Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Shabani Omari Shekilindi

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lushoto

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. SHAABANI O. SHEKILINDI: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa nipongeze Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi hasa kwa Waziri na timu yake yote kwa hotuba yao nzuri ambayo imejaa matumaini makubwa ya Watanzania hasa wakulima.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niendelee kuipongeza Wizara kwa kupunguza tozo hasa kwenye zao la kahawa. Serikali kutoa tozo 17 siyo kitu cha mchezo. Sambamba na hayo, Wilaya ya Lushoto inalima kahawa na kutoa tani zaidi ya 300 kipindi cha nyuma, lakini sasa hivi ni tani 40 tu ndiyo zinazopatikana. Hii yote ni kulitupa kabisa zao la kahawa ambalo linaipatia Serikali pesa za kigeni na zao hili Wilaya ya Lushoto limeonekana ni zao ambalo linalimwa na wazee tu na siyo vijana, yote hayo ni kutowawekea vijana miundombinu mizuri na kuhamasisha kupenda kahawa na zaidi vijana kukimbilia mijini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na hayo Idara ya Kilimo ilikuwa inapanda miche ambayo walikuwa wanaipata au kununua TACRI N39, miche hii inakaa muda wa miaka mitatu inazaa na kila mbuni wa mbegu hii unatoka kilo tatu lakini Idara ilishindwa kutokana na ukosefu wa fedha. Kwa hiyo, niishauri Serikali yangu itoe tamko katika Halmashauri zile pesa za kahawa wanazotoza ushuru wazirudishe zinunue miche ile ili kuokoa zao la kahawa linalokufa katika Wilaya ya Lushoto.

Mheshimiwa Mwenyekiti, huwezi kutenganisha Wizara ya Kilimo na Wizara ya Maji pamoja na Wizara ya Ujenzi. Kule Lushoto kuna mvua nyingi zinazoendelea kunyesha na zimeleta madhara makubwa na kuharibu miundombinu ya barabara pamoja na madaraja kuvunjika. Hivyo, kusababisha mpaka sasa hivi ninavyoandika mchango wangu huu mazao ya wakulima yanaozea shambani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hivyo niishauri Serikali yangu itoe pesa za dharura ili kwenda kutengeneza barabara zile ili wananchi wasiendelee kupata hasara ya mazao yao maana ukitegemea Halmashauri zetu hazina pesa za kutengeneza barabara zile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hayo kuna barabara ya mchepuo ya kuanzia Dochi – Ngulwi hadi Mombo barabara ile niliisemea sana kuwa iwe mbadala lakini mpaka leo hakuna hatua yoyote iliyochukuliwa na kama ingetengenezwa kusingekuwa na upatikanaji wa hasara ya mazao ya wakulima. Kwa hiyo, niiombe Serikali yangu itengeneze barabara ile.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu wakulima wa chai Mponde, takribani miaka minne sasa kiwanda kile cha chai kimefungwa, kwenye hotuba inaonesha kiwanda kile kimepewa mfuko wa jamii (LAPF) lakini mpaka sasa mfuko huo umefika mara moja tu kuona kiwanda kile. Kwa heshima na taadhima naiomba Serikali yangu hasa Waziri wa Kilimo aende Lushoto eneo la Mponde ili akaone wakulima wanavyonyanyasika na chai yao. Wakulima wale wamefikia kula mlo mmoja kwa siku na kushindwa kulipa mpaka bili za umeme.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo cha mbogamboga; kilimo hiki kimetupwa pembeni kabisa wakati kilimo hiki ndicho kinachochangia mapato makubwa katika Halmashauri. Naishauri Serikali yangu iwaandalie wakulima hawa miundombinu ili waweze kulima kilimo cha umwagiliaji. Kwa mfano, mvua hizi zinazoendelea kunyesha kungejengwa mabwawa yangenufaisha wakulima wetu na kulima kilimo chenye uhakika na chenye tija kuliko ilivyo sasa, mvua zinaendelea kuharibu miundombinu ya barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba niishauri Serikali yangu ifufue kiwanda cha mbolea Tanga ili kuwezesha mbolea kupatikana kwa urahisi na kwa bei nafuu. Naishauri Serikali yangu ipeleke Benki ya Wakulima Mikoani hadi Wilayani kwa sababu huko ndiko kwenye wakulima au wahitaji kuliko Benki hiyo kuwa Dar es Salaam.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naunga mkono hoja.