Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

Hon. Cecilia Daniel Paresso

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

2

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Ofisi ya Rais (TAMISEMI, Utumishi na Utawala Bora) kwa Mwaka wa Fedha 2016/2017.

MHE. CECILIA D. PARESSO: Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza Mfuko wa TASAF; Fedha hizi ni mkopo toka World Bank kiasi cha dola za Kimarekani 220,000,000 ili kusaidia kaya maskini nchini. Kaya hizo kulingana na utofauti wa mahitaji, hupewa kati ya sh. 20,000 hadi sh. 62,000 kila baada ya miezi miwili.
Mheshimiwa Naibu Spika, mpango huu ni wa miaka mitano, je, Serikali imejipangaje kufanya mradi huu uwe endelevu? Je, Serikali itaweza kugharamia mradi huu pindi muda wa mradi kwisha ukifika?
Mheshimiwa Naibu Spika, pili, Serikali imekuwa na mwenendo wa kuanzisha miradi na Mifuko mingi bila kuwa endelevu na kutoleta tija inayotakiwa. Mfano wa Mifuko iliyoanzishwa ni pamoja na Mabilion ya JK, Mfuko wa Wanawake na Vijana (Halmashauri za Wilaya), TASAF, Mfuko wa Dhamana ya Mikopo, Mfuko wa Amana ya Ubinafsishaji na sasa shilingi milioni 50 kila kijiji. Kwa nini Serikali haioni umuhimu wa kubadili mtindo huu wa kutoa fedha mikononi mwa wananchi kwani kwa kufanya hivyo haiwezi kuondoa umaskini au kuboresha maisha yao, umuhimu ungewekwa kwanza kuboresha huduma muhimu za kijamii kwa kiwango cha juu na ndipo tuwaze mpango huo wa kutoa fedha kwa wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, je, katika Mifuko hiyo tathmini ya kina imefanywa ili kupima matokeo yaliyotarajiwa? Ni kwa kiwango gani Mifuko hiyo imekuwa endelevu? Serikali haioni umuhimu wa kuachia sekta binafsi ifanye na kutekeleza mpango huu na Serikali ibaki kama mdhibiti? Nashauri Serikali ijipime upya na kuacha kufanya mambo au maamuzi kwa mazoea.