano, katika mgodi wa Mkoa wa Geita pale GGM, Watanzania wengi wanafanya kazi pale na wanafanya kazi nzuri. Hata Mgodi wa Tulawaka ambao ulichukuliwa na Serikali, Watanzania wanafanya kazi pale ya uzalishaji wa dhahabu, kwa kweli inaonekana Watanzania tunaweza, kwa maana hiyo tujipe moyo na tujitahidi tu kujiamini kwamba tunaweza. (Makofi)
Mheshimiwa Naibu Spika, niombe kwa mara nyingine nchi hii imejaliwa kuwa na neema ya maji basi maji ya Ziwa Victoria ambayo yamefika katika Wilaya ya Kahama kutoka Mwanza, tunaiomba Serikali itoe fedha kwa ajili ya kuyafikisha katika Wilaya yetu ya Mbogwe ambayo iko umbali wa kilomita 60 tu kutoka maji ya Ziwa Victoria yalipofikishwa. Itakuwa ni jambo la kheri na inaweza ikatusaidia kukabiliana na mabadiliko ya tabianchi ambayo mara zote yamekuwa yakisababisha ukame katika maeneo mbalimbali ya nchi hii. Kwa hiyo, kupatikana kwa maji ya Ziwa Viktoria katika Wilaya yetu ya Mbogwe inaweza ikawa ni ufumbuzi wa muda mrefu wa tatizo la maji.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, niiombe Serikali kwa wakati wake izisaidie halmashauri, wilaya na mikoa mipya ili ziweze kujenga ofisi zake kwa wakati na tuweze kupiga hatua kama ilivyo katika mikoa mingine.
NAIBU SPIKA: Mheshimiwa Masele ahsante.
MHE. AUGUSTINO M. MASELE: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru na naunga mkono hotuba ya Mheshimiwa Rais. (Makofi)