Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Innocent Sebba Bilakwate

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kyerwa

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

1

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. INNOCENT S. BILAKWATE: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote nimshukuru Mungu kwa kupata nafasi hii ya kuchangia Wizara hii muhimu sana kwa Watanzania.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nichukue nafasi ya kipekee kumshukuru Mheshimiwa Rais, Mheshimiwa Waziri na watendaji wote kwa kutimiza ahadi ya kuondoa kodi/tozo ambazo zilikuwa zinamdidimiza mkulima. Mheshimiwa Rais wetu kila anapoahidi lazima atekeleze, namshukuru sana.

Mheshimiwa Mwenyekiti, Wizara ya Kilimo ndiyo uti wa mgongo wa Taifa letu, tunapoongelea Tanzania ya viwanda na kwenda kwenye uchumi wa kati lazima tuwekeze nguvu yetu kwenye kilimo cha kisasa, kilimo kilichofanyiwa utafiti, kilimo chenye kumuwezesha mkulima kupata mbegu bora, kilimo ambacho kitamuwezesha Mtanzania kupata soko la uhakika lazima tuweke miundombinu wezeshi kwa wakulima wetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nasema hayo kwa sababu Watanzania zaidi ya asilimia 65 ni wakulima. Pamoja na hayo ukweli ni kwamba sekta hii imesahaulika kabisa hasa hasa maeneo ya vijijini ambako wakulima wamekata tamaa. Kilimo ndio uchumi wa Taifa, ninaamini tukiwekeza nguvu yetu kwenye kilimo Taifa letu litainuka kwa muda mfupi. Taifa letu limejaliwa maji mengi sana yaliyo ardhini lakini pia tuna vipindi vingi vya mvua, karibu nchi nzima tunapata mvua ya kutosha.

Mheshimiwa Mwenyekiti, tunaipongeza Serikali kwa kodi na tozo mbalimbali zilizoondolewa kwenye mazao. Hata hivyo bado zipo kodi nyingine ambazo hazijaondolewa. Niombe Serikali kuziondoa ili mkulima aweze kufaidi bei nzuri za mazao. Pia niiombe Serikali kutoa bei elekezi kwa kila zao kila mwaka.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba niishauri Serikali kujifunza katika mataifa mengine ambayo mataifa hayo ni yenye ukame, lakini mataifa hayo yametumia kilimo cha umwagiliaji ambacho kimeinua mataifa hayo yamepaa sana kiuchumi kupitia sekta hiyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, niongelee ufugaji, kama tunataka kuondoa migogoro mingi ya wakulima na wafugaji lazima tuhakikishe tunalinda maeneo ambayo yalitengwa kwa ajili ya wafugaji na wakulima ili wananchi wetu wasiendelee kuuana na kuondoa chuki kati yao ambayo inaendelea kukua na kuleta matatizo makubwa.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naongelea hili kwa sababu maeneo mengi yaliyotengwa yamevamiwa na watu, Serikali ipo na inaiona migogoro hii ambayo mpaka leo hii ni mikubwa. Nasema haya nikiwa na ushahidi, kwenye Jimbo langu Serikali ilitenga maeneo ya wafugaji, yakatangazwa kwenye Gazeti la Serikali na kupewa GN. 620 ya mwaka 1987, lakini maeneo hayo yamevamiwa na matajiri na kuzungushia uzio na tayari wamepatiwa hatimiliki ya miaka 99, Serikali imekaa kimya wafugaji wanateseka hawana maeneo ya kufugia.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nataka Mheshimiwa Waziri kulifuatilia jambo hili ambalo limeleta mgogoro mkubwa Jimboni kwangu. Pia nataka kujua eneo ambalo lilitangazwa na Serikali na kupewa GN linawezaje kubadilishwa matumizi bila tangazo lingine la kubadilisha tangazo la kwanza? Tusipomaliza migogoro hii italeta matatizo makubwa kwa Taifa letu.

Mheshimwia Mwenyekiti, baada ya kusema hayo naunga mkono hoja.