Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Omary Tebweta Mgumba

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Morogoro Kusini Mashariki

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. OMARY T. MGUMBA: Mheshimiwa Mwenyekiti, nashukuru kupata nafasi hii ili niweze kutoa mchango wangu katika Wizara hii muhimu kwa uchumi wa Watanzania wengi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pamoja na mchango wangu wa mdomo, niko hapa katika kuongeza mchango wangu huo wa awali nilioutoa kwa kuchangia kwa mdomo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na umuhimu wa viwanda nchini na kutokana na umuhimu wa ajira na fedha za kigeni na ushindani uliopo katika soko la kimataifa, naomba kuishauri Serikali kama ifuatavyo kwa kuongezea katika ule mchango wa mdomo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali kukutana na wawekezaji wa ndani wa kubangua korosho haraka iwezekanavyo ili kutambua matatizo wanayowakabili hususan kushindwa kupata malighafi, kushindwa kubangua korosho kutokana na uwezo wa viwanda vyao na wengine kufunga na kuhamia nchi za jirani kama Msumbiji na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa kuwa tunayo makampuni ya ndani kama vile ETG, Sunshine Group, Hyseas, MECT na hata yale yaliyofungwa kama vile Olam (T) Ltd., Buko Agro Focus, Micronix, Premier Cashew, Lindi Farmer na kadhalika.

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kukutana nao, Serikali itabaini wana matatizo gani na aina ya msaada gani wanahitaji kutoka Serikali ili Serikali ije na mipango, sera na mikakati ya kuweza kubangua korosho zetu ndani ya nchi ili kuongeza thamani ya korosho zetu, kutengeneza thamani ya korosho zetu, kutengeneza ajira kwa vijana wetu na kuongeza mapato ya Taifa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile naishauri Serikali kuwapa kipaumbele wawekezaji wa ndani wa kuchakata mazao ya kilimo hususan wabanguaji wa korosho katika mnada wa Stakabadhi Ghalani kwa kuwa unaweza kushindana na wabanguaji wa nje na wafanyabiashara wa korosho ghafi kwenda nje, sababu mataifa ya nje wanatoa ruzuku kwa wafanyabiashara hao na gharama za uendeshaji ziko chini katika nchi ya India, Brazil na Vietnam na kusababisha korosho inayobanguliwa nchini kuwa na gharama kubwa na kusababisha kuwa na bei ya juu katika soko la kimataifa na kukosa ushindani wa soko.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia naomba Serikali itoe kipaumbele kwa wawekezaji wa ndani kupata korosho katika minada ya mwanzo ili kupata korosho bora ambazo zina viwango vikubwa vya ubora kabla ya zile korosho za mwanzo zinazoathiriwa na mvua.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali kuongeza export toka asilimia 15 mpaka asilimia 20 na hili ongezeko kwenda kuwapa ruzuku wabanguaji wa ndani na kuvutia wawekezaji wengi zaidi na kutengeneza ajira na kuongeza thamani ya bidhaa zetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kutokana na sababu za kihistoria na kwa sababu za ushindani wa soko la korosho katika soko la dunia, naishauri Serikali kutokujiingiza tena katika biashara ya kubangua korosho. Kama tulivyojenga viwanda 11 mwishoni mwa miaka ya 1970 vya kubangua lakini tulishindwa na kuua kabisa zao la korosho.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hivyo kwa sababu suala hapa siyo kubangua tu korosho, suala la msingi ni soko la kuuzia korosho zilizobanguliwa katika soko la dunia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, pia lengo mojawapo la kubinafsisha na kupata mbinu na masoko ya kimataifa, soko la kimataifa lina ushindani mkubwa kwa kuwa walaji wanataka au wanapenda kununua kutokana na brand na jina la makampuni waliyoyazoea. Sasa wasiwasi wangu tutawekeza lakini tunashindwa kuuza katika masoko hayo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nashauri kwamba baada ya kuwekeza kama Serikali, ni bora kuwapa ruzuku na vivutio wawekezaji wa kubangua korosho nchini ili kupunguza gharama za uzalishaji ili kuweza kushindana na kwa kuwa wengi wana masoko katika masoko ya kimataifa, itakuwa ni rahisi kushindana kuliko Serikali au Bodi ambayo haina wateja kwa sasa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mwisho na siyo kwa umuhimu, nataka kupata kauli ya Serikali kuhusu ununuzi wa ufuta mwaka huu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hili kwa sababu tarehe 9 Mei, 2017 Mkuu wa Mkoa wa Lindi katika kikao cha wadau wa zao la ufuta alitoa tamko la soko la ununuzi wa ufuta msimu wa mwaka 2017/2018, utakuwa wa Stakabadhi Ghalani. Pia tarehe 17 Mei, 2017 Baraza la Madiwani la Halmashauri ya Kilwa ambalo ni sehemu ya Mkoa wa Lindi limekaa na kutoa tamko nalo kuwa mwaka huu soko la ufuta litakuwa ni soko huria.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa kuwa hizo ni kauli kutoka kwa viongozi wa Serikali halali, Serikali Kuu na Serikali ya Halmashauri ambazo zimeleta mkanganyiko mkubwa kwa wakulima na wafanyabiashara, ukizingatia msimu uko karibu kuanza na makampuni yameshaajiri wafanyakazi, mawakala na kuchukua maghala ya kukusanyia ufuta na kusababisha taharuki kubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, namwomba Mheshimiwa Waziri atakapokuja kufunga hoja yake, aje atuambie nini kauli ya Serikali kuhusu mfumo wa ununuzi wa ufuta mwaka huu, utakuwa ni mfumo upi? Wa soko huria au stakabadhi ghalani?

Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya kusema hayo, naunga mkono hoja. Ahsante.