Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

Hon. Abdallah Haji Ali

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Kiwani

Contributions

nil

Answers

nil

Commettees

0

Ministries

nil

Makadirio ya Mapato na Matumizi ya Serikali kwa Mwaka wa Fedha 2017/2018 – Wizara ya Kilimo, Mifugo na Uvuvi

MHE. ABDALLAH HAJI ALI: Mheshimiwa Mwenyekiti, awali ya yote namshukuru Mwenyezi Mungu muweza wa mambo yote. Pili, nakushukuru wewe binafsi kwa umahiri wa kazi yako ya hapa Bungeni.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naanza mchango wangu juu ya suala zima la uvuvi. Uvuvi hapa Tanzania ni sekta ambayo ikiwekezwa vizuri inaweza ikatoa mchango mkubwa sana katika Taifa hili.

Mheshimiwa Mwenyekiti, nchi yetu imebarikiwa kwa kuwa na eneo kubwa la bahari, mito, maziwa na eneo kubwa la mabwawa ambayo maeneo hayo yamesheheni rasilimali kubwa ya samaki na mazao mengine ya baharini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahari ni kama shamba lililosheheni samaki wengi wa kutosha, shamba ambalo halihitaji mbolea, madawa wala halihitaji pembejeo ya aina yoyote.

Mheshimiwa Mwenyekiti, bahari yetu ni shamba linalotaka kuvunwa tu na mazao yake ni muhimu na ni bidhaa unayoweza kuuza duniani popote. Kwa fursa hii tuliyoipata kutoka kwa Mwenyezi Mungu kwa kuwa na bahari kubwa yenye samaki wengi hatukuwa na sababu yoyote kuwa soko la kununua samaki kutoka nchi nyingine. Hata hivyo, ni ukweli usiopingika kwamba Tanzania kweli ni soko la nchi nyingine kama Afrika ya Kusini, China na nchi nyingine kwa kununua samaki na kutumika hapa kwetu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, upatikanaji wa samaki baharini ni pamoja na kuwepo dhamira ya makusudi ya Serikali ya kuweka miundombinu ya kisasa na ya uhakika. Nipende kusema kwamba katika eneo hili Serikali haijaonesha utayari kwa kuifanya sekta ya uvuvi kuwa mchangiaji mkubwa kwenye pato la Taifa. Hii ni kwa sababu hatuoni juhudi kubwa ya Serikali kutayarisha miundombinu sahihi ya kumudu uvuvi kama vile zana za kisasa zenye uwezo mkubwa wa kuvua bahari kuu, lakini pia ujenzi wa bahari ya uvuvi, vyuo vya uvuvi vitakavyotoa wahitimu wenye uwezo mkubwa lakini pia uwepo wa viwanda ili samaki wakivuliwa waweze kushughulikiwa ipasavyo.

Mheshimiwa Mwenyekiti, eneo la sekta ya uvuvi kama Serikali itachukulia umuhimu wa kipekee ndio mwarobaini utakaolisaidia Taifa kuongeza mapato na kutoka katika hatua hii na kulisogeza Taifa mbele katika nyanja mbalimbali. Sekta hii ikipewa fursa pia itaweza kutoa fursa nyingi za ajira kwa Watanzania na kutoa unafuu wa maisha kwa kupunguza umaskini.

Mheshimiwa Mwenyekiti, naishauri Serikali iitendee haki neema ya uvuvi na kuitendea haki neema hii ya bahari tuliyonayo tunaweza kuondokana na umaskini wa kipato cha mtu mmoja mmoja na Taifa kiujumla wake. Namwomba Mheshimiwa Waziri japo kwa uchache atupe maelezo ya kina kuhusu uvuvi, Serikali imejipangaje?