Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Zuberi Mohamedi Kuchauka

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Mwenyekiti, kwanza kabisa naomba nianze kwa kumshukuru Mungu kwa kunipa uzima na kuweza leo kuandika mchango wangu kwenye Wizara hii.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kilimo ni sekta muhimu sana katika nchi yetu japo Mheshimiwa Waziri kwenye hotuba yake anasema kilimo kinaajiri asilimia 65.5 ya Watanzania wote. Jambo hili siyo kweli kwani Watanzania wengi wako vijijini na wanategemea kilimo kwa uchumi wao. Hivyo, kilimo huajiri zaidi ya asilimia 75 ya Watanzania, lakini kwa masikitiko makubwa ni kwamba sekta hii haijapewa umuhimu unaostahili, ndiyo maana Wizara hii imetengewa fedha kidogo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tatizo kubwa katika sekta ya kilimo ni uhaba wa masoko ya uhakika na bei ya mazao husika. Hamasa pekee ya kukuza kilimo ni bei nzuri ya mazao na soko la uhakika. Vilevile miundombinu ya barabara ni muhimu sana katika kukuza kilimo nchini, kwani kuna mazao kama vile viazi, nyanya na matunda yanashindwa kulifikia soko kwa kukosa barabara.

Mheshimiwa Mwenyekiti, zao la ufuta kwa sasa linalimwa katika maeneo mengi katika nchi yetu. Hivyo ni wakati sasa Bodi ya Mazao Mchanganyiko ikatazamwa upya na ikiwezekana zao la ufuta likaundiwa bodi yake ili kuwapatia tija wakulima kwani hadi sasa tatizo kubwa la
ufuta ni uhakika wa masoko hasa kwenye mikoa ya Kusini (Lindi na Mtwara).

Mheshimiwa Mwenyekiti, vilevile Serikali ingetilia mkazo sana ili mazao haya yasindikwe nchini badala ya kuendelea kuuza mazao ghafi.

Mheshimiwa Mwenyekiti, mgao wa chakula cha njaa ni bora ukazingatia mahitaji na kufuata jiografia ya nchi yetu. Mfano, Mkoa wa Lindi tunakuwa na uhaba mkubwa wa chakula kati ya miezi ya Desemba hadi Aprili. Hivyo, kuwapelekea chakula mwezi Mei ni sawa, kwani kipindi hiki huwa ni cha mavuno kwa wakulima wengi na shida ya chakula huwa imeisha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kama ilivyo kwa mgao wa chakula cha msaada, mgao wa pembejeo za kilimo ni lazima uendane na mazingira halisi, kwani vipindi vya msimu wa mvua haulingani nchi nzima. Mfano, kwa Mkoa wa Lindi, mazao ya nafaka hupandwa mwezi Desemba hadi Januari na kwa zao la korosho uwekaji wa dawa huanza kati ya mwezi Mei hadi Julai. Hivyo, pembejeo ya zao la korosho zinatakiwa kuwafikia wakulima kati ya mwezi Machi na Aprili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, sekta inayotegemewa zaidi katika usindikaji kwa mazao ya kilimo ni sekta binafsi, lakini Serikali haijaonesha dhamira thabiti ya utekelezaji wa jambo hili. Wawekezaji wengi wanashindwa kufanya hivyo, kwani gharama za uzalishaji hapa nchini ni kubwa sana na hii inatokana na wingi wa mamlaka zinazosimamia jambo hili. Kwa mfano, TFDA, TBS, OSHA, EWURA na kadhalika. Kodi ni nyingi sana hapa nchini, punguzeni kodi kuvutia wawekezaji.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nia njema ya kuwa na Vyama vya Ushirika nchini haijatusaidia sana, kwani elimu juu ya ushirika haijatosha, hivyo kupelekea Vyama vya Ushirika kuwa mzigo wa wakulima nchini. Vyama vingi vya ushirika badala ya kukuza masoko ili kusaidia wanachama wao, wenyewe ndiyo vimekuwa kikwazo kwa ustawi wa wakulima, ushindani wa kibiashara katika masoko ya wakulima hakuwapi tija viongozi wa ushirika, hivyo wao huwakumbatia wanunuzi wachache kwa manufaa yao binafsi na siyo ushirika kwa ujumla.

Mheshimiwa Mwenyekiti, katika Wilaya ya Liwale tumepata mwekezaji wa zao la alizeti na yuko tayari kujenga kiwanda na uchujaji, lakini hadi leo mwekezaji huyu bado anazungushwa kupata ardhi. Japo Halmashauri ya Liwale ilishampatia ardhi ya kutosha, lakini Kamishna wa Ardhi bado anakuwa na kigugumizi katika jambo hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Wana-Liwale tunaomba mwekezaji huyu apatiwe ardhi ili Liwale tuweze kukuza ajira na uchumi wa Halmashauri yetu.