Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Abdallah Dadi Chikota

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nanyamba

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. ABDALLAH D. CHIKOTA: Mheshimiwa Mwenyekiti, napenda kumpongeza Waziri na Naibu Waziri kwa kazi nzuri wanayoifanya. Aidha, pongezi za kipekee ziwaendee kwa namna wanavyosimamia tasnia ya korosho tangu waingie Wizarani.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mchango wangu utajikita katika maeneo yafuatayo, kwanza ni pembejeo za korosho. Naipongeza Serikali kwa uamuzi wake wa kutoa pembejeo za ruzuku kwa asilimia 100. Matarajio yangu ni kuwa pembejeo hizi zitakuwa motisha kwa wakulima wa korosho na hivyo kuongeza uzalishaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, hata hivyo, kama ilivyokuwa inafanyika huko nyuma pembejeo hizi hazitoshelezi mahitaji ya pembejeo kwa wakulima wa korosho. Wakulima watalazimika kununua zingine kwa bei ya soko ili kukidhi mahitaji yao. Kiasi hiki nacho kisiachwe hivi kuwe na utaratibu wa manunuzi kama itakavyofanywa kwenye mbolea. Tusipofanya hivyo mkulima atapata pembejeo kiasi ya ruzuku na nyingi kununua kwa bei ya juu, hivyo atailaumu Serikali kwa utaratibu huu badala ya kupongeza.

Mheshimiwa Mwenyekiti, utendaji kazi wa Maafisa Ushirika. Kumekuwa na malalamiko mengi juu ya utendaji kazi wa Maafisa Ushirika hususan katika tasnia ya korosho. Maafisa hawa baadhi yao hushirikiana na viongozi wasio waadilifu wa vyama vya ushirika ili kufanya ubadhirifu kwa fedha za wakulima. Naishauri Serikali kupitia Tume ya Ushirika na Wizara kufuatilia utendaji kazi wa Maafisa hawa ili wale ambao siyo waadilifu wachukuliwe hatua ya kinidhamu kusafisha uozo uliopo katika kada hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo cha mihogo. Mikoa ya Mtwara na Lindi, inazalisha kiasi kikubwa cha mihogo lakini wakulima wanakata tamaa kwa sababu ya bei ndogo ya zao hili sokoni. Naishauri Serikali kutumia fursa iliyopatikana hivi karibuni ya kuingiza muhogo wetu nchini China kwa kusimamia vizuri taratibu za soko la zao hili ili mkulima apate bei ya juu itakayomshawishi kuzalisha zaidi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, dosari zilizojitokeza katika mfumo wa stakabadhi ghalani kwa msimu 2016/2017; msimu wa mwaka huu, 2016/2017 kulikuwa na mafanikio makubwa ya marekebisho ya mfumo huu. Hata hivyo, kuna dosari zifuatazo:-

(i) Kuchelewa malipo kwa wakulima na hivyo kuleta manung’uniko yasiyo ya lazima;

(ii) Wakulima kulipwa fedha tofauti na bei iliyouzwa kwenye mnada, kama korosho zilizouzwa kwa kilogramu Sh.3,800, wakulima wanalipwa Sh.3,400 bila maelezo yoyote; na

(iii) Wanunuzi kupanga bei hivyo bei mnadani kushuka siku hadi siku.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri Serikali ifanyie kazi dosari hizi ili kuimarisha mfumo wa stakabadhi ghalani.